banner

Wednesday, September 30, 2020

MAJALIWA APOKEA WANACHAMA 20 WA CHADEMA BUKOBA MJINI

 


*Wamo Mwenyekiti wa Vijana wa Mkoa, Naibu Katibu Mkuu Tanzania Bara,

MJUMBE wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Chama cha Mapinduzi (CCM), Kassim Majaliwa leo amewapokea wanachama 20 kutoka Chama cha Demokrasia (CHADEMA) ambao wameamua kurudi CCM. 

Wanachama hao wameongozwa na Mwenyekiti wa Vijana wa CHADEMA wa Mkoa wa Kagera, Francis Mutachunzibwa ambaye pia alimtambulisha aliyekuwa Naibu Katibu Mkuu wa BAVICHA, Getrude Ndibalema ambaye alijiuzulu uongozi tangu mwaka jana.

Akizungumza kwa niaba ya wenzake, Mutachunzibwa amesema: “Ninaijua vizuri CHADEMA, nilipotea, nilitenda dhambi lakini sasa nimeamua kurudi nyumbani, nipokeeni.

“Ninawaomba wana-Bukoba tumchague Dk. Magufuli, mashine ya kusaga na kukoboa, jembe la nguvu. Kuanzia kesho, nitamnadi yeye na Advocate Byabato hadi kieleweke," amesema.

Akizungumza na maelfu ya wakazi wa mji wa Bukoba leo jioni, waliojitokeza kwenye mkutano uliofanyika uwanja wa Mashujaa, Manispaa ya Bukoba, mkoani Kagera, Majaliwa aliwataka wakazi hao wajitafakari sana wanapofikiria kumchangua mtu wa kuongoza nchi.

“Tunataka kiongozi mwenye hofu ya Mungu na ili umpate ni lazima umjue historia yake. Kuongoza nchi si lelemama, kiongozi wa nchi ni Mkuu wa Nchi, tena ni Mkuu wa Majeshi," amesema Majaliwa.

Majaliwa ambaye ameanza ziara katika Mkoa wa Kagera kumuombea kura mgombea urais kwa tiketi ya CCM, Dk. John Pombe Magufuli, ametumia fursa hiyo kuwaombea kura mgombea ubunge wa jimbo la Bukoba Mjini kwa tiketi ya CCM, Wakili Steven Byabato, mgombea udiwani wa Kata ya Bilele, Tawfiq Sharif Salum na madiwani wengine wa jimbo hilo.

Aliwasimamisha wazee wa Kagera wakiwemo aliyekuwa Meya wa Bukoba, Dk. Anatoly Amani, aliyekuwa mbunge wa jimbo hilo, Balozi Khamis Kagasheki ambao wote waliomba kura za Dk. Magufuli, Wakili Byabato na madiwani wa jimbo hilo.

Kwa upande wake, aliyekuwa Waziri wa Viwanda, Charles Mwijage, amesema Muleba wana ajenda ya kuhakikisha kura zote zinaenda kwa Dk. Magufuli na wabunge wa CCM na akawataka wana-Bukoba nao wafanye hivyo ili kuhakikisha majimbo yote tisa yanabakia CCM na pia wanapata wabunge wanne wa viti maalum.

MSIDANGANYIKE KUHUSU BEI YA KAHAWA - MAJALIWA

 



NA MWANDISHI WETU

MJUMBE wa Kamati kuu ya Halmashauri Kuu ya Chama cha Mapinduzi (CCM), Kassim Majaliwa amesema serikali imedhamiria kuhakikisha kilimo kinamnufaisha mkulima wa Tanzania. 

"Watu wasije kuwadanganya kwamba serikali haiwajali, siyo kweli. Kuna sababu zilizochangia kuyumba kwa bei ya kahawa kwenye soko la dunia."

Ametoa kauli hiyo leo mchana alipokuwa  akizungumza na wakazi wa Rubale Latina mkutano uliofanyika kwenye viwanja vya shule ya msingi Rubale, wilayani Bukoba, mkoani Kagera.

"Serikali ya awamu ya tano ilipoingia madarakani, iliazimia kufufua mazao matano ya kimkakati ambayo ni kahawa, pamba, korosho, chai na tumbaku. Mazao haya bei ilishuka na si katika zao la kahawa tu.

"Kuyumba kwa bei haikuwa katika zao la kahawa tu bali katika mazao mengine kama pamba na korosho. Kahawa bei yake iliathirika kwa sababu ya ugonjwa wa Corona. Korosho bei ilishuka kutoka sh.3,300 hadi sh. 1,900. Pamba pia ilishuka bei," amesema. 

Amesema Kenya ndiko mnada wa kahawa huwa unafanyika lakini hadi sasa bado wanasumbuliwa na ugonjwa wa Corona kwa hiyo haikuwa rahisi kufanya biashara katika kipindi chote hicho.

Majaliwa ambaye ameanza ziara katika Mkoa wa Kagera kumuombea kura mgombea irais kwa tiketi ya CCM, Dk. John Pombe Magufuli ametumia fursa hiyo kuwaombea kura mgombea ubunge kwa tiketi ya CCM, Jason Rweikiza, mgombea udiwani wa kata ya Rubale, Rwegasira Renatus Rwechungura na madiwani wengine wa jimbo hilo.

Kuhusu maji, amesema sh. bilioni 4.09 zilitolewa ili kuboresha miradi ya maji katika vijiji kadhaa ambayo yote imekamilika. Almevitaja vijiji hivyo kuwa ni  Ibwera, Kasharu, Kitahya, Katale, Itongo, Bituntu, Kibona, Katoro, Mikoni, Kibirizi Ngarama, Ruhoko na Ruhunga.

Saturday, September 26, 2020

KISIWA CHA GANA KUPATIWA KIVUKO KIPYA


NA MWANDISHI WETU

CHAMA cha Mapinduzi (CCM), kimeahidi kutoa kivuko kwa wananchi wa kisiwa cha Gana, kilichopo Kata ya Ilangala, wilayani Ukerewe.

Ahadi hiyo imetolewa jana (Ijumaa, Septemba 25, 2020) na Mjumbe wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya CCM, Kassim Majaliwa katika mkutano wa kampeni uliofanyika kitongoji cha Gana.

Katika mkutano huo, Majaliwa alimnadi mgombea ubunge wa Jimbo la Ukerewe kupitia tiketi ya CCM, Joseph Mkundi na madiwani. Pia Majaliwa aliwataka wananchi wa Gana wamchague mgombea urais kwa tiketi ya CCM, Dk. John Pombe Magufuli katika uchaguzi mkuu ujao wa urais, wabunge na madiwani utakaofanyika Oktoba 28, mwaka huu.

Akitoa ahadi hiyo mbele ya wananchi wa kisiwa cha Gana, Majaliwa alisema uamuzi huo ni utekelezaji wa Ilani ya uchaguzi ya CCM ya mwaka 2020-2025 yenye kurasa 303. Kivuko hicho kitatoa huduma kati ya Kakuru na Gana.

Alisema Ilani ya CCM imetoa maelekezo kwa Serikali ijayo itekeleze idadi kubwa ya miradi ya kimkakati ikiwemo kuboresha usafiri wa majini ili kuwandolea adha wananchi wanaoishi katika maeneo ya visiwani.  

Majaliwa alisema wananchi zaidi ya 3000 wa Gana, wanahitaji kivuko bora ambacho kitatoa fursa kwao kufanya shughuli za uvuvi na biashara ili kujipatia kipato.

"Hapa Gana tutaleta kivuko, hiki kisiwa ni kikubwa kina idadi kubwa ya watu ambao wanahitaji huduma bora ya usafiri wa majini. Serikali yenu imeweka mipango mizuri kwa ajili yenu," alisema Majaliwa.

Alisema chama kitaendelea kutekeleza Ilani yake kwa vitendo kwa kuboresha huduma za wananchi katika visiwa vyote nchini ikiwemo wilaya ya Ukerewe mkoani Mwanza yenye visiwa 38.

Mbali na kutoa ahadi ya kivuko, Majaliwa alisema Serikali ijayo itapeleka boti za doria kulinda usalama wa wavuvi ambao wakati mwingine wanafanya shughuli zao kwa mashaka wakihofia uvamizi wa majambazi wanaotoka nchi jirani.

Kwa upande wake, Mkundi alisema kipaumbele cha kwanza baada ya kuingia bungeni ni kuhakikisha Serikali ijayo inaboresha huduma ya afya kwa kujenga idadi kubwa ya zahanati ndani ya kisiwa hicho.

"Gana tuna changamoto ya zahanati, umeme na maji. Nitakuwa daraja zuri kati yenu na Serikali ili kuhakikisha huduma hizi zinawafikia kwa haraka naomba mumchague Rais Magufuli ili mambo yetu yaende vizuri," alisema Mkundi.

Paschal Bukuru ambaye ni mfanyabiashara ya duka, alisema ujio wa kivuko utakuwa mkombozi kwa wananchi wa Gana, kwa kuwa muda mrefu wamekuwa wakitumia mitumbwi kwenda Nansio kufuata mahitaji.

Bukuru alisema wafanyabiashara wamekuwa wakipata changamoto ya kuleta bidhaa zao wakitokea Nansio kwa kuwa hawana usafiri wa uhakika, hivyo ujio wa kivuko hicho utakuwa na manufaa makubwa kwao.

Katika kipindi cha miaka mitano ijayo, CCM imeahidi kuboresha vivuko ikiwemo ujenzi wa kivuko cha Rugezi-Kisorya (Mwanza). Pia ujenzi wa vivuko vipya vinane utaanza ambao ni Ijinga-Kahangala (Mwanza), Musoma-Kinesi (Mara), Nyamisati-Mafia (Pwani), Msangamkuu-Msemo (Mtwara), Nyakalilo-Kome (Mwanza), Bwiro-Bukondo (Ukerewe), Irugwa-Murutanga (Ukerewe) na Kakuru – Ghana (Ukerewe).

 

KIWANDA CHA TANGAWIZI SAME KUANZA UZALISHAJI NOVEMBA

 






NA PIUS NTIGA, SAME

KIWANDA cha kuchakata zao la Tangawizi kilichopo Wilaya ya Same mkoani Kilimanjaro kitaanza kuchakata zao Novemba mwaka huu baada ya kupata mwekezaji.

Kiwanda hicho kilianzishwa mwaka 2012 kikimilikiwa na Chama cha Ushirika cha Tangawizi Mamba, Miamba lakini kiliharibika muda mfupi baadaye na hivyo kusikitisha shughuli zake.

Mkurugenzi wa Uwekezaji wa (PSSSF), Fortunatus Magambo ambao ndiyo mwekezaji mpya wa kiwanda hicho jana amekabidhi kwa menejimenti mashine za kuchakata Tangawizi zilizotolewa na mfuko huo mbele ya Mkuu wa Wilaya ya Same, Rosemary Senyamule

Katika mkutano na wananchi wa Mamba, Miamba ambao ulihudhuriwa pia na Amsha Amsha 2020 ya Uhuru FM kijijini hapo, Magambo amesema mashine hizo za kisasa zimenunuliwa nchini China kwa gharama ya sh bilioni 1.83  na zinafanya kazi bila kutoa sauti.

Kwa mujibu wa ubia huo, PSSSF ina hisa ya asilimia 60 huku 40 zikiwa za wananchi wa Wilaya ya Same ambao zao lao kuu la Biashara ukiachia Mkonge ni Tangawizi.

Aidha, amesema kiasi cha sh milioni 800 zitatumika kwa ajili ya ujenzi na ukarabati wa majengo ya kiwanda, ofisi, hospitali, Karakana na miundombinu pamoja na matumizi ya awali ya kiwanda hicho.

"Tunataka kuona mradi huu unakamilika na kusaidia kuboresha hali ya maisha ya wananchi wa Same na utakamilika kwa wakati

"Wataalamu kutoka China wanatarajiwa kuwasili nchini mwezi Oktoba mwaka huu kwa ajili ya kufunga mashine hizi tayari kwa kuanza uzalishaji," alsema Magambo.

Naye Mkuu wa Wilaya ya Same, Rosemary Senyamule, amewaambia wananchi waliohudhuria mkutano huo kuwa serikali ya awamu tano imejipambanua kuwa ni ya Tanzania ya viwanda, hivyo uwepo wa kiwanda hicho utachochea kukuza vipato vyao na taifa kwa ujumla.

Amesema tani 5,000 kwa mwaka zinahitajika kiwandani hapo, hivyo akawataka wakulima kuongeza uzalishaji wa Tangawizi ambayo itakuwa inasindikwa hapa hapa nchini kwa matumizi ya hapa nchini na nje ya nchi.

Aidha, DC Rosemary amesema soko la Tangawizi litakuwa kubwa baada ya uzalishaji kuanza.

Pia amewataka wananchi kuwapuuza Wanasiasa wakiwemo wa upinzani wanaojipitisha kwao wakidai kuwa mashine za kiwanda hicho wamezileta wao wakati zimeletwa na serikali ya awamu ya tano.

"Wananchi wangu wa Same hasa hapa Mamba,  Miamba, Corona ilichelewesha ufungaji wa  mashine hizo lakini sasa zipo hapa na nyie leo mmeshuhudia, hivyo muda wowote zitaanza kufanya kazi, endeleeni kuiunga mkono serikali yenu" alisema DC Rosemary

Wakizungumza na Amsha Amsha 2020 ya Uhuru FM, baadhi ya wananchi akiwemo Mzee Ndimangwa Manento, aliyetoa shamba lake kwa ajili ya kujengwa kiwanda hicho cha Tangawizi, wameishukuru serikali kwa kusikiliza kilio chao cha kuleta mashine za kisasa zisizo na sauti na akawaomba wananchi wenzake mwaka huu wasifanye makosa katika uchaguzi mkuu wakampigie kura nyingi Rais Magufuli, wabunge na madiwani wa CCM.

Wakati huo huo, zaidi ya sh milioni 400 zimetumika kujenga majengo mapya ya kituo cha afya cha Ndungu ikiwemo maabara, chumba cha kuhifadhi maiti, jengo la upasuaji, pamoja na wodi ya akina mama wajawazito. 

Hayo yamesema na Afisa Mipango wa Halmashauri ya Same,  Simion Mzee wakati akizungumza na Amsha Amsha 2020 ya Uhuru FM.

Nao baadhi ya wananchi wa Ndungu akiwemo Hatibu Mlindoko, wamepongeza serikali kwa kuwajengea kituo hicho cha afya na wakaiomba kupandisha hadhi kituo hicho ili kiwe  Hospitali.

Kaimu Mganga Mkuu kituo hicho, Hamis Waziri Juma amesema kabla ya majengo hayo walikuwa wanatoka rufaa nyingi kwenda Hospitali ya Wilaya ya Same kwa ajili ya matibabu lakini sasa wajawazito wanajifungua katika kituo hichi na hivyo kupunguza gharama ya wanachi kuwapeleka Same.

Katika hatua nyingine, zaidi ya sh milioni 60 zimetumika kwa ajili ya ukarabati wa shule Kongwe ya Sekondari ya Same katika miaka mitano ya serikali ya awamu ya tano chini ya Rais Magufuli.

Mkuu wa Shule hiyo iliyoanzishwa mwaka 1954 Mwalimu Hoza Mgonja, amesema  Majengo 24 yamekarabatiwa yakiwemo Mabweni, Jiko,  Madarasa, Maabara, Zahanati, Ofisi na kujenga Tenki la Maji kwa ajili ya matumizi ya Shule hiyo ambayo sasa ni ya Kidato cha Tano na Sita.

Wakizungumzia mafanikio hayo baadhi ya Wanafunzi wamesema Shule hiyo sasa imekuwa ya kisasa baada ya Majengo ya zamani kubadilishwa na kujengwa mapya imesaidia pia kuongeza ufaulu na walimu kufundisha katika mazingira mazuri na wameipongeza Serikali.

Aidha, shilingi Milioni-25 zimepelekwa na serikali kukarabati na kujenga  Ofisi na Madarasa Mawili katika Shule ya Sekondari Mamba, iliyopo Kata ya Mamba, Miamba Wilayani Same Mkoani Kilimanjaro.

Kiasi hicho cha fedha kimetajwa na Mkuu wa Shule hiyo Elizabet Irira, ambaye pia ameipongeza serikali kwa kupeleka kiasi hicho cha fedha Shuleni hapo, hatua ambayo pia imepongezwa na Wanafunzi wa Shule hiyo iliyopo Milimani Kilometa 90 kutoka Mjini Same hadi Mamba, Miamba.

Friday, September 25, 2020

SABUNI ILIYO PIGWA MNADA NA TRA SIYO SALAMA




NA MWANDISHI WETU

SABUNI ya Unga ambayo muda wake wa matumizi umeisha lakini imeuzwa kwa njia ya mnada na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) siyo salama hivyo haifai kutumiwa.

Tahadhari hiyo imetolewa jana na afisa mwandamizi wa Shirika la Viwango (TBS), jina lake tunalihifadhi wakati akizungumza na TANZANIA PANORAMA kuhusu madhara yanayoweza kuwapata watu watakaotumia bidhaa hiyo.

Akijibu hilo, amesema ni kosa kuuza au kusambaza bidhaa ambayo muda wake wa matumizi umeisha na siyo salama kuitumia ingawa matatizo ya kiafya yanayoweza kumpata mtumiaji ni suala la kitabibu na inategemea kemikali zilizotumika kuitengeneza.

"Matatizo ya kiafya ni suala la kitabibu na inategemea kemikali gani kwa sababu sabuni zinatofautiana 'composition' ya kemikali lakini itoshe tu kusema tu bidhaa yoyote iliyo'expire' haifai na siyo salama kwa matumizi na anayeuza hatendi haki," alisema afisa huyo.

Mkemia Mkuu wa Serikali, Daniel Ndiyo alipoulizwa kuhusu suala hilo alisema wanaoweza kulizungumzia ni TBS.

Mapema mwezi huu TRA imeuza kwa njia ya mnada shehena ya sabuni ya unga ambayo muda wake wa matumizi umeisha.

Shehena hiyo ya sabuni isiyofaa kutumika baada ya muda wake kuisha iliingizwa nchini kutoka nje na kukaa bandarini bila kulipiwa ushuru kwa muda mrefu kabla TRA haijaamua kuiuza.

Habari za uhakika zilizokusanywa na TANZANIA PANORAMA zimeonyesha kuwa shehena hiyo ni ya mifuko 1,800' ya sabuni ya unga aina ya AKO na imeuzwa kwa njia ya mnada na maafisa wa TRA huku wakijua kuwa wanatenda kosa linaloweza kuwa na athari mbaya kwa watakaoitumia sabuni hiyo.

Thamani ya sabuni hiyo ni sh milioni 300 na kabla ya kunadiwa ilikuwa imehifadhiwa katika bandari kavu (ICD) ya Kampuni ya Azam

Mkurugenzi wa Elimu kwa Mlipa Kodi wa TRA, Richard Kayombo alithibitisha kuuzwa kwa shehena hiyo ingawa kabla ya kuthibitisha alikanusha na kutaka atumiwe ushahidi.

Katika majibu yake, Kayombo alisema "Sasa bwana ni hivi. Ni kweli huo mzigo unaousema ni kweli ulikuwepo TRA. Ni kweli kabisa. Na mnada wake wa kwanza ulikuwa Agosti 24, 2020 lakini aliyeshinda hakuja kulipa hivyo ikabidi ufanyike mnada mwingine ndiyo ukauzika

" Ni kama kulikuwa na pande mbili zilizokuwa zikiushindania kwa sababu yule mnunuzi wa kwanza hakuja kulipa hivyo ikabidi ufanyike mnada mwingine ndipo shehena ile ikachukuliwa kwa sh. milioni 21.5."