banner

Friday, September 25, 2020

IRUGWA KUPATA KITUO CHA AFYA

 



NA MWANDISHI WETU

WAZIRI Mkuu, Kassim Majaliwa amesema Serikali ya Chama Cha Mapinduzi itajenga kituo kipya cha afya katika Kata ya Irugwa, Wilaya ya Ukerewe mkoani Mwanza ili kuwaondolea adha ya kusafiri umbali mrefu wananchi wa kata hiyo kufuata huduma za kitabibu

Akizungumza leo na wakazi wa Kata ya Irugwa wakati wa mkutano wa kumuombea kura mgombea urais wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Rais John Magufuli, amesema uamuzi huo unakwenda sambamba na ahadi ya Ilani ya Uchaguzi ya 2020 - 2025.

Waziri Mkuu Majaliwa ambaye pia ni Mjumbe wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya CCM, amesema  katika ilani ya uchaguzi ya 2020-2025, ukurasa wa 186 unasomeka, "hadi  kufikia 2025 serikali itaongeza vituo vya kutolea huduma za afya kwa asimilia 20 ya vituo 8,446 vilivyopo sasa; vipaumbele vitawekwa  katika ujenzi wa vituo vya afya na ukamilishwaji wa maboma kwa kuzingatia uwiano wa kijiografia, idadi ya watu na wingi wa wagonjwa."

Amesema Serikali ya Rais Magufuli imekwishatoa sh milioni 49.2 kwa ajili ya ujenzi wa jengo moja la kujifungilia  katika zahanati Irugwa.

Akizungumza kuhusu utekelezaji wa miradi ya maji kama ilivyoainishwa kwenye ilani ya uchaguzi, alisema ilani imeweka mipango imara ya kushughulikia upatikanaji wa maji vijijini kama hatua ya kutekeleza azma ya Rais Magufuli  ya kumtua mama ndoo kichwani.

Kuhusu usafiri wa majini, Waziri Mkuu Majaliwa amesema Serikali ya CCM ikiingia madarakani inakusudia kujenga vivuko mbalimbali kikiwemo kivuko cha Irugwa, Murtanga, Gana, Kakakuru na Lugezi hadi Kisorya.

" Kwa mujibu wa ilani ya uchaguzi ya CCM, ukurasa wa 83 hadi 84, Chama Cha Mapinduzi kimeielekeza serikali ikamilishe ujenzi wa vivuko vipya nane kikiwemo cha Irugwa - Murutanga wilayani Ukerewe.

"Pia ilani imeelekeza serikali ianze kutekeleza mradi wa ujenzi wa maegesho ya Lugezi - Kisorya mkoani Mwanza, Kome na Nyakalilo mkoani Mwanza, Utete huko Pwani, Chato- Nkome huko Geita, Iramba na Majita mkoani Mwanza na Irugwa," alisema.

 

No comments:

Post a Comment