NA MWANDISHI WETU
MGOMBEA ubunge wa Jimbo la Mbeya Mjini kwa tiketi ya
Chama Cha Mapinduzi (CCM) Dk.Tulia Ackson jana amepiga hodi katika Kata ya
Sinde kuomba kura huku akiwa amebeba ujumbe unawaotaka wananchi wa jimbo hilo
kulala wanapokula.
Katika mkutano huo uliohudhuriwa na maelfu ya
wananchi, Dk Tulia amesema watu waliozowea kula kwa dada na kulala
kusikojulikana waanze kujiandaa kwenda kulala wanakokula.
Dk Tulia amewaomba wananchi wa Kata ya Sinde kukipa
ridhaa ya uongozi CCM kwa kipindi kingine cha miaka mitano kwa kumchagua Rais
John Pombe Magufuli kuwa Rais, kumchagua yeye kuwa Mbunge na pia kuwachagua
madiwani wa CCM.
Amesema wananchi wa Kata ya Sinde wana kila
sababu ya kumchagua Rais Magufuli katika uchaguzi mkuu wa Oktoba 28, mwaka huu
ili apate fursa ya kukamilisha kazi kubwa na ya kutukuka anayolifanyia taifa.
"Ninapokuja hapa kwenu ndugu zangu mimi siyo
mgeni, kuna watu wanasikika huko wakisema kwamba tunakula kwa dada halafu
tutalala sijui wapi… safari hii tunalala tulipokula. Kura yetu safari hii
tutaipeleka kwenye maendeleo na maendeleo safari hii hapa Mbeya ni CCM tu.
“Mpaka hapa ninapozungumza na nyie baada ya
kushuhudia mafuriko ya watu waliojitokeza kuungana nasi katika maeneo ya Kata
za Nzovwe, Isyesye, Igawilo, Sinde na mahali kwengineko mimi mbunge wa
kujiongeza nilishafanya 'connection'.
"Hapa ninapozungumza, mipango kazi ipo tayari,
watu wanafanya usanifu ili miundombinu yetu ikae sawa.
“Watu wa Mbeya safari hii tunaenda kwa kasi ya
kujiongeza na kasi hii inatoka Chama Cha Mapinduzi pekee, pigieni kura zote CCM
mjionee maendeleo yatakavyoinuka kwa kasi ya ajabu. Mtu akija kwenu kuwapiga
propaganda muulizeni umetufanyia nini kabla ya kuja hapa kuomba kura?” Dk.
Tulia.





