banner

Monday, September 21, 2020

FATUMA KARUME AFUKUZWA IMMMA ADVOCATES

 



NA MWANDISHI WETU

KAMPUNI ya uwakili ya IMMMA imemfukuza mwanahisa wake, Fatuma Karume.

Barua ya kufukuzwa kwa Fatuma Karume, maarufu kwa jina la shangazi, ya Septemba 16, 2020 ambayo TANZANIA PANORAMA BLOG imeiona imesainiwa  na Mkurugenzi mwenza wa Kampuni ya IMMMA, Sadock Magai ikiwa na maelekezo yanayomtaka wakili huyo kufungasha virago vyake ndani ya mwezi mmoja.

Barua ya kufukuzwa kwa Fatuma aliisambaza yeye mwenyewe kwenye mitandao ya kijamii akiambatanisha na ujumbe kuwa kila kitu kina mwanzo na mwisho.

Katika andishi lake hilo Fatuma anaandika kuwa amefukuzwa kwenye ofisi aliyosaidia kuijenga na kosa lake ni uanaharakati.

Wakili na mwanaharakati Fatuma amefukuzwa na washirika wake wa muda mrefu katika fani ya sheria baada ya kujihusisha na mashambulizi ya mara kwa mara dhidi ya watu mbalimbali wakiwemo viongozi wa serikali.

Aidha, Fatuma amepata kushambuliwa hadharani na mmoja wa wazazi wake kutokana na mwenendo wake wa kuwashambulia kwa lugha isiyokuwa na staha viongozi wakuu wa kitaifa na bila kujali kuwa baba yake mzazi amepata kuwa kiongozi mkuu wa Zanzibar.

Katika barua yake ya kumfukuza Fatuma, Magai anaandika kuwa mwanaharakati huyo anaondolewa kwenye umiliki wa kampuni na akusanye vilivyo vyake katika ofisi hiyo ndani ya mwezi mmoja.

Magai anaandika zaidi akielekeza kuwa Fatuma anapaswa kurudisha kila kitu alichonacho ambacho ni mali ya Kampuni ya IMMMA na pia kesi alizokuwa anazisimamia
azikabidhi na hasa kesi ya Kampuni ya Shivacom na Vodacom.

Andiko la Magai linaeleza pia kuwa Fatuma atalipwa stahiki zake kwa mujibu wa sheria.

No comments:

Post a Comment