Jengo
la Zahanati ya Kijiji cha Ntope
kilichopo Kata ya Sanza, Wilaya ya Manyoni, Mkoa wa Singida ambalo
ujenzi wake ulianza 2013. Mradi huu unadaiwa kughubikwa na vitendo vya ufisadi
NA MWANDISHI WETU
MGANGA Mkuu wa Wilaya ya Manyoni (DMO) Furaha Mwakafula
amesema ujenzi wa Zahanati ya Kijiji cha Ntope kilichopo Kata ya Sanza,
Wilaya ya Manyoni mkoani Singida haujakamilika kwa miaka minane sasa
kutokana na ukosefu wa fedha.
Mwakafula ameyasema hayo leo wakati wa mahojiano na
TANZANIA PANORAMA kuhusu kukwama kwa ujenzi wa zahanati hiyo na madai ya
ufisadi dhidi ya fedha zilizotolewa na serikali kwa ajili ya ujenzi huo.
Amesema mbali na zahanati hiyo, ujenzi wa nyumba ya
daktari wa kijiji ulikamilika na ilianza kutumiwa na mtumishi ambaye hakuwa wa
kada ya afya aliyepewa na uongozi wa kijiji.
"Taarifa nilizonazo mimi ni kwamba ujenzi wa
zahanati hiyo ulianza mwaka 2012, katika bajeti ya mwaka 2012/2013 zilitolewa
sh milioni 20 zikatumika kujenga sehemu ya boma ambalo halikukamilika na tangu
wakati huo haijatolewa fedha nyingine. Kwa hiyo ujenzi umekwama kwa miaka yote
hiyo kwa sababu ya ukosefu wa fedha," alisema Mwakafula.
Alipoulizwa kuhusu madai kuwa zilitolewa sh milioni
60 ila zilizoelekezwa kwenye ujenzi ni sh milioni 20 huku sh milioni 40
zikihamishiwa kwenye fungu lisilojulikana na hazijapata kurejeshwa hadi sasa
alisema hizo zinaweza kuwa hisia za watu au upotoshaji wa makusudi.
"Kuna mambo mawili hapo ambayo ni vizuri
yaeleweke, moja ni kwamba kuna fungu la fedha kutengwa kwenye bajeti na kuna
fungu la fedha husika kupelekwa na kupokelewa kwenye mradi. Sasa mimi
nimethibitishiwa na wataalamu wa mipango kuwa fedha iliyotolewa na kutumika
kwenye mradi huo ni sh milioni 20 tu," alisema Mwakafula.
Aidha mganga mkuu huyo alisema mradi mwingine wa
ujenzi wa nyumba ya daktari ulioanza sambamba na zahanati ya Ntope ulikamilika
na uongozi wa Kijiji cha Ntope uliitoa nyumba hiyo itumiwe na mtumishi wa
serikali ambaye hakuwa wa kada wa afya hadi ilipoharika paa.
"Kuhusu nyumba ya daktari yenyewe ilikamilika
na uongozi wa kijiji uliitoa kwa mtumishi ambaye hakuwa wa kada ya afya. Huyo
aliitumia hadi ilipoezuka paa lake. Hivi sasa ndiyo tunafikiria kuitengeza ili
ianze kutumika kama zahanati ya kijiji," alisema.
Aidha, Mwakafula alisema taarifa kuwa zahanati ya
Kijiji cha Ntope ambayo haijawahi kutoa huduma hupewa mgao wa dawa kutoka MSD
ni za kweli na dawa hizo huwa zinaelekezwa zahanati za jirani ambazo
zinawahudumia wananchi wa Kijiji cha Ntope.
" Hilo kweli fungu la fedha za dawa katika
zahanati ya Ntope huwa linatoka kila mwaka lakini kwa sababu haipo fedha hizo
huwa zinaelekezwa zahanati za jirani ambazo zinatoa huduma kwa wananchi wa
Kijiji cha Ntope," alisema.


No comments:
Post a Comment