banner

Wednesday, September 30, 2020

MAJALIWA APOKEA WANACHAMA 20 WA CHADEMA BUKOBA MJINI

 


*Wamo Mwenyekiti wa Vijana wa Mkoa, Naibu Katibu Mkuu Tanzania Bara,

MJUMBE wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Chama cha Mapinduzi (CCM), Kassim Majaliwa leo amewapokea wanachama 20 kutoka Chama cha Demokrasia (CHADEMA) ambao wameamua kurudi CCM. 

Wanachama hao wameongozwa na Mwenyekiti wa Vijana wa CHADEMA wa Mkoa wa Kagera, Francis Mutachunzibwa ambaye pia alimtambulisha aliyekuwa Naibu Katibu Mkuu wa BAVICHA, Getrude Ndibalema ambaye alijiuzulu uongozi tangu mwaka jana.

Akizungumza kwa niaba ya wenzake, Mutachunzibwa amesema: “Ninaijua vizuri CHADEMA, nilipotea, nilitenda dhambi lakini sasa nimeamua kurudi nyumbani, nipokeeni.

“Ninawaomba wana-Bukoba tumchague Dk. Magufuli, mashine ya kusaga na kukoboa, jembe la nguvu. Kuanzia kesho, nitamnadi yeye na Advocate Byabato hadi kieleweke," amesema.

Akizungumza na maelfu ya wakazi wa mji wa Bukoba leo jioni, waliojitokeza kwenye mkutano uliofanyika uwanja wa Mashujaa, Manispaa ya Bukoba, mkoani Kagera, Majaliwa aliwataka wakazi hao wajitafakari sana wanapofikiria kumchangua mtu wa kuongoza nchi.

“Tunataka kiongozi mwenye hofu ya Mungu na ili umpate ni lazima umjue historia yake. Kuongoza nchi si lelemama, kiongozi wa nchi ni Mkuu wa Nchi, tena ni Mkuu wa Majeshi," amesema Majaliwa.

Majaliwa ambaye ameanza ziara katika Mkoa wa Kagera kumuombea kura mgombea urais kwa tiketi ya CCM, Dk. John Pombe Magufuli, ametumia fursa hiyo kuwaombea kura mgombea ubunge wa jimbo la Bukoba Mjini kwa tiketi ya CCM, Wakili Steven Byabato, mgombea udiwani wa Kata ya Bilele, Tawfiq Sharif Salum na madiwani wengine wa jimbo hilo.

Aliwasimamisha wazee wa Kagera wakiwemo aliyekuwa Meya wa Bukoba, Dk. Anatoly Amani, aliyekuwa mbunge wa jimbo hilo, Balozi Khamis Kagasheki ambao wote waliomba kura za Dk. Magufuli, Wakili Byabato na madiwani wa jimbo hilo.

Kwa upande wake, aliyekuwa Waziri wa Viwanda, Charles Mwijage, amesema Muleba wana ajenda ya kuhakikisha kura zote zinaenda kwa Dk. Magufuli na wabunge wa CCM na akawataka wana-Bukoba nao wafanye hivyo ili kuhakikisha majimbo yote tisa yanabakia CCM na pia wanapata wabunge wanne wa viti maalum.

No comments:

Post a Comment