banner

Thursday, December 10, 2020

MeTL YAZUNGUMZIA TUHUMA ZINAZOIANDAMA

 

Mwenyekiti wa Makampuni ya MeTL, Gulam dewji

NA MWANDISHI WETU

UONGOZI wa Kampuni zilizo chini ya mwamvuli wa Mohamedi Enterprises Tanzania Limited (MeTL) umesema utatafuta njia ya kumaliza mgogoro baina yake na wafanyakazi ambao ni raia wa India katika meza ya mazungumzo.

Hayo yameelezwa na mmoja wa maafisa wa kampuni hiyo aliyetumwa na Mkurugenzi wa MeTL, Gulam Dewji kutoa ufafanuzi kwa Tanzania PANORAMA Blog kuhusu andishi lililowekwa kwenye mitandao ya kijamii likiwatahadhalisha raia wa India wote kuepuka kufanya kazi katika kampuni za MeTL.

Andiko hilo mtandaoni linaeleza kuwa Ubalozi wa India umekuwa ukipokea kwa mfululizo malalamiko ya wafanyaakazi wa Kampuni za MeTL kunyanyaswa na uongozi pamoja na mwajiri wao kuwafungulia kesi za kughushi mahakamani kiasi cha kusababisha wanafamilia wa wafanyakazi hao kulazimika kurejea India.

Kwamba Mwenyekiti wa Makampuni ya MeTl, Gulam Dewji na maafisa waandamizi wamekuwa wakiwafanya vitendo vya unyanyasaji na udhalilishaji wafanyakazi hao wanapofikisha malalamiko kwao.

Linahitishwa kwamba raia wote wa India wasikubali kuajiriwa na Kampuni za MeTL kutokana na mwenendo usiofaa wa viongozi wake wa juu.

Gulam

Alipoulizwa Mwenyekiti Gulam, kuhusu suala hilo kupitia simu yake ya kiganjani alisema aandikiwe maswali kwa maandishi ili ayajibu na alipoandikiwa, muda mfupi baadaye mtu mmoja mwenye asili ya kiasia alituma ujumbe kwa njia ya whatsapp akieleza kuwa ametumwa na Gulam kufikisha ujumbe kwa Tanzania PANORAMA Blog.

Ujumbe aliuotuma ulisomeka; ‘Bwana Dewji amezungumza na sisi na ametuhakikishia uwajibikaji wa menejimenti katika kulinda maslahi ya wafanyakazi. Tumekubaliana kuwa na mazungumzo ya kina, tungependa kutatua jambo hili kwa njia ya mazungumzo.’

Ujumbe mwingine chini ya huo aliuotuma ulisomeka; ‘leo hii mmelalamika mazingira ya watu wenu ila tusema ukweli pia mnawanyanyasa sana watanzania sema tu wanashindwa nani wa kuwasemea pia kutokana na hali za maisha yao ila mazingira ya ufanyaji kazi siyo.

Jitahidi za Tanzania PANORAMA Blog kuzungumza na Ubalozi wa India kuhusu suala hili zinaendelea.    

BOSI AIRTEL ALIVYOKWAPUA MAMILIONI BILA KUBAINIKA

 



NA MWANDISHI WETU

IMEBAINIKA kuwa, mmoja wa waliokuwa maofisa wa juu wa kampuni ya simu za mkononi ya Airtel, alichota mamilioni ya shilingi za kampuni hiyo kwa kufanya nayo biashara hewa.

Ili kufanikisha uchotaji wa mamilioni hayo, kigogo huyo ambaye jina lake tunalifadhi kwa sasa, alifungua kampuni iliyokuwa ikitoa huduma kwenye minara ya simu ya Aitel na kuweka mtu wa kuisimamia ili kuficha uhusika wake.

Uchunguzi wa awali kuhusu ufisadi wa mali za umma uliofanywa na Tanzania PANORAMA Blog kwa Kampuni ya Aitel umeonyesha kuwa, Airtel baada ya kubadilishwa jina kutoka Zain, kigogo huyo aliyekuwa amekwishachota pesa nyingi kwa kufanya biashara za udanganyifu, alifungua kampuni ambayo haraka haraka ilianza kupewa zabuni za Airtel.

Kwa mujibu wa uchunguzi, kampuni iliyofunguliwa ( jina tunalo) iliwekwa chini ya usimamizi wa mtu mwingine ambaye alikuwa akiripoti moja kwa moja kwa kigogo huyo na yeye alikuwa akifika kukagua mwenendo wake siku za mwisho wa wiki ambazo wafanyakazi hawakuwa kazini.

Uchunguzi umeonyesha kuwa kigogo huyo alitumia nafasi yake katika Airtel kutazama mianya ya kuiwezesha kampuni yake kupata zabuni hewa zenye thamani ya mamilioni ya fedha, jambo ambalo lingefanikiwa kampuni hiyo ingefungwa au kubadilishwa jina na iwapo ingetiliwa shaka na kuanza kufuatiliwa na mamlaka serikali, kigogo huyo angeacha kazi na kukimbilia nje ya nchi; na hiyo ingetegemea na hali halisi ya wakati ambao ingegundulika.

Tanzania PANORAMA Blog katika uchunguzi wake imebaini kuwa kigogo huyo baada ya kufanikiwa kuchomeka jina la kampuni yake kwenye menejimenti ya Airtel kama moja ya kampuni zenye sifa ya kufanya biashari kubwa, kwa kutumia wadhfa wake alianza kushawishi zabuni zenye thamani kubwa ipewe kampuni yake.

Uchunguzi umebaini kuwa haraka haraka bosi huyo aliwasilisha kwa menejimenti pendekezo la kununuliwa kwa jenereta mbili kubwa kutoka nje ya nchi kwa ajili ya kuendesha minara ya Airtel.

Pendekezo hilo liliainisha bei ya jenereta hizo kuwa; moja gharama yake ni Dola za Marekani 240,000 na ya pili Dola za Marekani 480,000 ambazo zingekaa makao makuu tayari kufanya kazi wakati wa dharura.

Mchakato wa ununuzi wa jenereta hizo ulifanyika haraka na malipo yalifanyika kwa mikupuo mitatu. Mkupuo wa kwanza ulihusisha malipo ya Dola za Marekani 480,000 ambazo zililipwa kwa invoice mbili na Dola za Marekani 240,000 invoice moja.

Hata hivyo Tanzania PANORAMA Blog inaripoti kwa uhakika kuwa manunuzi ya jenereta hizo hayakufanyika bali pesa hizo ziliwekwa kibindoni na bosi huyo.

Taarifa zinaeleza kuwa wakati akiandaa mpango mwingine wa kuchota zaidi ya Dola za Marekani 500,000 Serikali ya Awamu Tano ilianza kufuatilia mwenendo wa kampuni hiyo ili kuinusuru isife kutokana na hali mbaya iliyokuwa nayo.

"Baada ya Serikali ya Awamu ya Tano kuanza kufuatilia mwenendo wa kampuni kwa karibu, bosi alijua sasa atakuwa hatarini akaamua kuacha kazi mara moja kabla hajafanikisha mipango yake mingine.

"Wakaguzi wa serikali walipokuja waligundua kuwa manunuzi ya hizo jenereta yalikuwa hewa kwani hakukuwa na hizo jenereta bali hela za Airtel zilikwapuliwa zikawekwa mfukoni lakini hawakuweza kumnasa bosi kwa sababu alikuwa ameishaacha kazi.

"Na ilikuwa ngumu kumnasa kwa sababu yeye alikuwa nyuma ya ile kampuni ambayo aliweka mtu wake, huyo ndiyo akawa bosi. Huyo ndiyo alipata msukosuko kidogo lakini sasa yupo huru.

"Kwa sababu serikali ilishindwa kumbaini hakukimbilia nje ya nchi bali alikwenda nje kidogo ya jiji akajenga shule yake kubwa huko akaanzisha na biashara zake nyingine. Mke wake ambaye alikuwa mtumishi wa NSSF aliyeaacha kazi ili kusaidiana na yule bwana aliyemuweka kuendesha hiyo kampuni ya wizi sasa ndiyo anatokeza zaidi kwenye biashara zake, " kilieleza chanzo cha ndani cha taarifa.

Tanzania PANORAMA Blog itaripoti ufisadi huu kwa kina mara baada ya kukamilisha uchunguzi wake.

 

Wednesday, December 9, 2020

POLISI WAACHIWA MZIGO WA KUMTAFUTA MWANAFUNZI ALIYEPOTEA ST MARY'S SEK

 

Katibu Mkuu Akwilapo

NA MWANDISHI WETU

KATIBU Mkuu wa Wazara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Leonard Akwilapo amesema wajibu wa kumtafuta  mwanafunzi wa Shule ya Sekondari ya Bweni ya St Mary's, Labna Said Salim aliyepotea akiwa chini ya uangalizi wa shule ni wa Jeshi la Polisi

Ameyasema hayo jana katika mahojiano yake na Tanzania PANORAMA Blog ambayo ilimuuliza mchango wa wizara kumtafuta mwanafunzi huyo aliyepotea Oktoba 4, 2020.

"Hilo jambo wenye wajibu ni polisi na ndiyo maana sisi halijafika kwetu na hata kama lingekuwa limefika tungelipeleka polisi kwa sababu wao ndiyo wenye wajibu wa mambo kama hayo," alisema Akwilapo.

Labna


Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Kipolisi Kinondoni, Ramandani Kingai alipoulizwa jana kuhusu hatua waliyofikia katika msako huo alisema mpasa sasa hawafikiwa kumpata mwanafunzi huyo

Alipoulizwa kuhusu vijana saba waliokamatwa wakivuta bangi nyumbani kwa Kamishna Mstaafu wa Jeshi Magereza ambaye jina lake limehifadhiwa, Kamanda Kingai alisema vijana hao ambao ni wanafunzi bado wanafanya mitihani ya kumaliza kidato cha nne hivyo wanasubiriwa mpaka watakapomaliza ndipo hatua za kisheria zitachukuliwa dhidi yao.

Taarifa ya uchunguzi wa awali wa kupotea kwa mwanafunzi huyo iliyotolewa na Afisa Elimu Sekondari wa Wilaya ya Kinondoni, Joseph Kapere ambaye ni mjumbe wa timu iliyoundwa na Serikali ya Wilaya ya Kinondoni kuchunguza kupotea kwa mtoto huyo, mahali alipo sasa na mazingira ya kutoweka kwake ilieleza kuwa timu hiyo ilithibitisha pasipo shaka kuwa Shule ya Sekondari ya St Mary’s Mbezi Makonde imepungukiwa sifa zinazostahili kutoa elimu kwa mwanafunzi.

Wajumbe wengine katika timu hiyo ni Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Kipolisi Kinondoni, Ufisa Usalama na Mdhibiti wa Ubora wa Elimu Kanda.

Kapere alisema tayari Mkuu wa Shule ya St. Mary's, Recca Ntipoo amehojiwa na kuungama kutenda makosa katika baadhi ya mambo kwenye sakata hilo na kwamba aliipeleka timu hiyo mahali alikodai Labna alikwenda kuishi na mpenzi wake baada ya kutoroka shule.

Alisema timu ilibaini shule hiyo ilifanya makosa kutotoa taarifa polisi kuhusu kutoweka kwa mtoto na pia kukaa kimya  siku nne bila kutoa taarifa kwa wazazi kuhusu kutoweka kwake wala kuwajulisha kuwa amewaeleza walimu hataki shule.

Katika maelezo yake Kapere alisema, Ntipoo aliungama kufahamu vitendo vya mwanafunzi kutoka shule kwa kuruka ukuta usiku na kwenda maeneo hatarishi kwao jambo ambalo Mwalimu huyo aliliona kuwa  la kawaida kwa sababu alikuta likifanyika shuleni hapo.

Aidha, Kapere alisema timu ilibaini shule hiyo kuwa na mazingira machafu, kukosa ulinzi wa kutosha na kutokuwa na ukuta imara.

Alisema mambo mengine yaliyogundulika katika uchunguzi wa timu hiyo ni kubainika kwa nyumba ya Kamishna Mstaafu wa Jeshi la Magereza ambayo ina shamba la bangi  ambamo walikutwa wavulana saba, wanafunzi wa Shule ya Sekondari ya St Mary's waliokuwa wakivuta pamoja.

 Mwanafunzi msichana Labna wa Shule ya Sekondari ya Bweni ya St. Mary’s iliyoko Mbezi Makonde alitoweka shuleni tangu Oktoba 4, 2020 na kutokomea kusikojulikana na hadi sasa hajapatikana.

Labna alitoweka akiwa chini ya uangalizi wa shule lakini taarifa za kutoweka kwake zilitolewa Oktoba 8, 2020 na matron wake Sarah Murra aliyempigia simu mama mzazi wa Labna akiulizia kama ameishafika nyumbani.

Katika hatua ya kushangaza, uongozi wa Shule ya Sekondari ya St Mary’s haukutoa taarifa polisi kuhusu kutoweka kwa mwanafunzi huyo na badala yake wazazi ndiyo walioripoti tukio la mtoto wao kupotea akiwa shuleni.

MKANDARASI SOKO LA TANDALE MWIZI MDOGO MDOGO - MKURUGENZI KINONDONI

 

Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kinondoni, Aron Kigurumjuli


NA MWANDISHI WETU

MKURUGENZI wa Halmashauri ya Wilaya ya Kinondoni, Aron Kigurumjuli amesema mkandarasi aliyepewa kandarasi ya kujenga soko jipya la Tandale, Namis Corporation LTD ni mwizi mdogo mdogo ambaye akikamatwa hurejesha alichoiba.

Kigurumjuli aliyasema hayo wiki iliyopita katika mahojiano maalumu na Tanzania PANORAMA Blog yaliyofanyikia Kinondoni Dar es Salaam.

Alikuwa akijibu kuhusu madai kuwa, mkandarasi huyo alighushi leseni yake ya biashara na alibainika kutenda kosa hilo wakati akisaka zabuni ya ujenzi wa soko la Tandale.

Katika majibu yake, Kigurumjuli alisema Namis Corporation LTD haikughushi leseni ya biashara isipokuwa ilifanya udanganyifu ulioiwezesha kuwa inalipa pesa kidogo kinyume na hitaji la leseni yake na hivyo ikawa inaiibia serikali pesa kidogo za tozo ya leseni.

Kigurumjuli alisema, wataalamu wake walibaini kuwepo kwa dosari hiyo kwenye leseni ya Namis Corporation LTD wakati wa ukaguzi wa nyaraka uliofanyika kabla ya kuzawadiwa zabuni ya ujenzi wa soko la Tandale.

"Unasema inadaiwa si ndiyo? sasa mimi nakwambia madai hayo ni uongo. Namis hajaghushi leseni ya biashara, sema, acha nikusaidie yule alikuwa akiiba kidogo hela za serikali. Ni mwizi mdogo mdogo tu lakini tulimbaini tukambana, akakiri tukampiga faini, akalipa.

"Alikuwa anaibaje, sikiliza. Leseni za biashara zipo za aina nyingi sana, zipo za mpaka Dola za Marekani 200,000. Huyu leseni yake alipaswa alipie kiwango cha juu lakini yeye akakataka ya kiwango cha chini, akawa analipa below ya kiwango anachopaswa kulipa. Kama sikosei kwa shughuli zake za ukandarasi alipaswa kulipa 60,000 lakini yeye akawa analipa 30,000.

" Sasa wakati wa ukaguzi wa nyaraka zake alipokuwa ameomba tenda ya soko la Tandale wataalamu wangu wakagundua huyu anatuibia, anaiibia serikali. Wakambana, alibishabisha kidogo lakini alibanwa haswa akakubali kulipa.

"Tulimpiga faini kubwa. Shilingi milioni nane ya miaka mitano aliyokuwa amefanya ujanja wake. Sasa huyu huwezi kumpa kosa kubwa hilo la kughushi, huyu ni mwizi mdogo mdogo tu na alibanwa akalipa. Hayo mengine sasa kamuilize mwenyewe," alisema Kigurumjuli.

Tanzania PANORAMA Blog imemtafuta Mkurugenzi wa Namis Corporation LTD, Thomas Uiso kuzungumzia suala hilo bila mafanikio kwani tongu aliposema mambo yote yanayohusiana na kukwama kwa ujenzi wa soko jipya la Tandale ambalo yeye ndiye mkandarasi aulizwe Mkurugenzi Kigurumjuli amekuwa hapokei simu wala kujibu ujumbe wa maandishi.

Tanzania PANORAMA jana lilimpigia simu Uiso hakupokea na lilimtumia ujumbe wa maandishi kumuuliza kuhusu jambo hilo hakuujibu licha kuonyesha umemfikia na ameusoma.

Taarifa zilizolifikia Tanzania PANORAMA Blog zilieleza kuwa kampuni hiyo ulighushi leseni ya biashara na ilipata kandarasi mbalimbali kwa kutumia leseni hiyo ya kughushi.

Tuesday, December 8, 2020

TANROADS NA KISA CHA NDOTO ZA KAKAKUONA KWA WATANZANIA

 

Mtendaji Mkuu wa TANROADS, Partick Mfugale

MAISHA ya wananchi wa Tanzania kwa kiasi kikubwa sasa yamebadilika. Miundombinu ya barabara na madaraja ya kisasa ambayo hapo awali Watanzania waliyaona kwenye picha na sinema zilizoandaliwa katika nchi za Ulaya na Amerika, sasa ipo nchini na kwa kiwango kikubwa imekuwa msaada kwa safari zao wenyewe na pia kusafirisha mazao na bidhaa za biashara.

Mabadiliko hayo ya maisha ya wanachi wa Tanzania yameenda sambamba na mabadiliko ya mwenendo wa uchumi wa Taifa. Uchumi wa Tanzania sasa unakuwa kwa kasi kubwa na tayari umekwishachumpa kutoka kwenye uchumi wa nchi masikini hadi uchumi wa kati, miaka mitano kabla ya matarajio.

Wataalamu wa uchumi wanaeleza kuwa kuchumpa kwa uchumi wa Tanzania kutoka ule wa nchi masikini hadi uchumi wa kati miaka mitano kabla ya matarajio kumewezeshwa pamoja na mambo mengine, ujenzi wa miondombinu imara na yenye kuvutia jambo linaloifanya nchi, kwanza kufikika sehemu zote lakini pia kuwa na mandhari ya kuvutia.

Haikuwa kazi rahisi kuyafikia mafanikio haya katika sekta ya ujenzi wa miundombinu. Wapo Watanzania waliotokwa jasho la damu na chumvi kuyawezesha na kinara wa utiririkaji jasho la kuigeza Tanzania kuwa mithili ya paradiso ni Rais John Pombe Magufuli ambaye kwa miaka mitano ya awamu ya kwanza ya utawala wake, ratiba yake ya kulala imebadilika, analala kwa saa chache na muda mwingi yupo kibaruani akichuruzikwa jasho.

Rais John Pombe Magufuli


Wa pili katika hili, ni Wakala wa Barabara, (Tanroads) ambao mabadiliko ya kiutendaji katika taasisi za serikali yaliyoasisiwa na Rais Dk. Magufuli mara tu alipoingia marakani mwaka 2015  yaliwafanya wawe kama wanajimu kwa kutafasili ndoto za mnyama mdogo anayejulikana kwa jina la Kakakuona.

Kakakuona hutembea akiota kuwa akikutana na binadamu na kufanikiwa kukimbia kwa kasi ili binadamu asimkamate kisha akajificha asionekane basi atakuwa na uwezo wa kibinadamu wa kufanya maendeleo makubwa katika maisha yake.

Binadamu nao, (baadhi ya jamii) huota kwamba wakimuona mnyama mdogo Kakakuona, basi kuna baraka mbele yao kwa sababu mnyama huyo haonekana hovyo hovyo. Na hivyo ndivyo ilivyokuwa kwa Tanroads ambayo ndoto za Kakakuona kutaka kukimbia kwa kasi kisha ajifiche ili awe kama binadamu na maendeleo yake imezifanya ziwe za kweli na kwa Watanzania waliokuwa wakiota siku wakikutana na Kakakuona basi kuna baraka inayokuja mbele yao, Tanroads imezigeuza ndoto zao kuwa kweli. 

Ukweli huu umo katika kazi za kutukuka zilizofanywa na Tanroads kwenye ujenzi wa madaraja ambayo sasa yamegeuka kuwa vivutio vya utalii kwa watanzania wenyewe na hata baadhi ya wageni kutoka mataifa ya nje kutokana na muonekane wake wa kuvutia. Mbali na hilo, ndoto za watanzania katika baadhi ya maeneo ambako kulikuwa na matatizo makubwa ya kufika na hata uhai wa watu kupotea kwa sababu ya kukosa madaraja, hali hiyo sasa haipo, madaraja yamejengwa na hapa chini ni orodha fupi ya madaraja hayo.

DARAJA LA MAGUFULI

 Kwa mujibu wa Meneja wa Wakala wa Barabara (TANROADS) wa Mkoa wa Morogoro, Mhandisi Dorothy Ntenga, Daraja la Magufuli lililojengwa katika Mto Kilombero liligharimu zaidi ya shilingi bilioni 50 ambazo zote zilitolewa na Serikali.



Kwamba ujenzi wa daraja hilo umezingatia viwango vilivyowekwa kwenye mkataba na mkandarasi ambaye ni kampuni ya M/S China Railway 15 Group Corporation.

 Daraja hilo linarahisisha shughuli za usafirishaji wa mazao, ufugaji na madini katika Wilaya za Ulanga, Malinyi na Kilombero.



Ilikuwa ndoto ya muda mrefu kwa wananchi hao kupata daraja na wakati likijengwa, mmoja wa wakazi wa maeneo hayo, Zainabu Mtalanga alipata kumwambia aliyekuwa Waziri wa Ujenzi, Profesa Makame Mbarawa kuwa;  “Tunaishukuru serikali kwa ujenzi wa daraja hili kwani limekuwa mkombozi kwetu wananchi wa Wilaya za Ulanga na Kilombero.



“Hapo nyuma vifo vingi vimetokea pasipo kutegemewa wakati tukitumia kivuko kufuata huduma za kijamii wilaya jirani ambapo kuna huduma zote za muhimu.”

DARAJA LA MAGARA

Taarifa ya Meneja wa Tanroads Mkoa wa Manyara, Mhandisi Bashiri Rwesingisa, kuhusu ujenzi wa Daraja la Magara inaeleza kuwa ujenzi wake uligharimu zaidi ya shilingi bilioni 12



Lilijengwa na Mkandarasi M/s China Railway Seventh Group likiwa na urefu wa mita 84 na barabara za maingilio KM 4 na linaunganisha Hifadhi ya Taifa ya Manyara na Tarangire kupitia Mayoka, pamoja na kuunganisha mashamba makubwa ya mpunga na miwa yaliyopo ng’ambo ya pili ya Mto na Masoko ya Babati na Arusha.



Daraja la Magara ni kichocheo cha ukuaji wa utalii na uchumi  katika Mkoa wa Manyara na Taifa kwa ujumla likiwa umbali wa KM 21 kutoka Mbuyu wa Mjerumani katika barabara kuu ya Babati – Arusha na sasa linawezesha kuvuka Mto Magara katika barabara ya Mkoa ya Mbuyu wa Mjerumani – Mbulu yenye urefu wa KM 49.

DARAJA LA MOMBA

Meneja wa Tanroads wa Mkoa wa Rukwa, Mhandisi Ndelalutse Karoza analieleza daraja hilo kuwa ni kiunganishi cha mkoa huo na Mkoa wa Songwe kwa upande wa Bonde la Ziwa Rukwa na limejengwa kwa fedha za walipa kodi wa Tanzania kwa 100.



Kwa mujibu wa Karoza, gharama za ujenzi wa Daraja la Momba  ni shilingi bilioni 17.7 na limejengwa na Kampuni ya ukandarasi ya Genjio Engineering Group Cooperation ya China

Karoza anasema ujenzi wa daraja hilo ni muhimu sana kwa mikoa ya Rukwa na Songwe pamoja na Tanzania kwa ujumla na kubainisha kuwa ukamilifu wa daraja hilo utawainua wananchi kiuchumi na kijamii ikiwemo kupunguza gharama za usafirishaji wa mazao.

Daraja la Mto Sibiti lipo Iramba mkoani Sindiga. Lina urefu wa mita 83 na gharama za ujenzi wake ni shilingi bilioni 19.2

 DARAJA LA NYERERE (KIGAMBONI)

Lipo Kurasini jijini Dar es Salaam na linamilikiwa kwa ubia kati ya Serikali ya Tanzania na NSSF.



Ni daraja la aina ya kuning’inia lililojengwa na Mkandarasi China Railway Jiangchang Engineering (T) Ltd na China Major Bridge Engineering Company. Lina urefi wa mita 680 na upana wa mita 27.5 na gharama yake ya ujenzi ni Dola za Marekani milioni 136

Daraja la Nyerere ndilo linalovuka mkondo wa kurasini jijini Dar es Salaam likiwa na njia sita za kupitisha magari. Daraja la Nyerere ndilo kubwa kuliko yote Afrika Mashariki na linavutia sana kutokana na kujengwa kwa ustadi.