banner

Thursday, October 15, 2020

WEZI WAJA NA MBINU MPYA DAR ES SALAAM

 



NA MWANDISHI WETU

MAGENGE ya uhalifu wa kutumia silaha jijini Dar es Salaam yamebuni mbinu mpya ya kutekeleza vitendo vya kihalifu pasipo watu walio karibu na eneo la tukio kubaini chochote.

Mbinu hiyo ni kuwateka abiria wanaokuwa wamepanda kwenye daladala kisha wahalifu hao huanza kupiga kelele kwa namna ya kushangalia na muziki ndani ya daladala hiyo hufunguliwa kwa sauti ya juu sana.

Katikati ya kelele hizo za muziki na ushagiliaji ndipo wahalifu huanza kushambuliwa abiria waliowapakia kwa visu na bisibisi kabla ya kuwapora fedha na mali wanazokuwa nazo kisha kuwatupa njiani.

Moja ya matukio hayo ya kuogofya lililoshuhudiwa na TANZANIA PANORAMA, limetokea Jumamosi, Oktoba 10, 2020 eneo la kunduchi njia panda ya kwenda Hoteli ya Bahari Beach, ambako daladala lililokuwa na genge wahalifu zaidi ya 20 lilisimama na mmoja wa wahalifu hao akatangaza kuwa linakwenda Makumbusho.

Katika kituo hicho, walipanda abiria watatu akiwemo Mwandishi wa TANZANIA PANORAMA na baada ya kupanda na daladala kuondoka, dereva alifungua muziki kwa sauti ya juu na wahalifu wakaanza kushangilia kwa nguvu kwa staili ya ushangiliaji wa mashabiki wa soka.

"Baada ya kufungua muziki kwa sauti ya juu na wao kuanza kupiga kelele ndiyo wakatoa mapanga na bisibisi wakaanza kutushambulia. Abiria ya kwanza mwanamke ambaye alikuwa ameng'ang’ania pochi yake alikatwa panga mkononi, mkononi ukaning'inia akaachia pochi akaanguka chini wakabembe hadi nyuma ya gari wakaanza kumsachi.

"Mimi nikajaribu kumwambia dreva asimamishe gari kumbe ni mwenzao maana alichomoa upanga mkali akanielekezea huku akinitaka nitulie. Wezi wale wakanivamia na sikuwa mbishi wakanipora na kunichakaza kwa ngumi za kutosha bila kujali kuwa sikutoa upinzani wowote kwao," alisema mwandishi wa TANZANIA PANORAMA.

Alisema gari hilo lilikuwa linaendeshwa kwa mwendo mkali na kabla ya kufika njiapanda ya mbuyuni abiria mmoja ambaye alikuwa amekatwa mapanga mara mbili  mwilini na kuporwa kila kitu alitupwa nje na kuachwa hapo kisha gari likaondoka kwa kasi tena.

"Baada tu ya kukata kona ya mbuyuni gari likashika mwelekeo wa Mwenge lilipunguza mwendo na mimi nikasukumwa nikatupwa hapo lakini nilifanikiwa kukariri namba na rangi za hiyo daladala, kwahiyo kwenye gari wakabaki na mateka mmoja mwanamke waliyekuwa wamemkata mkono" alisema.

Alisema alichukua bodaboda hadi kituo kidogo cha Polisi Mtongoni na kutoa taarifa ya kushambuliwa na kuporwa fedha na mali na kwamba gari hilo likifukuzwa na pikipiki litakamatwa kwa sababu amekariri namba zake na kwamba kuna abiria ndani amekatwa mkono lakini polisi walisema hawana uwezo wa kulifuatilia isipokiwa afunguliwe faili na suala lake litaanza kushughulikiwa Jumatatu.

Alisema alipewa RB namba KMT/RB/2428/2020 pamoja na PF3 kwa ajili ya kwenda kutibiwa na kuelekezwa kufika Kituo cha Polisi Kawe Jumatatu ya Oktoba 12, 2020, asubuhi ambako ataonana na mpelelezi wa kesi na taratibu nyingine kuendelea.

DK. MAGUFULI KUIMARISHA MUUNGANO, DK. MWINYI KUPAMBANA NA UDHALILISHAJI




NA MWANDISHI WETU

MJUMBE wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), Kassim Majaliwa amewataka wakazi wa Zanzibar wamchague Dk. John Pombe Magufuli kuwa rais kwa sababu ndiye mgombea pekee mwenye uwezo wa kudumisha Muungano.

"Nawaletea Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, amefanya makubwa kwenye uongozi wake uliopita. Hata kwenye wizara alizowahi kuongoza, pia amefanya makubwa. Ndiye mgombea pekee mwenye uwezo wa kutuunganisha Wazanzibari na Watanzania Bara,” alisema.

Wito huo aliutoa Jumatatu, Oktoba 12, 2020 wakati akizungumza na wakazi wa Mkoa wa Kaskazini Unguja, katika mkutano uliofanyika kwenye uwanja wa mpira wa Kairo, Kiwengwa, Wilaya ya Kaskazini B.

Alisema wako baadhi ya wagombea wanaotangaza kuuvunja muungano pindi wakichaguliwa na amewataka wananchi wa Zanzibar wawaepuke.

Alisisitiza kuwa kazi ya rais si ya mchezo na inataka mtu makini, kwa hiyo akawaomba wakazi hao wamchangue mtu ambaye ana uwezo wa kupambana na wala rushwa.

Majaliwa yuko Zanzibar kuwaombea kura mgombea urais kwa tiketi ya CCM, Dk. Magufuli, mgombea urais wa Zanzibar kwa tiketi ya CCM, Dk. Hussein Mwinyi, wagombea ubunge wa majimbo, wawakilishi na wagombea udiwani.

Akimuombea kura Dk. Mwinyi, Majaliwa alisema Chama Cha Mapinduzi kina benki ya kutosha ya makada wenye uwezo wa kuongoza. “Chama Cha Mapinduzi kina nafasi nyingi za uongozi na katika nafasi hii ya kuongoza Zanzibar, tumemleta Dk. Hussein Mwinyi.”

Alisema yapo mambo mengi mazuri yamefanywa na Dk. Ali Mohammed Shein na yaliyobakia yatakamilishwa na Dk. Mwinyi. “Masuala yote ya kipaumbele yamewekwa kwenye ilani ya uchaguzi yenye kurasa 303. Pia kitabu hiki kimesambazwa hadi kwenye shehia zenu. Kitafuteni mkisome ili muone mambo yaliyopangwa kufanyika kwa ajili ya Zanzibar.

“Maendeleo ya mifugo yamo humu, maendeleo ya uvuvi yamo humu, maendeleo ya ajira yamo, kuwezesha sekta binafsi yamo humu, kuwezesha viwanda yamo humu, kuwezesha wajasiriamali wadogo, wa kati na wakubwa nayo pia yamo humu,” alieleza.

Mapema, akinadi sera zake, Dk. Mwinyi alisema serikali yake itaimarisha uvuvi wa bahari kuu pamoja na bandari za uvuvi pamoja na ujenzi wa viwanda vya kusindika samaki ili kuongeza ajira na masoko kwa bidhaa za baharini.

Alisema ataimarisha ufugaji wa samaki ikiwa ni njia mojawapo ya kulinda mazingira. “Nitasimamia hilo la ufugaji wa samaki hasa kwenye maeneo ya mikoko kwa sababu tutakuwa pia tunalinda mazingira yetu,” alisema.

Alisisitiza kuwa atashughulikia tatizo la mmomonyoko wa maadili na hasa tatizo la matumizi ya dawa za kulevya na udhalilishaji wa wanawake na watoto. “Ninawaomba mtoe ushirikiano kwa sababu wanaofanya hivi vitendo mnawajua. Tusaidieni ili tuweze kudhibiti hivi vitendo vya udhalilishaji na dawa za kulevya,” alisema.

Akielezea kuhusu sekta ya maji, Dk. Mwinyi alisema upatikanaji wa maji safi na salama umefikia asilimia 72 na kwamba asilimia 28 iliyobakia ni ya kutoa maji kutoka barabara kuu hadi kwenye makazi ya watu. “Serikali yetu itakamilisha hiyo sehemu ndogo iliyobakia,” alisema.

Dk. Mwinyi alitumia fursa hiyo kuomba kura za Dk. Magufuli, Wabunge, Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi na Madiwani wa CCM.

Saturday, October 3, 2020

RAIS DK. MAGUFULI AUZWA KWA REKODI YAKE YA KUTUKUKA

 

NA MWANDISHI WETU

MJUMBE wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya Chama Cha Mapunduzi (CCM), Kassim Majaliwa jana amemuuza mgombea urais wa chama hicho, Dk. John Pombe Magufuli kwa rekodi yake ya kupigiwa mfano ya utendaji kazi.

Majaliwa ameutangazia umma wa Watanzania kuwa mgombea hiyo wa CCM ana rekodi ya kutukuka ya utendaji kazi katika kipindi cha miaka 20 alipokuwa Waziri katika wizara mbalimbali.

Akiwahutubia wakazi wa Ushirombo, Okotoba Mosi katika mkutano wa kampeni uliofanyika Kata ya Igulwa, wilayani Bukombe mkoani Geita, amesema Dt. Magufuli ana rekodi nzuri ya utendaji kazi.

"Dk. Magufuli tunamjua. Alikuwa Waziri katika nchi hii kwa miaka 20. Alikuwa Waziri wa Ujenzi akajenga barabara ambazo sote leo tunaziona. Alipoenda Wizara ya Ardhi, akapiga marufuku watumishi wa wizara hiyo kujilimbikizia viwanja vinne vinne.

"Nimekuja kuwaomba kura zenu. Ni lazima tumpe kura mtu ambaye tunaijua historia yake ya kwamba aliwahi kuwa kiongozi na ameweka historia," amesema.

Majaliwa amewataka wananchi wamchague kiongozi ambaye anaweza kuisimamia Serikali yake.

"Usipokuwa makini unaweza kumpa mtu nchi halafu akashindwa kuisimamia. Kiongozi anayefaa, mwenye uwezo wa kuratibu rasilimali zetu na kuzisimamia, si mwingine bali ni Dk. Magufuli," amesema.

Amehimiza watanzania wawachague wagombea wa CCM ili waweze kuzungumza lugha moja. "Ni muhimu tuwe na madiwani ili waunde baraza lao la madiwani, waongee lugha moja na wapeleke hoja zao kwa mbunge wao," amesema.

Majaliwa ambaye yuko kwenye ziara ya kumuombea kura mgombea urais kwa tiketi ya CCM, Dk. Magufuli alitumia fursa hiyo kumnadi mgombea ubunge wa Jimbo la Bukombe, Dotto Biteko na mgombea udiwani wa Kata ya Igulwa, Richard Mabenga.

"Dk. Magufuli amekuwa rais kwa miaka mitano, aliyoyafanya katika kipindi kifupi tunayaona. Dk. Magufuli huyu, wala rushwa ndiye kiboko yao. Leo niko mbele yako, bila kujali chama chako cha siasa, ninakuomba umpigie kura Dk. Magufuli. Niko mbele yenu, ninawaomba kura za wagombea wa CCM," amesisitiza.

Katika hatua nyingine, Majaliwa amesema Wilaya ya Mbogwe imetengewa sh. bilioni 3.9 kwa ajili ya ujenzi wa ofisi za Makao Makuu ya Wilaya hiyo.

Akielezea kuhusu sekta ya maji, amesema serikali imetoa fedha kwa ajili ya uboreshaji wa miradi ya maji ikiwemo mradi wa maji Kabanga – Nhomolwa ambao ulipatiwa sh. bilioni 1.2. “Fedha nyingine zilizotolewa ni shilingi bilioni 1.3 kwa ajili ya ujenzi wa mradi wa maji Mbogwe ambao utanufaisha maeneo ya Kasosobe, Bwelwa na Iboya.”

Amesema upanuzi wa mradi wa maji Nyakafuru umepatiwa sh. milioni 633 ambao utanufaisha maeneo ya Lulembela na Nyakafuru, Shinyanga A & B pamoja na usimikaji wa nguzo za umeme huko Nyakafuru, Shenda na Masumbwe.

Majaliwa amemaliza ziara yake mkoani Geita na anaendelea kutafuta kura katika Mkoa wa Shinyanga.

WATANZANIA WAASWA KUCHAGUA KIONGOZI ATAKAYEKUZA UHUSIANO WA KIDIPLOMASIA

 

NA MWANDISHI WETU

MJUMBE wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), Kassim Majaliwa amewaasa Watanzania kuchagua kiongozi ambaye atakuza uhusiano wa kidiplomasia na nchi jirani.

“Tanzania inazungukwa na nchi tisa ambazo baadhi yake ziko kwenye Jumuiya ya Afrika Mashariki na nyingine hazimo. Tunahitaji kiongozi ambaye ataweza kuhakikisha nchi hii inakuwa na uhusiano mwema na nchi jirani na nchi nyingine duniani kote lakini pia anayeweza kuilinda heshima ya nchi yetu,” amesema.

Majaliwa ameyasema hayo Alhamisi, Oktoba Mosi, 2020 wakati akizungumza na wakazi wa Kata za Nyakahura na Nyakanazi, wilayani Biharamulo, mkoani Kagera akiwa njiani kuelekea Wilaya za Bukombe na Mbogwe mkoani Geita.

Majaliwa ambaye amemaliza ziara yake mkoani Kagera ya kumuombea kura mgombea urais kwa tiketi ya CCM, Dk. John Pombe Magufuli alitumia fursa hiyo kumnadi mgombea ubunge wa Jimbo la Biharamulo Magharibi, Injinia Ezra Chiwelesa na wagombea udiwani wa CCM wa kata hizo, Apolinary Mgalula na Amos Madegwa.

Akielezea suala la vitambulisho vya uraia, amesema kote alikopita mkoani humo wananchi wanauliza kuhusu kuchelewa kutolewa kwa vitambulisho hivyo.

"Ucheleweshaji huu hauko hapa mkoani Kagera tu bali hata kwenye mikoa ya pembezoni ya Kigoma, Songwe, Katavi, Ruvuma, Mtwara, Lindi, Pwani, Arusha na Mara.

"Hii ni kwa sababu tunataka tujiridhishe na uraia wa waombaji kwani hili suala ni kwa usalama wa nchi yetu. Wale walioko jirani umbali wa km. 10 wanaruhusiwa kuja kutembea au kufanya biashara na kurudi kwao. Hawaruhusiwi kupata vitambulisho, hivi ni kwa Watanzania tu," amesema Majaliwa.

Kiongozi huyo amewahakikishia wakazi hao kwamba kila Mtanzania mwenye sifa atapata kitambulisho cha Taifa kwa kuwa ndiyo mkakati wa Serikali inayoongozwa na Rais Dk. Magufuli.

Majaliwa amesema Idara ya Uhamiaji inatakiwa kuwa makini kusimamia mchakato huo kwa sababu wapo baadhi ya raia wa nchi jirani wanatamani kupata kitambulisho cha Taifa kutokana na amani iliyopo nchini.

"Uhamiaji iwe makini haitapendeza kuona Mtanzania anakosa kitambulisho cha Taifa halafu mgeni kutoka nchi jirani anapata," amesema.

Hata hivyo, amewataka wakazi hao wasikubali kutoa rushwa kwa sababu hiyo ni haki yao na kwamba endapo itatokea wameombwa rushwa watoe taarifa.

"Mtu wa uhamiaji akidai rushwa ili akupatie kitambulisho toa taarifa mara moja ili tumshughulikie," amesisitiza.

WENGI WANAGHUSHI NYARAKA ZA SERIKALI - TMDA

 

NA MWANDISHI WETU

IMEELEZWA kuwa vitendo vya kughushi nyaraka za serikali vinafanywa na Watanzania wengi hapa nchini.

Akizungumza na TANZANIA PANORAMA jana, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Dawa na Vifaa Tiba( TMDA), Akida Khea, alisema siyo jambo jipya wala la kushtusha kwa nyaraka za serikali kughushiwa na kazi ya serikali ni kupambana na uhalifu huo.

Khea alikuwa akitoa ufafanuzi wa mwenendo wa uchunguzi wa tuhuma kuhusu Kampuni ya Multvet Farm Ltd ya jijini Dar es Salaam kuingiza nchini dawa za mifugo na kuzisambaza kwa matumizi kwa kutumia vibali vyenye shaka vya TMDA.

Msemaji wa TMDA, Gaudensia Simwaza ambaye awali alilieleza TANZANIA PANORAMA kuwa taasisi yake inaendelea na uchunguzi wa nyaraka za kampuni hiyo hivyo ipewe muda wa kutosha, jana alipoulizwa alisema mkurugenzi wake mkuu  alitaka kwanza kuzungumza na TANZANIA PANORAMA.

Katika mazungumzo yake na TANZANIA PANORAMA, Khea aliomba mkutano wa ana kwa ana kwa kuialika ofisini kwake Jumatatu, Oktoba 5, 2020 huku akisisitiza kuwa anahitaji kupata msaada utakaosadia uchunguzi unaofanywa taasisi yake.

Alisema, vitendo vya kughushi nyaraka za serikali siyo vipya kwani vimekuwa vikifanywa na watu wengi hivyo vipo kila mara na kwamba serikali imekuwa ikipambana navyo.

"Njoo ofisini tuzungumze, njoo utusaidie. Huyu mtu siyo wa kwanza. Wapo wengi tu. Hivi vitendo vya watu kughushi nyaraka za serikali vinafanywa na watu kila mara na serikali inapambana navyo kikamalifu," alisema Khea.

Inadaiwa kuwa Kampuni ya Multvet Farm Ltd inayoagiza dawa za mifugo kutoka nje ya nchi imekuwa ikitumia vibali vyenye shaka vya TMDA huku akilipa kodi zote za serikali.

Kwamba kampuni hiyo imekuwa ikitumia vibali vyenye shaka vya TMDA kwa zaidi ya miaka minne sasa na baadhi ya wataalamu wa afya ya mifugo wameeleza kuwa dawa ambazo hazijathibitishwa na TMDA kutumika katika mifugo zinaweza kuwa na athari mbaya katika ustawi wa mifugo na kuongeza kuwa hilo linaweza kuwa moja ya mipango ovu ya kuangamiza mifugo hapa nchini.

Mmiliki wa Kampuni ya Multvet Farm Ltd, Dk. Henry Ruhinguka alipoulizwa kuhusu kampuni yake kuelekezewa madai hayo kwanza alikanusha kuwa yeye siyo msemaji wa kampuni hiyo na pia alikanusha kufahamu lolote kuhusu madai hayo.

Hata hivyo uchunguzi wa TANZANIA PANORAMA umebaini kuwa Dk. Henry ndiye mmiliki wa kampuni hiyo na amekuwa mzungumzaji wake mkuu.

Katika mahojiano hayo Dk. Henry baada ya kuelezwa kuwa baadhi ya nyaraka zenye shaka za kampuni yake zilizotumika kuingiza dawa hizo TANZANIA PANORAMA limeziona, alisema, hayo ni mambo ya zamani na hivi sasa kampuni hiyo iliishaachana nayo.

Alisema ni kweli jambo hilo liliwahi kutokea na alilipeleka Dodoma kwa wakubwa  lakini hakufafanua alilipeleka kwa wakubwa gani na maamuzi yaliyochukuliwa.