banner

Friday, September 25, 2020

SERIKALI YATUMIA BIL 3.29 KUKARABATI SHULE ZA MSINGI


 

NA MWANDISHI WETU

SERIKALI imetumia shilingi bilioni 3.29 kukarabati na kugharamia shughuli za utawala, michezo, mitihani na posho kwa maafisa elimu kata na walimu wakuu kuanzia mwaka wa fedha 2015/2016 hadi 2019/2020.

Fedha hizo zimetolewa na serikali kupitia mpango wa elimu bila malipo unaotekelezwa na Serikali ya Rais John Pombe Magufuli ambao hadi sasa umezinufaisha pia shule za sekondari 23.

Hayo yameelezwa jana na Waziri Mkuu. Kassim Majaliwa ambaye pia ni Mjumbe wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) katika majukwaa ya kisiasa wilayani Ukerewe ambako amefika akiwa katika mfululizo wa ziara zake nchi nzima za kumnadi mgombea urais wa CCM, Rais John Magufuli.

Waziri Mkuu Majaliwa amesema katika utekelezaji wa mfumo wa uboreshaji wa miundombinu ya shule wa lipa kutokana matokeo (EP4R) ulioanza kutekelezwa 2015 hadi 2020, sh milioni 309 zilitolewa kwa ajili ya kukamilisha ujenzi wa miundombinu ya madarasa, vyoo na ofisi kwa shule mbalimbali zikiwemo Kalandero, Murutunguru na Kakerege.

Alisema kiasi kingine cha sh milioni 873 zilitolewa kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu ya madarasa, vyoo na maabara kwa shule za sekondari mbalimbali nchini zikiwemo Bukongo, Pius Msekwa, Bwisya, Muruti na Lugongo.

Ziara hiyo ya Waziri Mkuu Majaliwa ilimfikisha katika Kisiwa cha Bwisya kilichoko Kisiwa cha Ukara ambako alitembelea Kituo cha Afya cha Bwisya na kukagua wodi ya wanaume na ya Wazazi.

Kabla ya kukagua kituo hicho, Waziri Mkuu Majaliwa alifika kwenye mnara wa kumbukumbu ya watu waliokufa kwenye ajali ya kivuko cha MV Nyerere, Septemba 20, 201  ilikofanyika ibada fupi ya kuwaombea marehemu ikiongozwa na Padre Peter Paul wa Parokia ya Nyamwaga, Ukere na Sheikh Mudhakiru Maguza wa Msikiti wa Bwisya

No comments:

Post a Comment