banner

Saturday, October 3, 2020

WATANZANIA WAASWA KUCHAGUA KIONGOZI ATAKAYEKUZA UHUSIANO WA KIDIPLOMASIA

 

NA MWANDISHI WETU

MJUMBE wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), Kassim Majaliwa amewaasa Watanzania kuchagua kiongozi ambaye atakuza uhusiano wa kidiplomasia na nchi jirani.

“Tanzania inazungukwa na nchi tisa ambazo baadhi yake ziko kwenye Jumuiya ya Afrika Mashariki na nyingine hazimo. Tunahitaji kiongozi ambaye ataweza kuhakikisha nchi hii inakuwa na uhusiano mwema na nchi jirani na nchi nyingine duniani kote lakini pia anayeweza kuilinda heshima ya nchi yetu,” amesema.

Majaliwa ameyasema hayo Alhamisi, Oktoba Mosi, 2020 wakati akizungumza na wakazi wa Kata za Nyakahura na Nyakanazi, wilayani Biharamulo, mkoani Kagera akiwa njiani kuelekea Wilaya za Bukombe na Mbogwe mkoani Geita.

Majaliwa ambaye amemaliza ziara yake mkoani Kagera ya kumuombea kura mgombea urais kwa tiketi ya CCM, Dk. John Pombe Magufuli alitumia fursa hiyo kumnadi mgombea ubunge wa Jimbo la Biharamulo Magharibi, Injinia Ezra Chiwelesa na wagombea udiwani wa CCM wa kata hizo, Apolinary Mgalula na Amos Madegwa.

Akielezea suala la vitambulisho vya uraia, amesema kote alikopita mkoani humo wananchi wanauliza kuhusu kuchelewa kutolewa kwa vitambulisho hivyo.

"Ucheleweshaji huu hauko hapa mkoani Kagera tu bali hata kwenye mikoa ya pembezoni ya Kigoma, Songwe, Katavi, Ruvuma, Mtwara, Lindi, Pwani, Arusha na Mara.

"Hii ni kwa sababu tunataka tujiridhishe na uraia wa waombaji kwani hili suala ni kwa usalama wa nchi yetu. Wale walioko jirani umbali wa km. 10 wanaruhusiwa kuja kutembea au kufanya biashara na kurudi kwao. Hawaruhusiwi kupata vitambulisho, hivi ni kwa Watanzania tu," amesema Majaliwa.

Kiongozi huyo amewahakikishia wakazi hao kwamba kila Mtanzania mwenye sifa atapata kitambulisho cha Taifa kwa kuwa ndiyo mkakati wa Serikali inayoongozwa na Rais Dk. Magufuli.

Majaliwa amesema Idara ya Uhamiaji inatakiwa kuwa makini kusimamia mchakato huo kwa sababu wapo baadhi ya raia wa nchi jirani wanatamani kupata kitambulisho cha Taifa kutokana na amani iliyopo nchini.

"Uhamiaji iwe makini haitapendeza kuona Mtanzania anakosa kitambulisho cha Taifa halafu mgeni kutoka nchi jirani anapata," amesema.

Hata hivyo, amewataka wakazi hao wasikubali kutoa rushwa kwa sababu hiyo ni haki yao na kwamba endapo itatokea wameombwa rushwa watoe taarifa.

"Mtu wa uhamiaji akidai rushwa ili akupatie kitambulisho toa taarifa mara moja ili tumshughulikie," amesisitiza.

WENGI WANAGHUSHI NYARAKA ZA SERIKALI - TMDA

 

NA MWANDISHI WETU

IMEELEZWA kuwa vitendo vya kughushi nyaraka za serikali vinafanywa na Watanzania wengi hapa nchini.

Akizungumza na TANZANIA PANORAMA jana, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Dawa na Vifaa Tiba( TMDA), Akida Khea, alisema siyo jambo jipya wala la kushtusha kwa nyaraka za serikali kughushiwa na kazi ya serikali ni kupambana na uhalifu huo.

Khea alikuwa akitoa ufafanuzi wa mwenendo wa uchunguzi wa tuhuma kuhusu Kampuni ya Multvet Farm Ltd ya jijini Dar es Salaam kuingiza nchini dawa za mifugo na kuzisambaza kwa matumizi kwa kutumia vibali vyenye shaka vya TMDA.

Msemaji wa TMDA, Gaudensia Simwaza ambaye awali alilieleza TANZANIA PANORAMA kuwa taasisi yake inaendelea na uchunguzi wa nyaraka za kampuni hiyo hivyo ipewe muda wa kutosha, jana alipoulizwa alisema mkurugenzi wake mkuu  alitaka kwanza kuzungumza na TANZANIA PANORAMA.

Katika mazungumzo yake na TANZANIA PANORAMA, Khea aliomba mkutano wa ana kwa ana kwa kuialika ofisini kwake Jumatatu, Oktoba 5, 2020 huku akisisitiza kuwa anahitaji kupata msaada utakaosadia uchunguzi unaofanywa taasisi yake.

Alisema, vitendo vya kughushi nyaraka za serikali siyo vipya kwani vimekuwa vikifanywa na watu wengi hivyo vipo kila mara na kwamba serikali imekuwa ikipambana navyo.

"Njoo ofisini tuzungumze, njoo utusaidie. Huyu mtu siyo wa kwanza. Wapo wengi tu. Hivi vitendo vya watu kughushi nyaraka za serikali vinafanywa na watu kila mara na serikali inapambana navyo kikamalifu," alisema Khea.

Inadaiwa kuwa Kampuni ya Multvet Farm Ltd inayoagiza dawa za mifugo kutoka nje ya nchi imekuwa ikitumia vibali vyenye shaka vya TMDA huku akilipa kodi zote za serikali.

Kwamba kampuni hiyo imekuwa ikitumia vibali vyenye shaka vya TMDA kwa zaidi ya miaka minne sasa na baadhi ya wataalamu wa afya ya mifugo wameeleza kuwa dawa ambazo hazijathibitishwa na TMDA kutumika katika mifugo zinaweza kuwa na athari mbaya katika ustawi wa mifugo na kuongeza kuwa hilo linaweza kuwa moja ya mipango ovu ya kuangamiza mifugo hapa nchini.

Mmiliki wa Kampuni ya Multvet Farm Ltd, Dk. Henry Ruhinguka alipoulizwa kuhusu kampuni yake kuelekezewa madai hayo kwanza alikanusha kuwa yeye siyo msemaji wa kampuni hiyo na pia alikanusha kufahamu lolote kuhusu madai hayo.

Hata hivyo uchunguzi wa TANZANIA PANORAMA umebaini kuwa Dk. Henry ndiye mmiliki wa kampuni hiyo na amekuwa mzungumzaji wake mkuu.

Katika mahojiano hayo Dk. Henry baada ya kuelezwa kuwa baadhi ya nyaraka zenye shaka za kampuni yake zilizotumika kuingiza dawa hizo TANZANIA PANORAMA limeziona, alisema, hayo ni mambo ya zamani na hivi sasa kampuni hiyo iliishaachana nayo.

Alisema ni kweli jambo hilo liliwahi kutokea na alilipeleka Dodoma kwa wakubwa  lakini hakufafanua alilipeleka kwa wakubwa gani na maamuzi yaliyochukuliwa.

VIBARUA ONE WORLD CO. LTD WALIA KUNYANYASWA, KUTISHIWA MAISHA


NA MWANDISHI WETU

VIBARUA wa Kampuni ya One World Company Limited ya jijijni Dar es Salaam wamelalamika kuwa wananyanyaswa na kutishiwa maisha na mwajiri wao.

Wamesema mwajiri wao anakiuka makubaliano waliyoingia kufanya kazi, kutowapa mikataba ya ajira, kuwapunja malipo ya kazi wanazofanya kwa kampuni anazowapeleka kufanya kazi anazoingia nazo mikataba ya kumkodishia vibarua na kutopeleka fedha za makato katika mifuko ya pensheni.

Malalamiko hayo wameyatoa mwishoni mwa  wiki jijini Dar es Salaam katika mahojiano yao na TANZANIA PANORAMA.

"Tumeamua kuwatafuta nyie watu wa TANZANIA PANORAMA baada ya kuona nyie mko tofauti na wengine kwa sababu mnagusa matatizo ya Watanzania na kuyaweka hadhani. Ukiangalia kwenye mitandao unaona mnaandika habari ambazo haziandikwi na wengine ambazo zinagusa maisha ya watu wanyonge moja kwa moja.

" Sasa sisi tuna malalamiko yetu, tunaomba yafike serikalini na tunaomba serikali ije itusikilize sisi wananchi wake. Tunaomba kwanza kuiambia serikali kuwa huyu mwajiri wetu Kampuni ya One World Company Limited anatunyanyasa na kututishia maisha kila tunapojaribu kudai hata kile kidogo anachotudhulumu.

"Huyu mwajiri wetu anatufanyisha kazi kwa saa nyingi kuliko tulivyokubaliana, baadhi yetu wana miaka mingi sana kwenye kampuni lakini kila wakiomba ajira anasema anayetaka ajira aache kazi. Sasa tunashagaa huyu bwana mbona anakiuka sheria kwa sababu sheria inaelekeza mtu akifanya kazi kwa kipindi fulani anapaswa kuajiriwa.

"Jambo jingine ni pensheni, hapeleki pesa yetu kwenye mifuko ya jamii, na huko mahakama ya kazi wamemshindwa maana amekataa kupokea barua za mahakama  baada ya wenzetu kumfungulia shauri kwenye mahakama hiyo lakini kinachotuuma zaidi, huyu ana mikataba ya siri na baadhi ya makampuni hapa nchini ambayo huwa anayatafutia vibarua anawapeleka kufanya kazi huko na hayo makampuni yanamlipa ili alipe vibarua aliowapeleka.

" Kibaya hapo ni kwamba zile pesa zetu huwa anatulipa kidogo sana kiasi kikubwa anachukua yeye bila kujali kampuni hizo zinakuwa zimeishamlipa hela yake ya udalali. Tukimlalamikia kuwa anatuonea anasema ambaye amechoka kuishi aendelee kuhoji na ole wake atakayebainika kutoa siri za kampuni nje," alisema mmoja wa vibarua hao ambaye jina lake tunalihifadhi kwa sababu ya kulinda kibarua chake.

Akizungumzia malalamiko hayo. Mwanasheria wa vibarua hao, Saulo Kusakala alieleza kushangazwa na uongozi wa kampuni hiyo kwa kuonyesha kiburi hata kwa Mahakama.

"Kweli mimi ni mwanasheria wao, nimeamua kuwasaidia kwa sababu ukisikia mateso yao kwa kweli unawahurumia. Kama mwanasheria wao nilimuandikia barua huyo mwajiri ili nipate maelezo yake kuhusu malalamiko ya wafanyakazi wake alichojibu ni kwamba hawatambui. Yaani hana ushirikiano kabisa," alisema.

Alipoulizwa Mkurugenzi wa One World, Kelvin Tegwa kuhusu malalamiko hayo alisema hao waliokuja kwa waandishi wa habari wanajisumbua na alijigamba kuwa ana mkono mrefu hivyo atawabaini na atawashughulikia.

"Unasema wewe ni mwandishi wa habari, kwa hiyo wamekuja kwako ili utuchafue. Kwahiyo kwako ndiyo wanadhani watapata msaada? Labda nikuulize sasa wamekuja kalalamika kwako wewe utafanya nini? Wewe njoo tuongee ofisini hao waache niko nao mahakamani.

" Na ninakwambia tu mimi nafanya kazi na serikali, nina mkono mrefu hivyo hata hao waliokuja kwako nakuhakikishia ntajua na nitawashughulikia. Hii siyo kampuni ya kuchezea, alisema.

Muda mfupi baadaye TANZANIA PANORAMA lilipigiwa simu na mtu ambaye hakujitambulisha jina lakini uchunguzi wa namba aliyotumia umebaini kuwa imesajiliwa kwa jina la Dismas Damas ambaye alionya kuwa kitu chochote kinachohusu kampuni hiyo kisiandikwe.

Damas alisema iwapo maelekezo hayo yatakiukwa asiwepo wa kulalamika na kabla hajakata simu alisema yeye ni meneja wa Kampuni ya One World Company Ltd na milango yake ipo wazi kwa mazungumzo.

Thursday, October 1, 2020

SH. BILIONI 5.26 ZATUMIKA KUJENGA BARABARA NGARA

 



SHILINGI bilioni 5.26 zimetolewa kupitia Wakala wa Barabara za Mjini na Vijijini (TARURA) kwa ajili ya ujenzi na matengenezo ya barabara katika Wilaya ya Ngara, mkoani Kagera.

 “Kati ya hizo, shilingi bilioni 1.1 zimetengeneza barabara kwa kiwango cha lami kilomita 4.5 katika makao makuu ya wilaya hii.”

WHayo yamesemwa leo (Jumatano, Septemba 30, 2020) na Mjumbe wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya Chama cha Mapinduzi (CCM), Kassim Majaliwa wakati akizungumza na wakazi wa Kata ya Rulenge, katika mikutano uliofanyika kwenye stendi ya Rulenge.

Amesema kiasi kingine cha shilingi bilioni 4.16 zimetolewa kupitia TARURA kwa ajili ya ujenzi na matengenezo ya barabara ikiwemo barabara za Muhweza – Mukarehe, Keza – Nyanzovu, Mukalinzi – Mulonzi, Kibuba – Gwenzaza, Murugwanza - Runzenze (Airstrip), Chivu - Ntobeye – Nyakiziba,Buhororo – Mukididili, Ngara – Kumutana na Buhororo - Ruganzo (Airstrip)

Majaliwa ambaye leo anamalizia ziara yake mkoani Kagera ya kumuombea kura mgombea urais kwa tiketi ya CCM, Dk. John Pombe Magufuli alitumia fursa hiyo kumnadi mgombea ubunge wa jimbo la Ngara, Ndayisaba George Ruhoro na mgombea udiwani wa CCM wa kata ya Rulenge, John Niyonzima.

Mapema, akiwa njiani kuelekea Ngara akitokea Bukoba mjini, Majaliwa alisimamishwa na wakazi wa kata za Nyaishozi (Karagwe) na Kasulo Benaco (Ngara) ambako pia aliwanadi madiwani wa kata hizo. Pia aliwaeleza kwamba barabara ya kutoka Omurushaka hadi Benaco itajengwa kwa kiwango cha lami.

“Kwenye Ilani ya uchaguzi iliyopita ambayo inaisha sasa, barabara hii ilielezwa kwamba itakamilishwa kufanyiwa upembuzi yakinifu, na sasa inaenda kujengwa kwa lami kwa sababu kazi imeshafanyika.”

Pia aliitaja barabara nyingine ya kutoka Bugene – Kasulo (BENACO) yenye urefu wa km. 124 ambayo inatajwa kwenye uk. 75 wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM kwamba ni miongoni mwa barabara zitakazoanza kujengwa upya kwa kiwango cha lami.

 

HOSPITALI YA WILAYA KARAGWE YAKAMILIKA KWA 98%

 



*Mji wa Kayanga kupata barabara za lami, imo ya Murushaka – Murongo

SERIKALI ya Chama cha Mapinduzi (CCM) imetumia sh. bilioni 1.8 kujenga majengo mbalimbali ya hospitali ya Wilaya ya Karagwe ambayo yamekamilika kwa asilimia 98.

Hayo yamesemwa jana (Jumanne, Septemba 29, 2020) na Mjumbe wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya Chama cha Mapinduzi (CCM) Kassim Majaliwa wakati akizungumza na wakazi wa Kata ya Kayanga, katika mkutano uliofanyika kwenye uwanja wa Changarawe, wilayani Karagwe, mkoani Kagera.

Akielezea ujenzi wa vituo vya afya kwenye wilaya hiyo, Majaliwa alisema sh. milioni 900 zimetumika kwa ajili ya ujenzi na ukarabati wa miundombinu mbalimbali ya vituo vya afya ambapo kati ya hizo, sh. milioni 500 zimetumika wa majengo ya kituo cha afya cha Kayanga ambapo kituo hicho kimekamilika na kinatoa huduma.

"Shilingi milioni 400 zimetumika kwa ujenzi wa majengo ya kituo cha afya cha Nyakayanja na ujenzi umekamilika. Pia shilingi bilioni 2.5 zimetumika kwa ajili ya ununuzi wa dawa, vifaa tiba na vitendanishi huku fedha za dawa kwa mwezi zilikuwa ni wastani wa shilingi milioni 53,” alisema.

Akielezea uboreshaji wa miundombinu kwenye wilaya hiyo, Majaliwa alisema ukurasa wa 74-76 wa Ilani ya uchaguzi ya CCM, unaelezea mpango wa serikali kuanza ujenzi mpya (km 6,006.04) na ukarabati wa barabara kwa kiwango cha lami ikiwemo barabara ya Mugakorongo - Kigarama - Murongo yenye urefu wa km 105.

 “Ilani yetu imeenda mbele zaidi na kuelezea mpango wa kukamilisha/kuanza upembuzi yakinifu na usanifu wa kina (km 7,542.75) barabara za mikoa kadhaa ikiwemo barabara ya Murushaka – Murongo yenye km 125.”

Majaliwa ambaye yuko mkoani Kagera kumuombea kura mgombea urais kwa tiketi ya CCM, Dk. Magufuli alitumia fursa hiyo kumnadi mgombea ubunge wa jimbo la Karagwe, Innocent Bashungwa, mgombea udiwani wa kata ya Kayanga na wagombea wa CCM wa kata za wilaya hiyo.

Alisema sh. bilioni 1.4 zimetolewa kupitia Wakala wa Barabara za Mjini na Vijijini (TARURA) kwa ajili ya kufungua barabara mpya, matengenezo ya kawaida, matengenezo ya sehemu korofi, muda maalum na makalvati.

Alisema kati ya hizo, sh. milioni 585 zimetolewa kwa ajili ya matengenezo ya sehemu korofi na baadhi ya maeneo yaliyofanyiwa kazi ni ukarabati katika barabara ya Nyakagoyagoye-Karongoambao uligharimu sh. milioni 31.

Akielezea ukarabati uliofanywa, alisema sh. milioni 19 zimetumika katika barabara ya Kanyabuleza-Runyaga; sh. milioni 14 zimetumika na katika barabara ya Mato-Karehe; sh. milioni 23 zimetumika katika barabara ya Kihanga - Rwabitembe – Mshabaiguru, sh. milioni 16 zimetumika katika barabara yaNyakahanga – Kamahungu, sh. milioni 16 zimetumika katika barabara ya Kishoju – Bujuruga na sh. milioni 23 zimetumika katika barabara ya Igurwa-Kibona-Nyakahita.

Alizitaja barabara nyingine zilizofanyiwa ukarabati kuwa ni Katoju-Ihembe – Bisheshe iliyogharimu sh. milioni 98, barabara ya Kanyabuleza Jct-Makabulini iliyotumia sh. milioni 69, barabara ya KDVTC FADECO iliyotumia sh. milioni 73, barabara ya AMRI – CLASIC iliyogharimu sh. milioni 38 na barabara ya Rukore – Chanikailiyotumia sh. milioni 115.

 

Alisema TARURA ilifanya matengenezo ya madaraja na makalvati katika barabara za Katoju- Rugu - Ruhita (sh. milioni 17), Igurwa-Nyakashozi-Rwentuhe (sh. milioni13),Rukore - Chanika (sh. milioni 12),Rubale - Kibogoizi (sh. milioni 6) na barabara ya Kasheshe - Rubare (sh. milioni 7).

 

“Shilingi milioni 124 zimetumika kwa ajili ya matengenezo maalum katika barabara za Kajunguti - Rubare - Misha (km. 9), Nyabiyonza-Kafunjo(km. 6), Kibaoni Nyabiyonza Sec - Kakuraijo (km. 3.15), Nyakakika - Kandegesho (km.5), Lukole - Kigarama, Lukoyoyo – Kantabire -Nyakasimbi na Ahamulama – Busecha,” alisema.