banner

Wednesday, December 16, 2020

UBUNGO INTERCHANGE PICHA HALISI YA WATANZANIA


 

 NA MWANDISHI WETU

BARABARA za juu zilizopo eneo la Ubungo zinazofahamika zaidi kwa jina la Ubungo Interchange ni picha halisi ya uchapakazi, uwezo wa kiuchumi na utaalamu wa Watanzania.

Kila mtumiaji wa barabara hizo, awe mtanzania au raia wa kigeni licha ya kuvutiwa na uzuri wake anapopita juu yake, picha ya raia wazalendo wa Watanzania wanaoipenda nchi yao, pia humjia akilini.

Ubungo Interchange imejengwa na vijana wa kitanzania waliokuwa asilimia 90 ya wajenzi wote, imesimamiwa na wataalamu wa ndani ya Tanzania ambao ni Wakala wa Barabara (TANROADS) wakiongozwa na Mtendaji Mkuu, Patrick Mfugale huku meneja mradi akiwa Mhandisi Barakaeli Mmari.

Mfugale


Saruji, mchanga, nondo na vifaa vingine vyote vilivyotumika katika ujenzi wa barabara hizo kwa kiwango kikubwa ama zimetengenezwa na kuzalishwa na viwanda vya ndani vya Tanzania au ni vifaa vilivyo ndani ya Tanzania. Ubungo Interchange ni barabara za Watanzania zilizojengwa na Watanzania kwa kutumia akili, fedha, vifaa na nguvu kazi ya Watanzania wenyewe.

Barabara hizo za kuvutia katika ukanda wote wa Afrika Mashariki zinakutanisha barabara tatu za Mandela, Sam Nujoma na Morogoro na ujenzi wake ulikamilika Disemba, 2020.

Rais Magufuli


Rais John Pombe Magufuli alipotangaza mpango wa ujenzi wa barabara hizo kulikuwa na mapokeo ya aina mbili, kwanza ni Watanzania waliopokea taarifa za mpango huo kwa furaha kwa imani kwamba zitapunguza au kuondoa kabisa tatizo la msongamano wa magari katika eneo la Ubungo ambalo lilikuwa likidumaza sana uchumi wa mtu mmoja mmoja na taifa kwa ujumla.

Furaha hiyo pia ilijengeka katika nyuso za wananchi wengi kwa matumaini ya kupata ajira na zaidi ni tamaa ya maendeleo. Kila Mtanzania alitamani kuiona Tanzania ikiwa na interchange yenye mwonekano wa zile zilizo kwenye mataifa ya dunia ya kwanza

Mapokeo ya pili yalikuwa ya husda kutoka kwa maadui wa taifa ambayo nayo yaligawanyika katika makundi mawili makuu; la kwanza ni lile lililotamani mpango huo usifanikiwe na sababu yao kubwa ni kutotaka kuiona Tanzania ikipiga hatua za kimaendeleo huku kundi jingine ni lile lililotaka lihusike kwenye ujenzi ili kwanza livune pesa na kutoa ajira kwa watu wao ambao haina shaka wangeletwa kwa wingi kufanya kazi kwenye mradi huo na pia kutamani Tanzania iendelee kuwa tegemezi kwa kukosa pesa za ujenzi au kuomba msaada na wataalamu kutoka nje.

Matamanio haya yamekuwa hewa kwa sasa ambapo Watanzania wengi wanayaishi maono na falsafa za Rais Magufuli zinazowafanya watembee kifua mbele kwa sababu wanaamini wanaweza kuijenga nchi yao wenyewe na TANROADS imekuwa mfano bora kabisa katika hili.



Mei 2020, Mhandisi Barakaeli Mmari alipoutangzia umma kuwa kwa mara ya kwanza barabara ya ghorofa ya chini ya Morogoro itafunguliwa kwa majaribio ifikapo Mei 30, 2020 kwa kuruhusu magari kupita na Septemba 30, 2020 barabara ya ghorofa ya pili ya Nelson Mandela / Sam Nujoma itafunguliwa kwa majaribio pia, Watanzania na raia wa nchi jirani wanaotumia barabara ya Morogoro kama lango kuu la kuingilia jijini Dar es Salaam walianza kushuhudia picha halisi ya Tanzania mpya.



Mhandisi Mmari ambaye alitoa darasa la matumizi ya barabara hizo alisema kuna barabara ngazi tatu, ya chini, ya kati na ya juu. Ngazi ya chini itatumiwa na magari yanayotoka mjini kwenda Mwenge, Mwenge-Kimara, Kimara-Buguruni na Buguruni kwenda mjini. Vile vile, itatumiwa na magari yote yatakayokuwa yanapinda kushoto kwenye maungio hayo.

Alisema ngazi ya kati itatumiwa na magari yanayotoka Kimara kwenda mjini na yatokayo mjini kwenda Kimara.



Ngazi ya juu itatumiwa na magari yatokayo Mwenge kwenda Buguruni na yatokayo Buguruni kwenda Mwenge.

Mhandisi Mmari alisema barabara za juu zimejumuisha njia maalumu kwa ajili ya mabasi ya mwendo kasi.



Hivi sasa, Watanzania wakiwa wamezama katika ujenzi wa miradi mikubwa ya kitaifa, picha halisi ya ubora wa miradi hiyo inaonekana kwa kutazama na kupita juu ya barabara za ghorofa za Ubungo Interchange.

GULAM ATAFAKARI KUPAMBANA NA UBALOZI WA INDIA

 

Mwenyekiti wa Kampuni za MeTL, Gulam Dewji

NA MWANDISHI WETU

MFANYABIASHARI mwenye ukwasi wa kutosha ambaye kampuni, viwanda, mashamba na biashara zake zimetoa ajira kwa Watanzania na raia wa kigeni anatafakari kujibu mapigo dhidi ya Ubalozi wa India uliyoyataja makampuni yake kuwa siyo sehemu salama kufanya kazi.

Wiki iliyopita, siku moja baada ta Gulam kumpa maagizo mmoja wa wasaidizi wake kutuma ujumbe kwa Tanzania PANORAMA Blog wa kusaka suluhu baina ya menejimenti za Kampuni za Mohamedi Enterprises Tanzania Limited (MeTL) na wafanyakazi wa kigeni wanaodai kunyanyaswa alisema anajipanga kujibu mapigo.

Gulam alisema amesikitisha na tamko la ubalozi wa India lililosambazwa mitandaoni kwa sababu linalenga kuwatetea watu wanaomuibia na kumsumbua.

“Ndiyo nimeliona tamko kwani nani kasema hajui kuwa ni tamko la Ubalozi wa India, lakini mimi nasema nakusanya ushahidi halafu nitatoa tangazo kwa vyombo vya habari kwa sababu ubalozi unatetea wezi, unatetea watu wanaoniibia na kunitesa sana na hata polisi wanazo taarifa hizi. Sasa ninazungumza na ubalozi halafu nitatoa statement yangu ambayo mimi nitaitoa kama tangazo,” alisema Gulam.   

AWALI Tanzania PANORAMA Blog, iliripoti kuwa uongozi wa kampuni zilizo chini ya mwamvuli wa Mohamedi Enterprises Tanzania Limited (MeTL) umesema utatafuta njia ya kumaliza mgogoro baina yake na wafanyakazi ambao ni raia wa India katika meza ya mazungumzo.

Hayo yameelezwa na mmoja wa maafisa wa kampuni hiyo aliyetumwa na Mkurugenzi wa MeTL, Gulam Dewji kutoa ufafanuzi kwa Tanzania PANORAMA Blog kuhusu andishi lililowekwa kwenye mitandao ya kijamii likiwatahadhalisha raia wa India wote kuepuka kufanya kazi katika Kampuni za MeTL.

Andiko hilo mtandaoni linaeleza kuwa Ubalozi wa India umekuwa ukipokea kwa mfululizo malalamiko ya wafanyaakazi wa Kampuni za MeTL kunyanyaswa na uongozi pamoja na mwajiri wao kuwafungulia kesi za kughushi mahakamani kiasi cha kusababisha wanafamilia wa wafanyakazi hao kulazimika kurejea India.

Kwamba Mwenyekiti wa Makampuni ya MeTl, Gulam Dewji na maafisa waandamizi wamekuwa wakiwafanyia vitendo vya unyanyasaji na udhalilishaji wafanyakazi hao wanapofikisha malalamiko kwao.

Linahitimishwa kwamba raia wote wa India wasikubali kuajiriwa na Kampuni za MeTL kutokana na mwenendo usiofaa wa viongozi wake wa juu.

Alipoulizwa Mwenyekiti Gulam, kuhusu suala hilo kupitia simu yake ya kiganjani alisema aandikiwe maswali kwa maandishi ili ayajibu na alipoandikiwa, muda mfupi baadaye mtu mmoja mwenye asili ya kiasia alituma ujumbe kwa njia ya whatsapp akieleza kuwa ametumwa na Gulam kufikisha ujumbe kwa Tanzania PANORAMA Blog.

Ujumbe aliuotuma ulisomeka; ‘Bwana Dewji amezungumza na sisi na ametuhakikishia uwajibikaji wa menejimenti katika kulinda maslahi ya wafanyakazi. Tumekubaliana kuwa na mazungumzo ya kina, tungependa kutatua jambo hili kwa njia ya mazungumzo.’

Ujumbe mwingine chini ya huo aliuotuma ulisomeka; ‘leo hii mmelalamika mazingira ya watu wenu ila tusema ukweli pia mnawanyanyasa sana Watanzania sema tu wanashindwa nani wa kuwasemea pia kutokana na hali za maisha yao ila mazingira ya ufanyaji kazi siyo.

Jitahidi za Tanzania PANORAMA Blog kuzungumza na Ubalozi wa India kuhusu suala hili zinaendelea.    

MWANAFUNZI ALIYEPOTEA ST. MARY’S APATIKANA

 

Labna Said

NA MWANDISHI WETU

LABNA Salim Said,  mwanafunzi wa Shule ya Sekondari ya Bweni ya St. Mary’s iliyopo Mbezi Makonde ambaye alipotea tangu Oktoba 4, 2020, amepatikana.

Mwanafunzi huyo alipatikana Disembe 12, 2020, eno la Banana Relini akiwa amewekwa kinyumba na mwanaume ambaye jina lake halikufahamika mara moja baada ya kufanikiwa kuwakimbia polisi waliokwenda kuwakamata.

Taarifa za kupatikana kwa Labna zilithibitishwa na Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Kipolisi Kinondoni (RPC) Ramadhani Kingai katika mahojiano mafupi kwa njia ya simu ambaye alisema, taarifa za kupatikana kwa mwanafunzi huyo anazo lakini hawezi kuongea zaidi kwa sababu yupo kwenye kikao.

Mama mzazi wa Labna anayefahamika kwa jina la Rabia Swedan alisema walipata taarifa za kuwepo kwa mtoto wao eneo Banana Relini usiku na walifika eneo hilo wakiwa wameambatana na polisi wawili na kumkuta akiwa amelala chini pamoja na aliyemtorosha.

“Inasikitisha, tulipata taarifa za huyu mtoto kuwepo Banana Relini usiku, tukaenda Kituo cha Polisi Stakishari kuomba polisi, tukapewa wawili tukaambatana nao mpaka kwenye hiyo nyumba tukawakuta wamelala chini. Yule bwana aliyekuwa naye alipotuona na polisi akakurupuka akakimbia, sasa kwa sababu polisi walikuwa wawili hawakuweza kumfukuza.

“Mtoto alikuwa hoi, tulimpeleka Stakishari polisi huo usiku wa saa saba akakaa hapo wakimuhoji mpaka saa 12.00 asubuhi, kwa jinsi alivyokuwa wakatuambia tumpeleke hospitali.

“Tukampeleka Hospitali ya Amana na baada ya matibabu tukamchukua hadi Kituo cha Polisi Goba kwa sababu ndiko kesi yake inakopelelezwa, nao  wakamuhoji wakaturudishia tuendelee kumtibu ila akiwa na nafuu tutampeleka tena polisi,” alisema Swedan.   

Mwanafunzi msichana Labna wa Shule ya Sekondari ya Bweni ya St. Mary’s iliyoko Mbezi Makonde alitoweka shuleni tangu Oktoba 4, 2020 na kutokomea kusikojulikana hadi alipopatikana Disemba 12.

Labna alitoweka akiwa chini ya uangalizi wa shule lakini taarifa za kutoweka kwake zilitolewa Oktoba 8, 2020 na matron wake, Sarah Murra aliyempigia simu mama mzazi wa Labna akiulizia kama ameishafika nyumbani.

Katika hatua ya kushangaza, uongozi wa Shule ya Sekondari ya St Mary’s haukutoa taarifa polisi kuhusu kutoweka kwa mwanafunzi huyo na badala yake wazazi ndiyo walioripoti tukio la mtoto wao kupotea akiwa shuleni.

 

 

Thursday, December 10, 2020

MeTL YAZUNGUMZIA TUHUMA ZINAZOIANDAMA

 

Mwenyekiti wa Makampuni ya MeTL, Gulam dewji

NA MWANDISHI WETU

UONGOZI wa Kampuni zilizo chini ya mwamvuli wa Mohamedi Enterprises Tanzania Limited (MeTL) umesema utatafuta njia ya kumaliza mgogoro baina yake na wafanyakazi ambao ni raia wa India katika meza ya mazungumzo.

Hayo yameelezwa na mmoja wa maafisa wa kampuni hiyo aliyetumwa na Mkurugenzi wa MeTL, Gulam Dewji kutoa ufafanuzi kwa Tanzania PANORAMA Blog kuhusu andishi lililowekwa kwenye mitandao ya kijamii likiwatahadhalisha raia wa India wote kuepuka kufanya kazi katika kampuni za MeTL.

Andiko hilo mtandaoni linaeleza kuwa Ubalozi wa India umekuwa ukipokea kwa mfululizo malalamiko ya wafanyaakazi wa Kampuni za MeTL kunyanyaswa na uongozi pamoja na mwajiri wao kuwafungulia kesi za kughushi mahakamani kiasi cha kusababisha wanafamilia wa wafanyakazi hao kulazimika kurejea India.

Kwamba Mwenyekiti wa Makampuni ya MeTl, Gulam Dewji na maafisa waandamizi wamekuwa wakiwafanya vitendo vya unyanyasaji na udhalilishaji wafanyakazi hao wanapofikisha malalamiko kwao.

Linahitishwa kwamba raia wote wa India wasikubali kuajiriwa na Kampuni za MeTL kutokana na mwenendo usiofaa wa viongozi wake wa juu.

Gulam

Alipoulizwa Mwenyekiti Gulam, kuhusu suala hilo kupitia simu yake ya kiganjani alisema aandikiwe maswali kwa maandishi ili ayajibu na alipoandikiwa, muda mfupi baadaye mtu mmoja mwenye asili ya kiasia alituma ujumbe kwa njia ya whatsapp akieleza kuwa ametumwa na Gulam kufikisha ujumbe kwa Tanzania PANORAMA Blog.

Ujumbe aliuotuma ulisomeka; ‘Bwana Dewji amezungumza na sisi na ametuhakikishia uwajibikaji wa menejimenti katika kulinda maslahi ya wafanyakazi. Tumekubaliana kuwa na mazungumzo ya kina, tungependa kutatua jambo hili kwa njia ya mazungumzo.’

Ujumbe mwingine chini ya huo aliuotuma ulisomeka; ‘leo hii mmelalamika mazingira ya watu wenu ila tusema ukweli pia mnawanyanyasa sana watanzania sema tu wanashindwa nani wa kuwasemea pia kutokana na hali za maisha yao ila mazingira ya ufanyaji kazi siyo.

Jitahidi za Tanzania PANORAMA Blog kuzungumza na Ubalozi wa India kuhusu suala hili zinaendelea.    

BOSI AIRTEL ALIVYOKWAPUA MAMILIONI BILA KUBAINIKA

 



NA MWANDISHI WETU

IMEBAINIKA kuwa, mmoja wa waliokuwa maofisa wa juu wa kampuni ya simu za mkononi ya Airtel, alichota mamilioni ya shilingi za kampuni hiyo kwa kufanya nayo biashara hewa.

Ili kufanikisha uchotaji wa mamilioni hayo, kigogo huyo ambaye jina lake tunalifadhi kwa sasa, alifungua kampuni iliyokuwa ikitoa huduma kwenye minara ya simu ya Aitel na kuweka mtu wa kuisimamia ili kuficha uhusika wake.

Uchunguzi wa awali kuhusu ufisadi wa mali za umma uliofanywa na Tanzania PANORAMA Blog kwa Kampuni ya Aitel umeonyesha kuwa, Airtel baada ya kubadilishwa jina kutoka Zain, kigogo huyo aliyekuwa amekwishachota pesa nyingi kwa kufanya biashara za udanganyifu, alifungua kampuni ambayo haraka haraka ilianza kupewa zabuni za Airtel.

Kwa mujibu wa uchunguzi, kampuni iliyofunguliwa ( jina tunalo) iliwekwa chini ya usimamizi wa mtu mwingine ambaye alikuwa akiripoti moja kwa moja kwa kigogo huyo na yeye alikuwa akifika kukagua mwenendo wake siku za mwisho wa wiki ambazo wafanyakazi hawakuwa kazini.

Uchunguzi umeonyesha kuwa kigogo huyo alitumia nafasi yake katika Airtel kutazama mianya ya kuiwezesha kampuni yake kupata zabuni hewa zenye thamani ya mamilioni ya fedha, jambo ambalo lingefanikiwa kampuni hiyo ingefungwa au kubadilishwa jina na iwapo ingetiliwa shaka na kuanza kufuatiliwa na mamlaka serikali, kigogo huyo angeacha kazi na kukimbilia nje ya nchi; na hiyo ingetegemea na hali halisi ya wakati ambao ingegundulika.

Tanzania PANORAMA Blog katika uchunguzi wake imebaini kuwa kigogo huyo baada ya kufanikiwa kuchomeka jina la kampuni yake kwenye menejimenti ya Airtel kama moja ya kampuni zenye sifa ya kufanya biashari kubwa, kwa kutumia wadhfa wake alianza kushawishi zabuni zenye thamani kubwa ipewe kampuni yake.

Uchunguzi umebaini kuwa haraka haraka bosi huyo aliwasilisha kwa menejimenti pendekezo la kununuliwa kwa jenereta mbili kubwa kutoka nje ya nchi kwa ajili ya kuendesha minara ya Airtel.

Pendekezo hilo liliainisha bei ya jenereta hizo kuwa; moja gharama yake ni Dola za Marekani 240,000 na ya pili Dola za Marekani 480,000 ambazo zingekaa makao makuu tayari kufanya kazi wakati wa dharura.

Mchakato wa ununuzi wa jenereta hizo ulifanyika haraka na malipo yalifanyika kwa mikupuo mitatu. Mkupuo wa kwanza ulihusisha malipo ya Dola za Marekani 480,000 ambazo zililipwa kwa invoice mbili na Dola za Marekani 240,000 invoice moja.

Hata hivyo Tanzania PANORAMA Blog inaripoti kwa uhakika kuwa manunuzi ya jenereta hizo hayakufanyika bali pesa hizo ziliwekwa kibindoni na bosi huyo.

Taarifa zinaeleza kuwa wakati akiandaa mpango mwingine wa kuchota zaidi ya Dola za Marekani 500,000 Serikali ya Awamu Tano ilianza kufuatilia mwenendo wa kampuni hiyo ili kuinusuru isife kutokana na hali mbaya iliyokuwa nayo.

"Baada ya Serikali ya Awamu ya Tano kuanza kufuatilia mwenendo wa kampuni kwa karibu, bosi alijua sasa atakuwa hatarini akaamua kuacha kazi mara moja kabla hajafanikisha mipango yake mingine.

"Wakaguzi wa serikali walipokuja waligundua kuwa manunuzi ya hizo jenereta yalikuwa hewa kwani hakukuwa na hizo jenereta bali hela za Airtel zilikwapuliwa zikawekwa mfukoni lakini hawakuweza kumnasa bosi kwa sababu alikuwa ameishaacha kazi.

"Na ilikuwa ngumu kumnasa kwa sababu yeye alikuwa nyuma ya ile kampuni ambayo aliweka mtu wake, huyo ndiyo akawa bosi. Huyo ndiyo alipata msukosuko kidogo lakini sasa yupo huru.

"Kwa sababu serikali ilishindwa kumbaini hakukimbilia nje ya nchi bali alikwenda nje kidogo ya jiji akajenga shule yake kubwa huko akaanzisha na biashara zake nyingine. Mke wake ambaye alikuwa mtumishi wa NSSF aliyeaacha kazi ili kusaidiana na yule bwana aliyemuweka kuendesha hiyo kampuni ya wizi sasa ndiyo anatokeza zaidi kwenye biashara zake, " kilieleza chanzo cha ndani cha taarifa.

Tanzania PANORAMA Blog itaripoti ufisadi huu kwa kina mara baada ya kukamilisha uchunguzi wake.