banner

Saturday, October 3, 2020

VIBARUA ONE WORLD CO. LTD WALIA KUNYANYASWA, KUTISHIWA MAISHA


NA MWANDISHI WETU

VIBARUA wa Kampuni ya One World Company Limited ya jijijni Dar es Salaam wamelalamika kuwa wananyanyaswa na kutishiwa maisha na mwajiri wao.

Wamesema mwajiri wao anakiuka makubaliano waliyoingia kufanya kazi, kutowapa mikataba ya ajira, kuwapunja malipo ya kazi wanazofanya kwa kampuni anazowapeleka kufanya kazi anazoingia nazo mikataba ya kumkodishia vibarua na kutopeleka fedha za makato katika mifuko ya pensheni.

Malalamiko hayo wameyatoa mwishoni mwa  wiki jijini Dar es Salaam katika mahojiano yao na TANZANIA PANORAMA.

"Tumeamua kuwatafuta nyie watu wa TANZANIA PANORAMA baada ya kuona nyie mko tofauti na wengine kwa sababu mnagusa matatizo ya Watanzania na kuyaweka hadhani. Ukiangalia kwenye mitandao unaona mnaandika habari ambazo haziandikwi na wengine ambazo zinagusa maisha ya watu wanyonge moja kwa moja.

" Sasa sisi tuna malalamiko yetu, tunaomba yafike serikalini na tunaomba serikali ije itusikilize sisi wananchi wake. Tunaomba kwanza kuiambia serikali kuwa huyu mwajiri wetu Kampuni ya One World Company Limited anatunyanyasa na kututishia maisha kila tunapojaribu kudai hata kile kidogo anachotudhulumu.

"Huyu mwajiri wetu anatufanyisha kazi kwa saa nyingi kuliko tulivyokubaliana, baadhi yetu wana miaka mingi sana kwenye kampuni lakini kila wakiomba ajira anasema anayetaka ajira aache kazi. Sasa tunashagaa huyu bwana mbona anakiuka sheria kwa sababu sheria inaelekeza mtu akifanya kazi kwa kipindi fulani anapaswa kuajiriwa.

"Jambo jingine ni pensheni, hapeleki pesa yetu kwenye mifuko ya jamii, na huko mahakama ya kazi wamemshindwa maana amekataa kupokea barua za mahakama  baada ya wenzetu kumfungulia shauri kwenye mahakama hiyo lakini kinachotuuma zaidi, huyu ana mikataba ya siri na baadhi ya makampuni hapa nchini ambayo huwa anayatafutia vibarua anawapeleka kufanya kazi huko na hayo makampuni yanamlipa ili alipe vibarua aliowapeleka.

" Kibaya hapo ni kwamba zile pesa zetu huwa anatulipa kidogo sana kiasi kikubwa anachukua yeye bila kujali kampuni hizo zinakuwa zimeishamlipa hela yake ya udalali. Tukimlalamikia kuwa anatuonea anasema ambaye amechoka kuishi aendelee kuhoji na ole wake atakayebainika kutoa siri za kampuni nje," alisema mmoja wa vibarua hao ambaye jina lake tunalihifadhi kwa sababu ya kulinda kibarua chake.

Akizungumzia malalamiko hayo. Mwanasheria wa vibarua hao, Saulo Kusakala alieleza kushangazwa na uongozi wa kampuni hiyo kwa kuonyesha kiburi hata kwa Mahakama.

"Kweli mimi ni mwanasheria wao, nimeamua kuwasaidia kwa sababu ukisikia mateso yao kwa kweli unawahurumia. Kama mwanasheria wao nilimuandikia barua huyo mwajiri ili nipate maelezo yake kuhusu malalamiko ya wafanyakazi wake alichojibu ni kwamba hawatambui. Yaani hana ushirikiano kabisa," alisema.

Alipoulizwa Mkurugenzi wa One World, Kelvin Tegwa kuhusu malalamiko hayo alisema hao waliokuja kwa waandishi wa habari wanajisumbua na alijigamba kuwa ana mkono mrefu hivyo atawabaini na atawashughulikia.

"Unasema wewe ni mwandishi wa habari, kwa hiyo wamekuja kwako ili utuchafue. Kwahiyo kwako ndiyo wanadhani watapata msaada? Labda nikuulize sasa wamekuja kalalamika kwako wewe utafanya nini? Wewe njoo tuongee ofisini hao waache niko nao mahakamani.

" Na ninakwambia tu mimi nafanya kazi na serikali, nina mkono mrefu hivyo hata hao waliokuja kwako nakuhakikishia ntajua na nitawashughulikia. Hii siyo kampuni ya kuchezea, alisema.

Muda mfupi baadaye TANZANIA PANORAMA lilipigiwa simu na mtu ambaye hakujitambulisha jina lakini uchunguzi wa namba aliyotumia umebaini kuwa imesajiliwa kwa jina la Dismas Damas ambaye alionya kuwa kitu chochote kinachohusu kampuni hiyo kisiandikwe.

Damas alisema iwapo maelekezo hayo yatakiukwa asiwepo wa kulalamika na kabla hajakata simu alisema yeye ni meneja wa Kampuni ya One World Company Ltd na milango yake ipo wazi kwa mazungumzo.

Thursday, October 1, 2020

SH. BILIONI 5.26 ZATUMIKA KUJENGA BARABARA NGARA

 



SHILINGI bilioni 5.26 zimetolewa kupitia Wakala wa Barabara za Mjini na Vijijini (TARURA) kwa ajili ya ujenzi na matengenezo ya barabara katika Wilaya ya Ngara, mkoani Kagera.

 “Kati ya hizo, shilingi bilioni 1.1 zimetengeneza barabara kwa kiwango cha lami kilomita 4.5 katika makao makuu ya wilaya hii.”

WHayo yamesemwa leo (Jumatano, Septemba 30, 2020) na Mjumbe wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya Chama cha Mapinduzi (CCM), Kassim Majaliwa wakati akizungumza na wakazi wa Kata ya Rulenge, katika mikutano uliofanyika kwenye stendi ya Rulenge.

Amesema kiasi kingine cha shilingi bilioni 4.16 zimetolewa kupitia TARURA kwa ajili ya ujenzi na matengenezo ya barabara ikiwemo barabara za Muhweza – Mukarehe, Keza – Nyanzovu, Mukalinzi – Mulonzi, Kibuba – Gwenzaza, Murugwanza - Runzenze (Airstrip), Chivu - Ntobeye – Nyakiziba,Buhororo – Mukididili, Ngara – Kumutana na Buhororo - Ruganzo (Airstrip)

Majaliwa ambaye leo anamalizia ziara yake mkoani Kagera ya kumuombea kura mgombea urais kwa tiketi ya CCM, Dk. John Pombe Magufuli alitumia fursa hiyo kumnadi mgombea ubunge wa jimbo la Ngara, Ndayisaba George Ruhoro na mgombea udiwani wa CCM wa kata ya Rulenge, John Niyonzima.

Mapema, akiwa njiani kuelekea Ngara akitokea Bukoba mjini, Majaliwa alisimamishwa na wakazi wa kata za Nyaishozi (Karagwe) na Kasulo Benaco (Ngara) ambako pia aliwanadi madiwani wa kata hizo. Pia aliwaeleza kwamba barabara ya kutoka Omurushaka hadi Benaco itajengwa kwa kiwango cha lami.

“Kwenye Ilani ya uchaguzi iliyopita ambayo inaisha sasa, barabara hii ilielezwa kwamba itakamilishwa kufanyiwa upembuzi yakinifu, na sasa inaenda kujengwa kwa lami kwa sababu kazi imeshafanyika.”

Pia aliitaja barabara nyingine ya kutoka Bugene – Kasulo (BENACO) yenye urefu wa km. 124 ambayo inatajwa kwenye uk. 75 wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM kwamba ni miongoni mwa barabara zitakazoanza kujengwa upya kwa kiwango cha lami.

 

HOSPITALI YA WILAYA KARAGWE YAKAMILIKA KWA 98%

 



*Mji wa Kayanga kupata barabara za lami, imo ya Murushaka – Murongo

SERIKALI ya Chama cha Mapinduzi (CCM) imetumia sh. bilioni 1.8 kujenga majengo mbalimbali ya hospitali ya Wilaya ya Karagwe ambayo yamekamilika kwa asilimia 98.

Hayo yamesemwa jana (Jumanne, Septemba 29, 2020) na Mjumbe wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya Chama cha Mapinduzi (CCM) Kassim Majaliwa wakati akizungumza na wakazi wa Kata ya Kayanga, katika mkutano uliofanyika kwenye uwanja wa Changarawe, wilayani Karagwe, mkoani Kagera.

Akielezea ujenzi wa vituo vya afya kwenye wilaya hiyo, Majaliwa alisema sh. milioni 900 zimetumika kwa ajili ya ujenzi na ukarabati wa miundombinu mbalimbali ya vituo vya afya ambapo kati ya hizo, sh. milioni 500 zimetumika wa majengo ya kituo cha afya cha Kayanga ambapo kituo hicho kimekamilika na kinatoa huduma.

"Shilingi milioni 400 zimetumika kwa ujenzi wa majengo ya kituo cha afya cha Nyakayanja na ujenzi umekamilika. Pia shilingi bilioni 2.5 zimetumika kwa ajili ya ununuzi wa dawa, vifaa tiba na vitendanishi huku fedha za dawa kwa mwezi zilikuwa ni wastani wa shilingi milioni 53,” alisema.

Akielezea uboreshaji wa miundombinu kwenye wilaya hiyo, Majaliwa alisema ukurasa wa 74-76 wa Ilani ya uchaguzi ya CCM, unaelezea mpango wa serikali kuanza ujenzi mpya (km 6,006.04) na ukarabati wa barabara kwa kiwango cha lami ikiwemo barabara ya Mugakorongo - Kigarama - Murongo yenye urefu wa km 105.

 “Ilani yetu imeenda mbele zaidi na kuelezea mpango wa kukamilisha/kuanza upembuzi yakinifu na usanifu wa kina (km 7,542.75) barabara za mikoa kadhaa ikiwemo barabara ya Murushaka – Murongo yenye km 125.”

Majaliwa ambaye yuko mkoani Kagera kumuombea kura mgombea urais kwa tiketi ya CCM, Dk. Magufuli alitumia fursa hiyo kumnadi mgombea ubunge wa jimbo la Karagwe, Innocent Bashungwa, mgombea udiwani wa kata ya Kayanga na wagombea wa CCM wa kata za wilaya hiyo.

Alisema sh. bilioni 1.4 zimetolewa kupitia Wakala wa Barabara za Mjini na Vijijini (TARURA) kwa ajili ya kufungua barabara mpya, matengenezo ya kawaida, matengenezo ya sehemu korofi, muda maalum na makalvati.

Alisema kati ya hizo, sh. milioni 585 zimetolewa kwa ajili ya matengenezo ya sehemu korofi na baadhi ya maeneo yaliyofanyiwa kazi ni ukarabati katika barabara ya Nyakagoyagoye-Karongoambao uligharimu sh. milioni 31.

Akielezea ukarabati uliofanywa, alisema sh. milioni 19 zimetumika katika barabara ya Kanyabuleza-Runyaga; sh. milioni 14 zimetumika na katika barabara ya Mato-Karehe; sh. milioni 23 zimetumika katika barabara ya Kihanga - Rwabitembe – Mshabaiguru, sh. milioni 16 zimetumika katika barabara yaNyakahanga – Kamahungu, sh. milioni 16 zimetumika katika barabara ya Kishoju – Bujuruga na sh. milioni 23 zimetumika katika barabara ya Igurwa-Kibona-Nyakahita.

Alizitaja barabara nyingine zilizofanyiwa ukarabati kuwa ni Katoju-Ihembe – Bisheshe iliyogharimu sh. milioni 98, barabara ya Kanyabuleza Jct-Makabulini iliyotumia sh. milioni 69, barabara ya KDVTC FADECO iliyotumia sh. milioni 73, barabara ya AMRI – CLASIC iliyogharimu sh. milioni 38 na barabara ya Rukore – Chanikailiyotumia sh. milioni 115.

 

Alisema TARURA ilifanya matengenezo ya madaraja na makalvati katika barabara za Katoju- Rugu - Ruhita (sh. milioni 17), Igurwa-Nyakashozi-Rwentuhe (sh. milioni13),Rukore - Chanika (sh. milioni 12),Rubale - Kibogoizi (sh. milioni 6) na barabara ya Kasheshe - Rubare (sh. milioni 7).

 

“Shilingi milioni 124 zimetumika kwa ajili ya matengenezo maalum katika barabara za Kajunguti - Rubare - Misha (km. 9), Nyabiyonza-Kafunjo(km. 6), Kibaoni Nyabiyonza Sec - Kakuraijo (km. 3.15), Nyakakika - Kandegesho (km.5), Lukole - Kigarama, Lukoyoyo – Kantabire -Nyakasimbi na Ahamulama – Busecha,” alisema.  

 

UTATA WATANDA UINGIZAJI DAWA ZA MIFUGO

 


KAMPUNI ya Multvet Farm Ltd ya jijini Dar es Salaam inadaiwa kuingiza nchini dawa za mifugo na kuzisambaza kwa matumizi kwa kutumia vibali vyenye shaka vya Mamlaka ya Dawa na Vifaa Tiba (TMDA)

Taarifa za uhakika zilizoifikia TANZANIA PANORAMA zimedai kuwa sehemu kubwa ya vifaa hivyo inaagizwa kutoka Afrika Kusini na muagiza amekuwa akilipa kodi zote za serikali lakini katika hatua ya kushangaza amekuwa akitumia vibali vyenye shaka vya TMDA.

Vyanzo vya habari kutoka ndani ya Kampuni ya Multvet vimeeleza kuwa mwenendo huo wa kutumia vibali vyenye shaka ni wa muda mrefu tangu TMDA ilipokuwa ikijulikana kama Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA)

TANZANIA PANORAMA limeiona orodha ya baadhi ya vibali na dawa za mifugo zinazoingiwa nchini kwa kutumia vibali vyenye kutiliwa shaka vinaonyesha kutolewa na TFDA

Moja ya kibali kinachodaiwa kuwa na shaka kilicchoonwa na TANZANIA PANORAMA kinaonyesha kilitolewa Juni 17, 2018 kikiwa na namba TFDA - WEB0518/D/IPER/1032 na kilitumika kuingiza dawa za mifugo kutoka nchini Afrika Kusini.

Alipoulizwa mmoja wa wamiliki wa kampuni hiyo (jina tunalihifadhi) aliyesema yeye siyo msemaji rasmi, kwanza alikanusha kufahamu lolote kuhusu madai hayo lakini alipoelezwa kuwa TANZANIA PANORAMA limeona baadhi ya vibali vinavyodaiwa kutiliwa shaka na dawa ambazo zimekuwa zikiingizwa nchini kwa kutumia vibali vya aina hiyo alisema hayo ni mambo ya zamani na hivi sasa kampuni hiyo ilishaachana nayo.

Alisema hivi sasa yeye na washirika wake wanamiliki kiwanda cha kutengeneza dawa za mifugo lakini alipobanwa kuwa vibali vinavyodaiwa kutumiwa na kampuni yake kuingiza na kumbaza dawa hizo alisema ni kweli jambo hilo liliwahi kutokea na alilipeleka Dodoma kwa wakubwa bila kufafanua alilipeleka kwa wakubwa gani na likichukukiwa maamuzi gani.

Msemaji wa TMDA, Gaudencia Simwaza akizungumzia suala  hilo baada ya TANZANIA PANORAMA kumfikishia alisema taassii yake imelipokea na inaendelea na uchunguzi kabla ya kutoa tamko.

 

WACHINA 'WAOGA' NOTI DAR ES SALAAM



NA MWANDISHI WETU

KAMPUNI mbili za ujenzi za China, China Road and Breadge Corporation (CRBC) na SCG Overseas Tanzania Company Limited zinadaiwa kufanya biashara inayoziingia mabiilioni ya shilingi ambayo hayatozwi kodi.

Sambamba na biashara hiyo inayoyaingizia utajiri mkubwa lakini unaofubaza fuko la fedha zikusanywazwo na Mamlaka ya Mapato (TRA) kama kodi, Kampuni ya CRBC imekusanya na kutia kibindoni mamilioni ya fedha ilizokuwa ikiwakata wafanyakazi wake kama malipo ya pensheni.

Taarifa za uhakika zilizoifikia TANZANIA PANORAMA zimedai kuwa SCG Overseas Tanzania Company Limited ambayo iliingia nchini kwa ajili ya kujishughulisha na  ujenzi wa barabara na madaraja ilipewa msamaha wa kodi wa vifaa vyake vya ujenzi.

Inadaiwa kampuni hiyo ambayo sasa imemaliza shughuli zake hapa nchini, imekuwa ikikodisha vifaa ilivyokuwa ikitumia kwa shughuli zake  za ujenzi vikiwa na msamaha wa kodi kwa Kampuni ya CRBC ambayo huilipa mamilioni ya fedha.

Taarifa zaidi zilizokusanywa na TANZANIA PANORAMA zimeonyesha kuwa biiashara kati ya kampuni hizo mbili, licha ya kuwa yenye thamani kubwa, risiti zinazotolewa  kuthibitisha kufanyika kwa malipo hazitambuliki kwenye mfumo rasmi wa kikodi wa hapa nchini.

"Hawa wachina wa hizo kampuni mbili wanafanya biashara ya mabilioni kwa kukodishiana vifaa na mitambo ya ujenzi. Kiukweli wanaoga fedha hapa Dar as Salaam," alisema mmoja wa watoa taarifa.

Wakati huo huo, CRBC inadaiwa kuweka katika fuko lake ya fedha mamilioni ya shilingi waliyokuwa wakikatwa wafanyakazi wake kama malipo ya pensheni.

Katika mahojiano kati ya badhi ya wafanyakazi wa kampuni hiyo na TANZANIA PANORAMA huku wakiwa na nyaraka zao za malipo ya mshahara mkononi (salary slip) wamedai kwa zaidi ya mwaka mmoja walikuwa wakikatwa pesa katika mishahara yao kwa ajili ya pensheni lakini baada ya mikataba yao ya kazi kuisha wamebaini kuwa fedha hizo zilikuwa haziwasilishwi kwenye mifuko ya jamii.

Alipoulizwa Meneja Rasilimali Watu wa CRBC Alice Charles kuhusu madai hayo alikubali kuzungumzia suala ya malipo ya pensheni huku dai la kuwepo biashara baina ya CRBC na SCG  alisema hilo kwake ni zito na anayeweza kulisemea ni bosi wake aliyemtaja kwa jina moja la Zhang.

Alice alisema madai ya wafanyakazi kukatwa sehemu ya mishahara yao kwa ajili ya pensheni ni ya kweli.

Aidha Alice alieza zaidi kuwa fedha hizo badala ya kuwasilishwa kwenye mifuko ya kijamii zilikuwa zikiingizwa kwenye fuko Kuu la kampuni hiyo kwa sababu wafanyakazi hao walikuwa siyo wanachama wa mifuko hiyo.

Alice aliahidi kuwasiliana na bosi wake Zhang ili azungumzie madai ya kuwepo biashara baina ya CRBC na SCG na kwamba taarifa rasmi angeitoa kwa TANZANIA PANORAMA lakini kwa zaidi ya wiki mbili ameshindwa kutekeleza Ahadi yake hiyo.

Meneja wa Elimu kwa Mlipa Kodi wa TRA, Richard Kayombo alipotafutwa kuzungumzia iwapo taratibu za mamlaka hiyo zinaruhusu vifaa vilivyoingizwa nchini vikiwa na msamaha wa kodi kutumiwa kibiashara, simu yake iliita zaidi ya mara tano bila kupokelewa na hata alipotumiwa maswali kwa ujumbe mfupi kwenye simu yake ya kiganjani, aliyasoma lakini hakujibu chochote.

Jitihada za kumpata balozi wa China kuzungumzia hilo hazikiweza kuzaa matunda baada ya simu kuwa inaita bila kupokelewa.

Mwisho.