banner

Wednesday, September 30, 2020

MAJALIWA: SERIKALI YATEKELEZA MIRADI 1,423 YA MAJI

 


Kayanga ni miongoni mwa miji 28 iliyonufaika na sh. tril. 1.2 za miradi hiyo

MJUMBE wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya Chama cha Mapinduzi (CCM) Kassim Majaliwa amesema Serikali imetekeleza miradi ya maji 1,423 ikiwemo mradi wa kupeleka maji kwenye miji 28 inayotekelezwa kwa sh. trilioni 1.2.

“Kayanga imepata sh. bilioni 58, ni miongoni mwa miji 28 iliyopata fedha za mradi wa maji kitaifa ambao unajumuisha mikoa mingi,” amesema.

Ametoa kauli hiyo leo (Jumanne, Septemba 29, 2020) wakati akizungumza na wakazi wa kata ya Kayanga, katika mikutano uliofanyika kwenye uwanja wa Changarawe, wilayani Karagwe, mkoani Kagera.

Mikoa inayohusika na mradi huo miji yake kwenye mabano ni Tanga (Handeni/Korogwe, Muheza na Pangani); Njombe (Njombe, Wanging’ombe na Makambako); Kagera (Kayanga); Mtwara (Nanyumbu na Makonde) na Singida (Manyoni).

Pia Ruvuma (Songea); Tabora (Sikonge, Urambo-Kaliua); Mbeya (Rujewa na Chunya); Kigoma (Kasulu); Lindi (Kilwa Masoko); Mara (Mugumu, Rorya/Tarime); Geita (Geita na Chato); Singida (Singida Mjini na Kiomboi); Katavi (Mpanda); Dodoma (Chamwino na Chemba); Iringa (Mafinga); na Morogoro (Ifakara).

Majaliwa ambaye yuko mkoani Kagera kumuombea kura mgombea urais kwa tiketi ya CCM, Dk. Magufuli alitumia fursa hiyo kumnadi mgombea ubunge wa jimbo la Karagwe, Innocent Bashungwa, mgombea udiwani wa Kata ya Kayanga, na wagombea wa CCM wa kata za wilaya hiyo.

Amesema miradi mingine ya maji inayotekelezwa kwenye wilaya hiyo imetumia sh. bilioni 5.2 kwa ajili ya uboreshaji wa miradi ya maji. Ameitaja miradi hiyo kuwa ni mradi wa maji Kijiji cha Nyaishozi ambao umetumia sh. milioni 706, umekamilika na unatoa huduma.

“Shilingi bilioni 1.6 zilitumika kwa ujenzi wa mradi wa maji Kijiji cha Chamchuzi, mradi umekamilika na unatoa huduma, shilingi milioni 805 zilitumika kwa ujenzi wa mradi wa maji Chanika, mradi umekamilika na unatoa huduma," amesema.

Amesema sh. milioni 63 zilitumika kwa uchimbaji wa visima vinne na ufungaji wa pampu katika vijiji vya Okakajinja na Chonyonyo, mradi ambao umekamilika na unatoa huduma. 

Amesema fedha nyingine zilizotumika ni sh. milioni 120 kwa ajili ya mradi wa maji uchimbaji wa visima vinne na ufungaji wa pampu katika vijiji vya Mulamba na Nyarugando, ambao pia umekamilika na unatoa huduma.

Amesema sh. bilioni 2.4 zilitumika kwa ajili ya mradi wa maji Nyakakika, ambao uko katika hatua za umaliziaji na sh. milioni 251 zilitumika kwa ajili ya mradi wa maji Rugu, ambao nao upo kwenye hatua za majaribio.

No comments:

Post a Comment