KAMPUNI ya Multvet Farm Ltd ya jijini Dar es Salaam
inadaiwa kuingiza nchini dawa za mifugo na kuzisambaza kwa matumizi kwa kutumia
vibali vyenye shaka vya Mamlaka ya Dawa na Vifaa Tiba (TMDA)
Taarifa za uhakika zilizoifikia TANZANIA PANORAMA
zimedai kuwa sehemu kubwa ya vifaa hivyo inaagizwa kutoka Afrika Kusini na muagiza
amekuwa akilipa kodi zote za serikali lakini katika hatua ya kushangaza amekuwa
akitumia vibali vyenye shaka vya TMDA.
Vyanzo vya habari kutoka ndani ya Kampuni ya Multvet
vimeeleza kuwa mwenendo huo wa kutumia vibali vyenye shaka ni wa muda mrefu
tangu TMDA ilipokuwa ikijulikana kama Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA)
TANZANIA PANORAMA limeiona orodha ya baadhi ya
vibali na dawa za mifugo zinazoingiwa nchini kwa kutumia vibali vyenye kutiliwa
shaka vinaonyesha kutolewa na TFDA
Moja ya kibali kinachodaiwa kuwa na shaka
kilicchoonwa na TANZANIA PANORAMA kinaonyesha kilitolewa Juni 17, 2018 kikiwa
na namba TFDA - WEB0518/D/IPER/1032 na kilitumika kuingiza dawa za mifugo
kutoka nchini Afrika Kusini.
Alipoulizwa mmoja wa wamiliki wa kampuni hiyo (jina
tunalihifadhi) aliyesema yeye siyo msemaji rasmi, kwanza alikanusha kufahamu
lolote kuhusu madai hayo lakini alipoelezwa kuwa TANZANIA PANORAMA limeona
baadhi ya vibali vinavyodaiwa kutiliwa shaka na dawa ambazo zimekuwa
zikiingizwa nchini kwa kutumia vibali vya aina hiyo alisema hayo ni mambo ya
zamani na hivi sasa kampuni hiyo ilishaachana nayo.
Alisema hivi sasa yeye na washirika wake wanamiliki
kiwanda cha kutengeneza dawa za mifugo lakini alipobanwa kuwa vibali
vinavyodaiwa kutumiwa na kampuni yake kuingiza na kumbaza dawa hizo alisema ni
kweli jambo hilo liliwahi kutokea na alilipeleka Dodoma kwa wakubwa bila
kufafanua alilipeleka kwa wakubwa gani na likichukukiwa maamuzi gani.
Msemaji wa TMDA, Gaudencia Simwaza akizungumzia
suala hilo baada ya TANZANIA PANORAMA kumfikishia alisema taassii yake
imelipokea na inaendelea na uchunguzi kabla ya kutoa tamko.



