banner

Wednesday, December 9, 2020

POLISI WAACHIWA MZIGO WA KUMTAFUTA MWANAFUNZI ALIYEPOTEA ST MARY'S SEK

 

Katibu Mkuu Akwilapo

NA MWANDISHI WETU

KATIBU Mkuu wa Wazara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Leonard Akwilapo amesema wajibu wa kumtafuta  mwanafunzi wa Shule ya Sekondari ya Bweni ya St Mary's, Labna Said Salim aliyepotea akiwa chini ya uangalizi wa shule ni wa Jeshi la Polisi

Ameyasema hayo jana katika mahojiano yake na Tanzania PANORAMA Blog ambayo ilimuuliza mchango wa wizara kumtafuta mwanafunzi huyo aliyepotea Oktoba 4, 2020.

"Hilo jambo wenye wajibu ni polisi na ndiyo maana sisi halijafika kwetu na hata kama lingekuwa limefika tungelipeleka polisi kwa sababu wao ndiyo wenye wajibu wa mambo kama hayo," alisema Akwilapo.

Labna


Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Kipolisi Kinondoni, Ramandani Kingai alipoulizwa jana kuhusu hatua waliyofikia katika msako huo alisema mpasa sasa hawafikiwa kumpata mwanafunzi huyo

Alipoulizwa kuhusu vijana saba waliokamatwa wakivuta bangi nyumbani kwa Kamishna Mstaafu wa Jeshi Magereza ambaye jina lake limehifadhiwa, Kamanda Kingai alisema vijana hao ambao ni wanafunzi bado wanafanya mitihani ya kumaliza kidato cha nne hivyo wanasubiriwa mpaka watakapomaliza ndipo hatua za kisheria zitachukuliwa dhidi yao.

Taarifa ya uchunguzi wa awali wa kupotea kwa mwanafunzi huyo iliyotolewa na Afisa Elimu Sekondari wa Wilaya ya Kinondoni, Joseph Kapere ambaye ni mjumbe wa timu iliyoundwa na Serikali ya Wilaya ya Kinondoni kuchunguza kupotea kwa mtoto huyo, mahali alipo sasa na mazingira ya kutoweka kwake ilieleza kuwa timu hiyo ilithibitisha pasipo shaka kuwa Shule ya Sekondari ya St Mary’s Mbezi Makonde imepungukiwa sifa zinazostahili kutoa elimu kwa mwanafunzi.

Wajumbe wengine katika timu hiyo ni Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Kipolisi Kinondoni, Ufisa Usalama na Mdhibiti wa Ubora wa Elimu Kanda.

Kapere alisema tayari Mkuu wa Shule ya St. Mary's, Recca Ntipoo amehojiwa na kuungama kutenda makosa katika baadhi ya mambo kwenye sakata hilo na kwamba aliipeleka timu hiyo mahali alikodai Labna alikwenda kuishi na mpenzi wake baada ya kutoroka shule.

Alisema timu ilibaini shule hiyo ilifanya makosa kutotoa taarifa polisi kuhusu kutoweka kwa mtoto na pia kukaa kimya  siku nne bila kutoa taarifa kwa wazazi kuhusu kutoweka kwake wala kuwajulisha kuwa amewaeleza walimu hataki shule.

Katika maelezo yake Kapere alisema, Ntipoo aliungama kufahamu vitendo vya mwanafunzi kutoka shule kwa kuruka ukuta usiku na kwenda maeneo hatarishi kwao jambo ambalo Mwalimu huyo aliliona kuwa  la kawaida kwa sababu alikuta likifanyika shuleni hapo.

Aidha, Kapere alisema timu ilibaini shule hiyo kuwa na mazingira machafu, kukosa ulinzi wa kutosha na kutokuwa na ukuta imara.

Alisema mambo mengine yaliyogundulika katika uchunguzi wa timu hiyo ni kubainika kwa nyumba ya Kamishna Mstaafu wa Jeshi la Magereza ambayo ina shamba la bangi  ambamo walikutwa wavulana saba, wanafunzi wa Shule ya Sekondari ya St Mary's waliokuwa wakivuta pamoja.

 Mwanafunzi msichana Labna wa Shule ya Sekondari ya Bweni ya St. Mary’s iliyoko Mbezi Makonde alitoweka shuleni tangu Oktoba 4, 2020 na kutokomea kusikojulikana na hadi sasa hajapatikana.

Labna alitoweka akiwa chini ya uangalizi wa shule lakini taarifa za kutoweka kwake zilitolewa Oktoba 8, 2020 na matron wake Sarah Murra aliyempigia simu mama mzazi wa Labna akiulizia kama ameishafika nyumbani.

Katika hatua ya kushangaza, uongozi wa Shule ya Sekondari ya St Mary’s haukutoa taarifa polisi kuhusu kutoweka kwa mwanafunzi huyo na badala yake wazazi ndiyo walioripoti tukio la mtoto wao kupotea akiwa shuleni.

MKANDARASI SOKO LA TANDALE MWIZI MDOGO MDOGO - MKURUGENZI KINONDONI

 

Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kinondoni, Aron Kigurumjuli


NA MWANDISHI WETU

MKURUGENZI wa Halmashauri ya Wilaya ya Kinondoni, Aron Kigurumjuli amesema mkandarasi aliyepewa kandarasi ya kujenga soko jipya la Tandale, Namis Corporation LTD ni mwizi mdogo mdogo ambaye akikamatwa hurejesha alichoiba.

Kigurumjuli aliyasema hayo wiki iliyopita katika mahojiano maalumu na Tanzania PANORAMA Blog yaliyofanyikia Kinondoni Dar es Salaam.

Alikuwa akijibu kuhusu madai kuwa, mkandarasi huyo alighushi leseni yake ya biashara na alibainika kutenda kosa hilo wakati akisaka zabuni ya ujenzi wa soko la Tandale.

Katika majibu yake, Kigurumjuli alisema Namis Corporation LTD haikughushi leseni ya biashara isipokuwa ilifanya udanganyifu ulioiwezesha kuwa inalipa pesa kidogo kinyume na hitaji la leseni yake na hivyo ikawa inaiibia serikali pesa kidogo za tozo ya leseni.

Kigurumjuli alisema, wataalamu wake walibaini kuwepo kwa dosari hiyo kwenye leseni ya Namis Corporation LTD wakati wa ukaguzi wa nyaraka uliofanyika kabla ya kuzawadiwa zabuni ya ujenzi wa soko la Tandale.

"Unasema inadaiwa si ndiyo? sasa mimi nakwambia madai hayo ni uongo. Namis hajaghushi leseni ya biashara, sema, acha nikusaidie yule alikuwa akiiba kidogo hela za serikali. Ni mwizi mdogo mdogo tu lakini tulimbaini tukambana, akakiri tukampiga faini, akalipa.

"Alikuwa anaibaje, sikiliza. Leseni za biashara zipo za aina nyingi sana, zipo za mpaka Dola za Marekani 200,000. Huyu leseni yake alipaswa alipie kiwango cha juu lakini yeye akakataka ya kiwango cha chini, akawa analipa below ya kiwango anachopaswa kulipa. Kama sikosei kwa shughuli zake za ukandarasi alipaswa kulipa 60,000 lakini yeye akawa analipa 30,000.

" Sasa wakati wa ukaguzi wa nyaraka zake alipokuwa ameomba tenda ya soko la Tandale wataalamu wangu wakagundua huyu anatuibia, anaiibia serikali. Wakambana, alibishabisha kidogo lakini alibanwa haswa akakubali kulipa.

"Tulimpiga faini kubwa. Shilingi milioni nane ya miaka mitano aliyokuwa amefanya ujanja wake. Sasa huyu huwezi kumpa kosa kubwa hilo la kughushi, huyu ni mwizi mdogo mdogo tu na alibanwa akalipa. Hayo mengine sasa kamuilize mwenyewe," alisema Kigurumjuli.

Tanzania PANORAMA Blog imemtafuta Mkurugenzi wa Namis Corporation LTD, Thomas Uiso kuzungumzia suala hilo bila mafanikio kwani tongu aliposema mambo yote yanayohusiana na kukwama kwa ujenzi wa soko jipya la Tandale ambalo yeye ndiye mkandarasi aulizwe Mkurugenzi Kigurumjuli amekuwa hapokei simu wala kujibu ujumbe wa maandishi.

Tanzania PANORAMA jana lilimpigia simu Uiso hakupokea na lilimtumia ujumbe wa maandishi kumuuliza kuhusu jambo hilo hakuujibu licha kuonyesha umemfikia na ameusoma.

Taarifa zilizolifikia Tanzania PANORAMA Blog zilieleza kuwa kampuni hiyo ulighushi leseni ya biashara na ilipata kandarasi mbalimbali kwa kutumia leseni hiyo ya kughushi.

Tuesday, December 8, 2020

TANROADS NA KISA CHA NDOTO ZA KAKAKUONA KWA WATANZANIA

 

Mtendaji Mkuu wa TANROADS, Partick Mfugale

MAISHA ya wananchi wa Tanzania kwa kiasi kikubwa sasa yamebadilika. Miundombinu ya barabara na madaraja ya kisasa ambayo hapo awali Watanzania waliyaona kwenye picha na sinema zilizoandaliwa katika nchi za Ulaya na Amerika, sasa ipo nchini na kwa kiwango kikubwa imekuwa msaada kwa safari zao wenyewe na pia kusafirisha mazao na bidhaa za biashara.

Mabadiliko hayo ya maisha ya wanachi wa Tanzania yameenda sambamba na mabadiliko ya mwenendo wa uchumi wa Taifa. Uchumi wa Tanzania sasa unakuwa kwa kasi kubwa na tayari umekwishachumpa kutoka kwenye uchumi wa nchi masikini hadi uchumi wa kati, miaka mitano kabla ya matarajio.

Wataalamu wa uchumi wanaeleza kuwa kuchumpa kwa uchumi wa Tanzania kutoka ule wa nchi masikini hadi uchumi wa kati miaka mitano kabla ya matarajio kumewezeshwa pamoja na mambo mengine, ujenzi wa miondombinu imara na yenye kuvutia jambo linaloifanya nchi, kwanza kufikika sehemu zote lakini pia kuwa na mandhari ya kuvutia.

Haikuwa kazi rahisi kuyafikia mafanikio haya katika sekta ya ujenzi wa miundombinu. Wapo Watanzania waliotokwa jasho la damu na chumvi kuyawezesha na kinara wa utiririkaji jasho la kuigeza Tanzania kuwa mithili ya paradiso ni Rais John Pombe Magufuli ambaye kwa miaka mitano ya awamu ya kwanza ya utawala wake, ratiba yake ya kulala imebadilika, analala kwa saa chache na muda mwingi yupo kibaruani akichuruzikwa jasho.

Rais John Pombe Magufuli


Wa pili katika hili, ni Wakala wa Barabara, (Tanroads) ambao mabadiliko ya kiutendaji katika taasisi za serikali yaliyoasisiwa na Rais Dk. Magufuli mara tu alipoingia marakani mwaka 2015  yaliwafanya wawe kama wanajimu kwa kutafasili ndoto za mnyama mdogo anayejulikana kwa jina la Kakakuona.

Kakakuona hutembea akiota kuwa akikutana na binadamu na kufanikiwa kukimbia kwa kasi ili binadamu asimkamate kisha akajificha asionekane basi atakuwa na uwezo wa kibinadamu wa kufanya maendeleo makubwa katika maisha yake.

Binadamu nao, (baadhi ya jamii) huota kwamba wakimuona mnyama mdogo Kakakuona, basi kuna baraka mbele yao kwa sababu mnyama huyo haonekana hovyo hovyo. Na hivyo ndivyo ilivyokuwa kwa Tanroads ambayo ndoto za Kakakuona kutaka kukimbia kwa kasi kisha ajifiche ili awe kama binadamu na maendeleo yake imezifanya ziwe za kweli na kwa Watanzania waliokuwa wakiota siku wakikutana na Kakakuona basi kuna baraka inayokuja mbele yao, Tanroads imezigeuza ndoto zao kuwa kweli. 

Ukweli huu umo katika kazi za kutukuka zilizofanywa na Tanroads kwenye ujenzi wa madaraja ambayo sasa yamegeuka kuwa vivutio vya utalii kwa watanzania wenyewe na hata baadhi ya wageni kutoka mataifa ya nje kutokana na muonekane wake wa kuvutia. Mbali na hilo, ndoto za watanzania katika baadhi ya maeneo ambako kulikuwa na matatizo makubwa ya kufika na hata uhai wa watu kupotea kwa sababu ya kukosa madaraja, hali hiyo sasa haipo, madaraja yamejengwa na hapa chini ni orodha fupi ya madaraja hayo.

DARAJA LA MAGUFULI

 Kwa mujibu wa Meneja wa Wakala wa Barabara (TANROADS) wa Mkoa wa Morogoro, Mhandisi Dorothy Ntenga, Daraja la Magufuli lililojengwa katika Mto Kilombero liligharimu zaidi ya shilingi bilioni 50 ambazo zote zilitolewa na Serikali.



Kwamba ujenzi wa daraja hilo umezingatia viwango vilivyowekwa kwenye mkataba na mkandarasi ambaye ni kampuni ya M/S China Railway 15 Group Corporation.

 Daraja hilo linarahisisha shughuli za usafirishaji wa mazao, ufugaji na madini katika Wilaya za Ulanga, Malinyi na Kilombero.



Ilikuwa ndoto ya muda mrefu kwa wananchi hao kupata daraja na wakati likijengwa, mmoja wa wakazi wa maeneo hayo, Zainabu Mtalanga alipata kumwambia aliyekuwa Waziri wa Ujenzi, Profesa Makame Mbarawa kuwa;  “Tunaishukuru serikali kwa ujenzi wa daraja hili kwani limekuwa mkombozi kwetu wananchi wa Wilaya za Ulanga na Kilombero.



“Hapo nyuma vifo vingi vimetokea pasipo kutegemewa wakati tukitumia kivuko kufuata huduma za kijamii wilaya jirani ambapo kuna huduma zote za muhimu.”

DARAJA LA MAGARA

Taarifa ya Meneja wa Tanroads Mkoa wa Manyara, Mhandisi Bashiri Rwesingisa, kuhusu ujenzi wa Daraja la Magara inaeleza kuwa ujenzi wake uligharimu zaidi ya shilingi bilioni 12



Lilijengwa na Mkandarasi M/s China Railway Seventh Group likiwa na urefu wa mita 84 na barabara za maingilio KM 4 na linaunganisha Hifadhi ya Taifa ya Manyara na Tarangire kupitia Mayoka, pamoja na kuunganisha mashamba makubwa ya mpunga na miwa yaliyopo ng’ambo ya pili ya Mto na Masoko ya Babati na Arusha.



Daraja la Magara ni kichocheo cha ukuaji wa utalii na uchumi  katika Mkoa wa Manyara na Taifa kwa ujumla likiwa umbali wa KM 21 kutoka Mbuyu wa Mjerumani katika barabara kuu ya Babati – Arusha na sasa linawezesha kuvuka Mto Magara katika barabara ya Mkoa ya Mbuyu wa Mjerumani – Mbulu yenye urefu wa KM 49.

DARAJA LA MOMBA

Meneja wa Tanroads wa Mkoa wa Rukwa, Mhandisi Ndelalutse Karoza analieleza daraja hilo kuwa ni kiunganishi cha mkoa huo na Mkoa wa Songwe kwa upande wa Bonde la Ziwa Rukwa na limejengwa kwa fedha za walipa kodi wa Tanzania kwa 100.



Kwa mujibu wa Karoza, gharama za ujenzi wa Daraja la Momba  ni shilingi bilioni 17.7 na limejengwa na Kampuni ya ukandarasi ya Genjio Engineering Group Cooperation ya China

Karoza anasema ujenzi wa daraja hilo ni muhimu sana kwa mikoa ya Rukwa na Songwe pamoja na Tanzania kwa ujumla na kubainisha kuwa ukamilifu wa daraja hilo utawainua wananchi kiuchumi na kijamii ikiwemo kupunguza gharama za usafirishaji wa mazao.

Daraja la Mto Sibiti lipo Iramba mkoani Sindiga. Lina urefu wa mita 83 na gharama za ujenzi wake ni shilingi bilioni 19.2

 DARAJA LA NYERERE (KIGAMBONI)

Lipo Kurasini jijini Dar es Salaam na linamilikiwa kwa ubia kati ya Serikali ya Tanzania na NSSF.



Ni daraja la aina ya kuning’inia lililojengwa na Mkandarasi China Railway Jiangchang Engineering (T) Ltd na China Major Bridge Engineering Company. Lina urefi wa mita 680 na upana wa mita 27.5 na gharama yake ya ujenzi ni Dola za Marekani milioni 136

Daraja la Nyerere ndilo linalovuka mkondo wa kurasini jijini Dar es Salaam likiwa na njia sita za kupitisha magari. Daraja la Nyerere ndilo kubwa kuliko yote Afrika Mashariki na linavutia sana kutokana na kujengwa kwa ustadi.  

 

 

MKURUGENZI KINONDONI AANZA KUFANYA VITUKO

 

Mkurugenzi Manispaa ya Kinondoni, Aon Kigurumjuli

NA MWANDISHI WETU

MKURUGENZI wa Manispaa ya Wilaya ya Kinondoni, Aron Kigurumjuli, sasa ameanza kufanya vituko kwa kuwazuia waandishi wa habari kuingia na vitendea kazi vya aina yoyote ofisini kwake wanapokwenda kufanya naye mahojiano.

Kigurumjuli ameweka mlinzi katika mlango wa ofisi yake anayechagua watu wa kuingia na pia anachagua nani na yupi asiingie ambapo leo asubuhi, mlinzi huyo ameizuia Tanzania PANORAMA Blog kuonana na bosi wake kwa ajili ya kufanya mahojiano ikiwa na 'notebook' na kalamu mpaka itii sharti la kuingia mikono mitupu.

Katika hatua ya kushangaza, Kigurumjuli pia, wiki iliyopita alitoa maneno ya kashfa na kejeli kwa viongozi waandamizi wa serikali pamoja na aidha; leo hakupokea simu wala kujibu meseji kwa watu aliopanga miadi ya kukutana nao ofisini kwake.

Vituko hivi vya Kigurumjuli vimekuja siku chache baada ya yeye mwenyewe kuieleza Tanzania PANORAKA Blog kuwa amepata presha hivyo hawezi kwenda kazini baada ya kuripotiwa kwa taarifa za kukwama kwa ujenzi wa soko jipya la Tandale huku taarifa nyingine zikieleza kuwa ana hasira kwa sababu ya kuripotiwa kwa mkwamo wa ujenzi wa soko la Tandale na amejiapiza kuwashughulikia wanaofuatilia habari hiyo.

Katika tukio la leo asubuhi, Kigurumjuli alikuwa ametoa miadi ya kukutana ili azungumzie matatizo yaliyokwamisha ujenzi wa soko la Tandale. Miadi hiyo haikufanikiwa baada ya mlinzi aliyemuweka mlangoni kutaka aachiwe vitendea kazi vyote vya Tanzania PANORAMA Blog ikiwa ni pamoja na begi alilotaka apewe alishike.

"Toa vitu vyako vyote kwenye kibegi chako weka hapo kwenye kiti, hilo begi nipe hapa nilishike ukitoka utachukua vitu vyako nitakupa na begi lako," alieleza mlinzi ambaye jina lake halikufahamika.

Alipoelezwa kuwa ndani ya begi kuna kalamu, 'notebook' na nyaraka kadhaa na kufunguliwa akague na mwandishi alieleza yupo tayari kupekuliwa,  alisisitiza kuwa bosi wake ameagiza waandishi wasiingie na kitu chochote isipokuwa wao tu.

"Hii ni amri, kalamu na karatasi zako toa weka kwenye kiti, begi nipe hapa nitakushikia hatuna sababu ya kubishana," alisema kwa msisitizo.

Tanzania PANORAMA Blog haikumpatia begi mlinzi huyo kama alivyokuwa akisisitiza kwa sababu lilikuwa na taarifa za kuwepo kwa mipango miovu ya kupandikiziwa vitu visivyofaa kisha wangeitwa wana usalama kupekua begi hilo na kukuta vitu hivyo kabla ya kuwatia matatani kwa lengo la kuwazuia wasiripoti taarifa za soko la Tandale.

Unezi wa soko jipya la Tandale ulipokuwa umefikia mwezi Agosti


Kabla ya kuondoka eneo hilo, lilimpigia simu Mkurugenzi huyo kumjulisha hali halisi ilivyo hapo nje ya mlango wa ofisi yake, simu yake ilisikika ndani ikiita lakini hakuipokea na pia alitumiwa ujumbe mfupi wa maneno mara tatu ambao aliusoma lakini hakujibu.

Katika mahojiano ya wiki iliyopita kuhusu kukwama kwa ujenzi wa soko la Tandale na kuweka zuio kwa waandishi wa habari kiripoti habari za soko hilo bila ruhusa yake, Kigurumjuli alisema yeye binafsi ndiye aliyekwenda kutafuta fedha za ujenzi wa soko la Tandale, Wizara ya Fedha na Mipango na alipewa za kutosha ila tatizo lililopo sasa ni kukosekana kwa saruji.

Alipoulizwa sababu iliyomfanya yeye binafsi kwenda wizarani kushawishi kutolewa kwa fedha huku tayari aliyekuwa Waziri wa TAMISEMI, Selemani Jaffo akiwa amekwishatoa tamko kuhusu ujenzi wa masoko yaliyokuwa kwenye mpango wa kujengwa..... haraka alilikatisha swali hilo na kuanza kung'aka.

"Ni kinini hicho, Selemani Jafo ndiyo kitu gani hicho. Hapa unaongea na Mkurugenzi, upo ofisini kwa mkurugenzi usinitajie majina ya ajabu ajabu wewe. Huyo Jafo wakati nahangaika hazina alikuwepo?

 

Kigurumjuli

“Fedha nimetafuta mimi na nimepewa mimi na nimekujibu hivyo au ulisikia kuna Jafo au huyo mkuu wenu wa mkoa? Wao kazi si kutembea tu na ..... (anasema maneno yasiyofaa) kwenye miradi tunayotafuta sisi. Hivi sasa tuna tatizo la saruji usiniletee mambo ya wanasiasa hapa. Uliza swali jingine," alisema kwa sauti ya juu Kigurumjuli.

Aidha Kigurumjuli alikana kutoa maagizo kwa mkarandasi yanayowataka waandishi wa habari kuwa na vibali vya maandishi kutoka kwake wanapotaka kuripoti habari za ujenzi wa soko la Tandale.

Taarifa ya kuwepo kwa zuio hilo kwa waandishi wa habari lilitolewa na meneja miradi wa Kampuni Namis, James Msumali ambaye baada ya kufikiwa na Tanzania PANORAMA Blog na kuombwa kuzungumzia mkwamo huo alisema mkataba wa ujenzi una kipengele kinachozuia kutolewa kwa taarifa yoyote ya ujenzi wa soko mpaka kiwepo kibali cha maandishi kutoka Kigurumjuli.

Hata hivyo, Mkurugenzi wa kampuni ya Namis Thomas Uiso ambaye awali alikuwa ameitaka Tanzania PANORAMA Blog kumpelekea maswali kwa maandishi ili naye apate wasaa mzuri wa kuyajibu, ombi ambalo lilitekelezwa, alipotafutwa wiki iliyopita aliandika ujumbe wenye maneno machafu badala ya kujibu na muda mfupi baadaye aliufuta kisha alipiga simu na kueleza kuwa soko la Tandale linasimamiwa na Mkurugenzi ambaye ameagiza mwandishi yoyote anayetaka taarifa aelekezwe kwake.

"Maswali gani, wewe......(anaandika maneno ambayo hatuwezi kuyaandika). Nimepata taarifa zako mkurugenzi kanambia, hovyo sana wewe kumbe unachimba maisha ya watu. Ukimtaja Jafo au Kunenge ndiyo watu tutaogopa? Hao ni ........ (Anaandika maneno yasiyoandikika) huu ni utawala mwingine utapotea wewe na hutamuona Jafo wala Kunenge.

"Kuwa gentleman bhana, hapa ni mjini, haya ni maisha. Kwani unadhani hata nikiharibikiwa wewe ndiyo utapewa hiyo tenda? Ondoa huo uchafu ulioandika kwenye blog yako halafu kamuone mkurugenzi maisha yaendelee...., »alisema Uiso.

WIKI ILIYOPITA Tanzania PANORAMA Blog iliripoti kuwa, WAKATI Serikali ya Awamu ya Tano ikiwa imeelekeza nguvu kubwa kwenye ujenzi wa miundombinu, shule, hospitali na masoko, jitihada hizo zimeanza kuonyesha dalili ya kuingia doa baada ya kusimama kwa ujenzi wa soko jipya la Tandale.

Katikati ya hilo, msimamo wa serikali ya awamu ya tano wa kutoa taarifa zinazohusu shughuli za maendeleo bila ukiritimba, zinazofanywa na serikali ili kutoa fursa kwa wananchi kujua miradi inayotekelezwa kwa kodi zao, nao unaonekana kuingia doa baada ya mkandarasi anajenga soko la Tandale kuweka zuio la upatikanaji wa taarifa hizo.

Haya yamebainika baada ya Tanzania PANORAMA Blog kufika eneo la ujenzi wa soko jipya la Tandale mapema wiki iliyopita kufuatilia maendeleo ya ujenzi wa mradi huo baada ya kudokezwa na baadhi ya wafanyakazi kuwa umesimama kutokana na ukosefu wa fedha.

Tanzania PANORAMA baada ya kufika katika eneo la mradi lilishuhudia mafundi wakiwa wamekaa kivulini huku ujenzi ukiwa hauendelei na baada ya kuwahoji baadhi yao walisema wanasubiri kulipwa fedha zao waondoke kwa sababu mahali hapo hakuna kazi tena.

"Bora umekuja na sijui umeingiaje huku maana hamruhusiwi nyie kuingia humu na wakikuona watakugawana. Hapa hakuna kazi kama unavyoona ujenzi umesimama hakuna fedha. Tunasikia bosi hajalipwa huko serikalini ndiyo bado anafuatilia malipo lakini sisi tumeambiwa tukiulizwa tuseme tuna tatizo la simenti ambalo ni tatizo la kitaifa kwa sasa.

" Kama unaweza twende tukupeleke kwa msimamizi wetu ukamuhoji ila uwe unajiamini. Ila sisi tunasubiri akipata pesa kutoka serikalini akitulipa ndiyo basi tunatafuta kazi sehemu nyingine maana hata wiki hii mnafanya kazi wiki ijayo hakuna kazi sasa tunajiuliza hiyo serikali inatoa hela kwa wiki?" alisema mmoja wa mafundi hao.

Msimamizi wa mradi ambaye alipofikiwa na Tanzania PANORAMA na kuulizwa kwanza alielekeza afuatwe ofisini ambako alichukua simu na kuwasiliana na makao makuu ya kampuni yake kisha alisema;

"Unasema kuna wenzako kwenye gari wanakusubiri .... umesema hujapiga picha.... hili ni eneo la site, mtu yoyote haruhusiwi kuingia humu bila kibali cha makao makuu, awe mkuu wa mkoa, awe waziri anapotaka kuja hapa ni lazima awe na kibali kwa sababu anaweza kuangukiwa na kitu kizito kama nondo au ubao ukaaumia.

"Sasa nimeongea na makao makuu, nadhani umeona naongea na simu, kama una maswali nenda huko watakujibu na kama unataka kutembelea hapa uje na kibali cha maandishi kutoka makao makuu.

"Tena tumekuheshimu sana kwa sababu umeingia eneo ambalo haliruhusiwi ila kwa vile una wenzako nje njoo nikipitishe njia salama usije ukajikwaa halafu mkaanza kutunga uongo, " alisema.

Tanzania PANORAMA lilifika Makao Makuu ya Kampuni ya Namis, iliyopo Mbezi Africana ambayo ndiyo iliyopewa kandarasi ya kujenga soko la Tandale kwa ajili ya kupata maelezo ya kasimama kwa ujenzi wa soko hilo na kuelezwa kuwa mkataba wa ujenzi una kipengele kinachozuia kutoa taarifa yoyote ya mwenendo wa ujenzi isipokuwa kwa kibali cha Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni.

Akizungumza kuhusu katazo hilo lililo kwenye mkataba huo, Meneja Mradi aliyejitambulisha kwa jina la James Msumali alisema changamoto zinazowakabili katika ujenzi huo anaweza kuzizungumzia iwapo atapata idhini ya maandishi kutoka kwa Mkurugenzi wa Manispaa.

"Mimi ndiyo meneja mradi na ndiye ninayeweza kuzungumza, boss unayetaka kuonana naye hayupo. Utaratibu upo hivi, mkataba wetu una kipengele kinachoelekeza kuwa taarifa yoyote ya mradi haiwezi kutolewa mpaka kwa Kibali cha Mkurugenzi.

"Tena Kibali cha maandishi au anipigie simu yeye mwenyewe aseme nitoe taarifa kwako. Kwa hiyo nenda Manispaa kamtafute Mkurugenzi muombe kibali au mwambie anipigie simu ndiyo uje nikueleze hicho unachotafuta," alisema Msumali.

Alipofikiwa na kuelezwa hali hiyo, Mkurugenzi wa Manispaa ya Kinondoni, Aron Kigurumjuli alihoji ni kwanini Tanzania PANORAMA linafuatilia mradi wa ujenzi wa soko la Tandale wenye kelele nyingi badala ya  kuandika maendeleo ya ujenzi wa jengo la Ghorofa la ofisi ya Mkurugenzi au ujenzi wa bwawa na kufua umeme la Mwalimu Nyerere.

"Kwanini Ujenzi wa Soko la Tandale ambalo lina kelele nyingi saaana. Kwanini huandiki kuhusu ujenzi wa ghorofa hiyo hapo sasa umefikia ghorofa ya nne, kwanini huandiki kuhusu ujenzi wa bwawa la Mwalimu Nyerere? Kwanini huandiki kuhusu ujenzi wa Reli ya Kisasa, kwanini huandiki kuhusu stendi Mpya ya mabasi ya Dad es Salaam?

" Lakini nimeitwa mahali sasa siwezi kuwasiliza kwa sababu nimeitwa na wakubwa. Njooni kesho," alisema Kagurumjuli.

Alipotafutwa siku iliyofuata alisema kusimama kwa mradi huo kunachangiwa na sababu nyingi ikiwemo ya kukosekana kwa saruji. Alipoulizwa kuhusu zuio la kuandika habari za soko hilo alisema halitambui isipokuwa mwananchi anapaswa kufuata utaratibu kuingia katika miradi ya aina hiyo.

"Hilo zuio silijui na nitoe barua kwa mwandishi kwenda kuandika habari kutok lini hiyo. Hao watakuwa na yao lakini wananchi wanaruhusiwa kuingia kwenye miradi ya aina hiyo kwa kufuata utaratibu maalumu ulioandaliwa na (project manager) Meneja mradi," alisema Kagurumjuli.

Alipotafutwa Mkurugenzi Mtendaji wa Namis Corporate Ltd, Uiso alikataa kuzungumza lolote na kueleza aulizwe meneja mradi, Msumali.

Tanzania PANORAMA inaendelea kufuatilia sakata hilo.

TANZANIA INA WATU THABITI AFRIKA- DK ABBAS

 


NA MWANDISHI WETU

KATIBU Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dk. Hassan Abbas emesema watanzania ni watu thabiti  ba webte historia ya kutukuka katika mapambano ya ukombozi wa Bara la Afrika.

Dk Abbas ameyasema hayo jana alipotembelea makao makuu ya ofisi za Ukombozi wa Bara la Afrika kujionea changamoto zinazoukabili.

Akizungumza katika ofisi hizo, alisema Tanzania ni nchi yenye watu wenye historia thabiti barani Afrika kutokana na kushiriki kikamilifu kuzikomboa nchi nyingi barani Afrika.

"Tanzania si tu imetoa mchango mkubwa katika historia ya Ukombozi wa Afrika bali imegharamika mno kuanzia watu wetu, fedha zetu na hata kuiweka nchi yetu katika hatari ya kushambuliwa.

“Viongozi wetu walifanya uthubutu mkubwa na sisi leo sio watu poa, tuko imara kuilinda nchi yetu na sisi tuliopewa dhamana ya mradi huu lazima tutimize wajibu wetu ili kuitunza historia hii na kuwajengea vijana wa sasa uzalendo na utamaduni wa kuwa watu wa kuthubutu kwa ajili ya nchi yao na Afrika," alisema Dk. Abbas.

Katibu Mkuu Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dk. Hassan Abbas

Alisema kutokana na umuhuimu wa ofisi hizo ambazo Umoja wa Afrika (AU) uliamua makao makuu yake yawe Dar es Salaam na serikali imeuweka chini ya usimamizi wa Idara ya Utamaduni katika wizara ya Habari sasa unahamishwa kutoka Idara ya Utamaduni na kuwa moja kwa moja chini ya Ofisi yake.

"Tunataka kwenda kasi na kwa viwango, wazee wetu walithubutu kufanya mambo makubwa kutufikisha hapa tulipo, sasa naona mnafanya kazi kubwa lakini mradi huu bado unachangamoto nyingi ambazo Idara ya Utamaduni pekee haiwezi kuzipeleka kwa kasi, watabaki washauri wa kitaalamu tu kwangu na kwa mradi huu, lakini kuanzia leo 7, Disemba, 2020, mratibu wa mradi huu atawajibika na kuripoti moja kwa moja kwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari," aliagiza Dk. Abbas.