banner

Wednesday, September 23, 2020

AJIRA ZAIDI YA 2,000 ZAPATIKANA WILAYA YA SIHA MKOANI KILIMANJARO



NA PIUS NTIGA, SIHA

 ZAIDI ya ajira 2,000 zimepatikana Wilaya ya Siha mkoani Kilimanjaro katika kipindi cha miaka mitano.

 Nyingi kati ya ajira hizo zinahusisha miradi mbalimbali ukiwemo mradi mkubwa wa Shamba la Mwekezaji la Maparachichi unaojulikana kwa jina la Africado ambalo limetoa nafasi za kazi kwa wananchi wengi wilayani Siha.

 Sambamba na mradi huo mkubwa wa Africado uliopo Kijiji cha Kifufu, mradi mwingine mkubwa ulitoa ajira nyingi kwa wananchi wa Siha ni shamba la uzalishaji Mayai ya kisasa lenye ukubwa wa hekari 507 lililopo Kijiji cha Namwai ambalo mwekezaji wake ni Irvine Family. Miradi hii imezalisha ajira zaidi ya 700 Kati ya 2,000 za wananchi kuanzia mwaka 2015 hadi 2020.

 Akizungumza na Amsha Amsha 2020 ya Uhuru FM ikilenga kuainisha mafanikio ya Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Rais John Magufuli, 

Meneja Utawala wa Shamba la Africado, Berinda Meena amesema shamba hilo limesaidia kupatikana kwa ajira 500 za wananchi wa Siha zilizowawezesha kujikwamua kiuchumi na kujiongezea kipato.

 Amesema mbali ya kufanisha utoaji wa ajira kwa mamia ya wananchi wa Siha, shamba hilo la Africado lenye uwekezaji wa mabilioni ya shilingi linawasaidia wafanyakazi wake kuwajengewa uwezo wa ujuzi wa kilimo kwa kufunga vikonyo,  ambapo sehemu kubwa ya wafanyakazi wana mashamba yao binasfi.

 Meena amesema wafanyakazi pia wanapatiwa pembejeo bure na mwekezaji na mazao yao wanayauza kwa mwekezaji - Africado lengo likiwa kuwawezesha kuwa na soko la uhakika.

 po Mwekezaji wake ni James Pasoz raia wa Ujerumani.

 "Tangu Mwekezaji huyu, James Pasoz ambaye ni raia wa Ujerumani awekeze katika shamba hili sasa yapata miaka 10 anazalisha maparachichi na kuyauza Ulaya na Uarabuni.

 "Mwaka huu zaidi ya tani 3,600 zimezalishwa katika shamba hili na kuuzwa nje ya nchi.

 'Maandalizi ya shamba la Maparachichi ni miaka mitatu kuanzia hatua ya kupanda miche hadi kuvuna kwa kutumia mbegu ya hasi inayokuwa haraka" alisema Meena.

 Aidha, amesema serikali imekuwa ikitoa kipaumbele kwa kutoa leseni kupitia EPZ na msamaha wa kodi na kuwezesha eneo kubwa kwa kuweka mtaji mkubwa na hivyo ameipongeza serikali kwa kusamehe kodi ya ongezeko la thamani (VAT) kwa vitu ambavyo mwekezaji ananunua kwa ajili ya shamba hilo.

 Meena alisifu uhusiano mzuri baina ya mwekezaji na serikali ambao umewezesha shughuli za uzalishaji kuwa kutokwama.

 "Mazingira ya uwekezaji sasa ni mazuri kwa kiasi kikubwa, yamekuwa mazingira yanayosaidia kampuni kukuwa kwa kiasi kikubwa.

 "Kwa sababu ya kuwepo mazingira mazuri ya uwekezaji, mwekezaji sasa anatafuta maeneo mengine ya kuwekeza zaidi wilayani Siha.

 "Shamba hilo limekuwa na msaada mkubwa kwani kipato kinachopatikana  kimekuwa kikisaidia kukuza uchumi wa wananchi pamoja na kujenga shule ya msingi Karagoha na kutoa kampeni ya matibabu bure ya macho," amesema Meena.

 Wakati huo huo, Meneja Mwendeshaji wa Shamba la Mayai ya Kisasa la Joseph Kasegama, amesema shamba hilo limeondoa upungufu wa upatikanaji wa vifaranga vya Kuku na limesaidia upatikanaji wa ajira 120 kwa wananchi wa Siha na kuongeza pia mapato katika Halmashauri ya Wilaya ya Siha.

 "Shamba hilo la Irvine Family lenye hekari 507 lina Mabanda 507 yenye uwezo wa kuchukua kuku 9,000," amesema.

 Naye Mkuu wa Wilaya ya Siha, Onesmo Buswelu ameipongeza Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Rais Magufuli kwa kupeleka kiasi kikubwa cha fedha za maendeleo katika wilaya hiyo ambazo zimewezesha kukarabati pia Hospitali ya Wilaya ya Siha.

 "Tumepata fedha, fedha hizo zimesaidia kukabarati  Hospitali ya Kibong'oto inayotibu wagonjwa wa Kifua Kikuu (TB), shilingi bilioni saba zimepelekwa pale huku Hospitali ya Wilaya ya Siha ikipokea shilingi bilioni mbili zilizofanya ukarabati mkubwa," alisema.

 Aidha, amesema zaidi ya shilingi bilioni 50 zimetumika kujenga barabara za lami wilayani humo sanjari na kurahisisha upatikanaji wa huduma ya maji safi na salama.

 "Mpango wa elimu bure umesaidia kuongeza idadi ya wanafunzi wanaojiunga na elimu ya msingi na sekondari wakiwemo jamii ya wamasai.

 "Ni kwamba ukanda wa Kasikazini haujasaulika ni tofauti kabisa na ambavyo imekuwa ikisemwa kuwa ukanda huu umesahaurika kitu ambacho sio kweli," anasema Buswelu ambaye kauli yake inaungwa mkono Katibu Tawala wa Wilaya, Joseph Mabiti.

 Kuhusu uhusiano na wawekezaji amesema ni mzuri na hivyo kuwataka watu kupuuza kauli zinazotolewa kuwa hakuna uhusiano mzuri baina ya serikali na wawekezaji.

 


Akizungumzia Kampeni za Uchaguzi Mkuu zinazoendelea, Buswelu,  amewataka wanasiasa kunadi sera zao kwa utulivu na kuache mihemuko.

 Alisisitiza kuwa wananchi wanapaswa kutekeleza haki yao ya msingi kwa kujitokeza kwa wingi Oktoba 28 mwaka huu wakachague viongozi watakaowaletea  maendeleo ya haraka.

 Kwa upande wake Mganga Mkuu wa Hospitali ya Wilaya ya Siha, Dk. Andrew Method, amesema hivi karibuni mashine ya X-ray itafungwa na hivyo kupunguza changamoto ya wanachi kwenda kutafuta huduma ya vipimo KCMC pamoja na Hospitali ya Mawenzi ya Mjini Moshi.

 Aidha Hospitali hiyo ndani ya wiki chache zijazo majengo ya huduma na mama na mtoto yataanza kutumika, ambapo katika Hospitali hiyo vifo vinavyotokana na uzazi vimepungua hadi  kifo kimoja kwa mwaka.

 Aidha, Dk Method amesema hospitali hiyo itakuwa na uwezo wa kuwa na jengo la kisasa la kuhifadhi miili 20 ya marehemu kwa wakati mmoja.

 Pia amesema ndani ya miezi mitatu ijayo Hospitali hiyo ya Siha itapokea kiasi kikubwa cha dawa ambacho kitatoshereza hospitali hiyo na hata kuzidawa katika vituo vingine vya Afya nje ya Wilaya hiyo.

 Nao wananchi pamoja na watumishi wa Hospitali ya Wilaya ya Siha, wamepongeza uboreshaji wa Hospitali hiyo ambayo inatoa huduma kubwa za kibingwa ambazo walikuwa wakizipata nje ya Wilaya hiyo ya Siha.

 Mwisho

No comments:

Post a Comment