banner

Friday, December 4, 2020

WATUHUMIWA WA DAWA ZA KULEVYA WAFANYA MITIHANI YA KIDATO CHA NNE

 



NA MWANDISHI WETU

JESHI la Polisi limewaruhusu wanafunzi saba wanaosoma kidato cha nne katika Shule ya Sekondari ya St Mary’s, waliokamatwa wakivuta dawa za kulevya aina Bangi kufanya mitihani ya kumaliza kidato cha nne.

Akizungumza na Tanzania PANORAMA Blog, Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Kipolisi wa Kinondoni (RPC), Kamishna Msaidizi Ramadhani Kingai amesema, polisi imewaruhusu wanafunzi hao kufanya mitihani ya kumaliza elimu ya sekondari kwa sababu za kiutu na watakapomaliza hatua za kisheria dhidi ya tuhuma zao zitachukuliwa.

RPC Kingai amesema atatoa taarifa ya hatua zitakazochukuliwa na polisi Jumatatu, Oktoba 7, 2020a ambapo watakuwa wamekamilisha uchunguzi ukiwemo wa kutoweka kwa mwanafunzi aliyekuwa akisoma kidato cha tatu katika shule, Labna Salim Said.  

Vijana hao saba ambao majina yao hayajatajwa walikamatwa wakivuta na wakiwa na misokoto mingi ya bangi ndani ya nyumbani ya Kamishna Msataafu wa Jeshi la Magereza wakati wa msako wa Labna na baada ya kupekuliwa kwa nyumba hiyo ilingulika kuwa na shamba la bangi ndani ya ua unaoizunguka.

RPC Kingai alikataa kulitaja jina la Kamishna huyo na mahali ilipo nyumba yake ambamo walikutwa vijana hao wakiwa na misokoto ya bangi pamoja na shamba la bangi.

Katika hatua nyingine, RPC Kingai alisema hadi sasa polisi haijafanikiwa kumpata mwanafunzi Labna lakini juhudi za kumtafuta zinaendelea.

 Mwanafunzi msichana Labna wa Shule ya Sekondari ya Bweni ya St. Mary’s iliyoko Mbezi Makonde alitoweka shuleni tangu Oktoba 4, 2020 na kutokomea kusikojulikana na hadi sasa hajapatikana lakini katika hatua ya kushangaza Labna ambaye alitoweka akiwa chini ya uangalizi wa shule, taarifa za kutoweka kwake zilitolewa Oktoba 8, 2020 na matron wake Sarah Murra aliyempigia simu mama mzazi wa Labna akiulizia kama ameishafika nyumbani.

Uongozi wa Shule ya Sekondari ya St Mary’s haukutoa taarifa polisi kuhusu kutoweka kwa mwanafunzi huyo na badala yake wazazi ndiyo walioripoti tukio la mtoto wao kupotea akiwa shuleni.

Thursday, December 3, 2020

MBOWE AWEZA KUFUNGWA HADI MIAKA MIWILI

 




NA MWANDISHI WETU

MWENYEKITI wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) Freeman Mbowe anaweza kufungwa gerezani kifungo cha mpaka miaka miwili iwapo Mkurugenzi wa Mashtaka, Biswalo Mganga ataondoa huruma yake dhidi ya kosa alilolifanya yeye na wenzake la kudharua kwa makusudi nembo ya Taifa.

Hilo limebainika katika uchunguzi wa Tanzania PANORAMA Blog kuhusu makosa yanayoangukia kwenye kifungu namba saba (7) cha sheria ya Nembo ya Taifa ambayo Mbowe na wenzake waliyafanya wakati wa mkutano wa Baraza Kuu la Chadema wa kumchagua mgombea urais na makamu wake Mwaka 2020, katika ukumbi wa Mlimani City, siku chache kabla ya kuanza kwa kampeni zilizodumu kwa siku 60.

Kumbukumbu zilizopo zinaonyesha kuwa katika mkutano huo uliohudhuliwa pia na Tundu Lissu ambaye kitaaluma ni Mwanasheria anayezijua vema sheria za nchi, Lazaro Nyalandu, waziri wa zamani wa Maliasili na Utalii ambaye pia anazifahamu vema sheria na Mbowe ambaye alikuwa Mbunge katika Bunge la 11 akishiriki kutunga sheria za nchi, aliliiongoza baraza hilo kuimba wimbo wa Taifa huku yeye na wenzake hao wakiongezea maneno ambayo hayapo kisheria kwenye wimbo wa taifa.

Kwa mujibu wa sheria, kitendo hicho cha Mbowe na wenzake ni uvunjifu wa sheria namba saba kwa kuufanyia dhihaka wimbo wa taifa hivyo alipaswa kukamatwa yeye na wenzake wote waliofanya dhihaka hiyo na kushtakiwa mahakamani.

Hata hivyo Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP) Biswalo Mganga, mapema wiki hii ameeleza kuwa hakuamuru kukamatwa kwa Mbowe na wenzake kwa kutanguliwa na busara ya kutoleta sintofahamu katika taifa kipindi cha uchaguzi mkuu.

DPP, Biswalo Mganga


Kauli hiyo ya DPP Mganga imepata nguvu kubwa kutokana ukweli uliopo kuwa wakati wote wa kampeni na kipindi cha uchaguzi mkuu, maadui wa taifa na hasa mataifa ya mabeberu walilenga kuibua hekaheka ambazo zingezaa machafuko na kuifanya nchi isitawalike, yakiwatumia wanasiasa watanzania vibaraka wanaoishi katika mataifa hayo.

Katika hatua ya kushangaza, Mbowe ambaye haina shaka anajua kuwa alitenda kosa na anapaswa kushtakiwa lakini bado yupo huru, ameanzisha chokochoko zinazoashiria kumshinikiza DPP Mganga kutokuwa na huruma na wale wote waliotenda kosa la kudharau kwa makusudi nembo ya Taifa.

Chokochoko hiyo ya Mbowe imedhihirika mwishoni mwa mwezi uliopita baada kuongoza kikao cha Kamati Kuu ya Chadema iliyoketi kiimla kusikiliza na kuhukumu wabunge 19 wa viti maalumu wa chama hicho, kwa kutamka maneno yenye mwelekeo wa kutaka mmoja wa wabunge hao aliyekuwa akishtakiwa kwa kosa kama hilo hilo alilolifanya Mbowe la kudharau nembo ya taifa, arejeshwe gerezani baada ya DPP kumuachia kwa mamlaka aliyonayo kisheria.

Julai 4, 2020, Mbunge huyo akiwa katika Kijiji cha Puma, Wilaya ya Ikungi, Mkoa wa Singida alitenda kosa la kuimba wimbo wa taifa huku akiongeza maneno ambayo hayamo kisheria kwenye wimbo huo huku akipandisha bendera ya Chadema.

 

DC MURO AIBUA FURAHA ILIYOPOTEA MIAKA 12 KWA WANANCHI WA KIJIJI CHA MANYIRE

 

Mkuu wa Wilaya ya Arumeru, Jerry Murro


NA MWANDISHI MAALUMU- ARUMERU

FURAHA ilipotea ya wananchi wa Kijiji cha Manyire, Kata ya Mlangarini, Halmashauri ya Arusha waliokuwa wamenyang'anywa ardhi yao na mtu aliyefahamika kwa jina moja la William, mapema wiki hii ilirejea upya baada ya Serikali ya Wilaya ya Arumeru kuwarejea ardhi hiyo.

Shangwe zilizoambatana na vigelegele vya akina mama ziliibuka katika eneo ulipokuwa ukifanyika mkutano wa kutatua mgogoro wa ardhi baina ya wananchi wa kijiji hicho na William, baada ya Mkuu wa Wilaya ya Arumeru (DC), Jerry Muro kutangaza kuwa ardhi iliyokuwa imetwaliwa na Wiliam kutoka kwa wananchi hao imerejeshwa rasmi kwao na serikali.

Katika mkutano huo uliofanyika mapema wiki hii kijiji hapo, William alitakiwa na DC Muro kuwasilisha nyaraka zake zote zilizokuwa zikimpa uhalali wa umiliki wa ardhi lakini baada kukaguliwa na wataalamu wa ardhi wa serikali ilibainika kuwa hakukuwa na nyraka yoyote kati ya alizowasilisha iliyokuwa ikimpa uhalali huo.

"Nimekuja hapa ili tumalize hili tatizo lililodumu kwa miaka mingi! Hii ni serikali makini na Rais John Pombe Magufuli ametutuma tuje tusikilize kero zenu wananchi.

" Nimekuja, nimekagua, nimezunguka eneo ambalo kuna mgogoro wa ardhi uliosababisha nyumba kuchomwa moto. Tumeangalia vielelezo na nyaraka zote za maeneo ambayo Mzee William anasema ni mali yake.

"Hakuna nyaraka hata moja imethibitisha maeneo hayo ni mali ya Mzee William. Jinsi alivyopata hana vielelezo na hana nyaraka yoyote inayosema maeneo hayo ni mali yake.

" Hivyo serikali imejiridhisha na tunatamka maeneo yale ambayo wananchi walinyang'anywa na Mzee William tumewarudishia," alisema DC Muro.

Kutolewa kwa kauli hiyo na DC Muro kuliibua shangwe kutoka kwa wananchi na baadhi yao waliishukuru serikali ya wilaya kwa kuumaliza mgogoro huo wa ardhi uliokuwa ukihatarisha hali ya amani katika Kijiji cha Manyire.

DC Muro alifika kijijini hapo mapema wiki hii akiwa amefuatana na baadhi ya wataalamu wa ardhi kukagua uharibifu uliotokea kwenye nyumba iliyochomwa moto kwa sababu ya mgogoro wa ardhi.

Akiwa kijijini hapo DC Muro alifanya kikao na wananchi pamoja na boma la Mzee William ambapo watalaamu wa ardhi  walipitia upya vielelezo vya umiliki wa ardhi vya kila upande na kubaini upungufu mkubwa katika nyaraka za William.

 

SERIKALI KUANDAA TAMASHA, TUZO KUBWA ZA SANAA

 

Katibu Mkuu Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Dk. Hassan Abbas


NA MWANDISHI WETU

SERIKALI iko mbioni kuandaa tamasha kubwa la muziki na sanaa litakalofahamika kwa jina la moja ya vivutio vikubwa vya utalii vilivyopo hapa nchini.

Akizungumza wiki hii jijini Dar es Salaam na wadau wa sanaa na muziki, Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dk. Hassan Abbas amesema kwa kutambua urithi mkubwa wa sanaa uliopo nchini ukiwemo muziki, filamu, ngoma na uga mwingine, serikali kwa kushirikiana na wadau, itaratibu tamasha kubwa la aina yake litakalofanyika baadaye mwaka huu.

Dk. Abbas alisema sekta hiyo inapaswa kuhakikisha inaiburudisha jamii ya watanzania wachapakazi ipasavyo na kwamba sambamba na kuandaliwa kwa tamasha hilo, pia serikali kwa kushirikiana na wadau itarejesha tuzo za muziki na sekta nyingine zilizo chini ya wizara inayoiongoza..

"Moja ya kazi kubwa ya sekta ya sanaa nchini ni kuhakikisha jamii yetu inayochapa kazi sana kwa sasa inaburudika ipasavyo, sasa naona sanaa inakuja tu pale panapokuwepo mdhamini au mwandaaji fulani asipokuwepo hakuna matukio na nchi iko kimya.

"Serikali sasa inakwenda kuchechemsha sekta hii kwa kuratibu tamasha kubwa sana litakaloanzia Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam na kuendelea kuungana na Tamasha la Kimataifa la Sanaa Bagamoyo.


KAtibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Dk. Hassan Abbas akiwa katika picha ya pamoja na wadau wa wizara yake


"Tusisubiri wadhamini, wakija sawa, kama wako likizo basi mimi nasema sisi wenyewe tunaweza kwa umoja wetu sasa tukutane Uwanja wa Uhuru Disemba 26 mwaka huu na kisha Desemba 27 twende Bagamoyo.

"Wasanii wakiungana watajaza uwanja. Twende tutateremsha wasanii wetu wote ambao ni urithi wa sasa na baadaye wa nchi hii halafu tuone kama watu hawatakuja," amesema Dk. Abbas.

Dk. Abbas yupo katika ziara ya kikazi ya kukutana na wadau mbalimbali wa sanaa na sekta nyingine zilizo chini ya wizara yake.

 

Tuesday, December 1, 2020

NGUVU YA BUNGE YAJARIBIWA NA CC YA CHADEMA

 


NA MWANDISHI WETU

 HATIMAYE imebainikiwa kuwa uamuzi wa Kamati Kuu (CC) ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kuwavua uanachama makada wake 19 wanawake, kinaowatuhumu kwa utovu wa nidhamu na kula kiapo cha kuwa wabunge wa viti maalumu bila kupitishwa na chama ni mwendelezo wa matukio yake ya 'kisanii'

Hayo yameelezwa na wataalamu bingwa wa mambo ya kibunge, Wataalamu wa Katiba, Wanasheria nguli wa Sheria za Uchaguzi na maafisa wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) katika mahojiano maalumu na Tanzania PANORAMA Blog kuhusu hatua ya Kamati Kuu ya Chadema kuwavua ubunge makada wake hao na uhalali wa uamuzi wa Spika kuwaapisha nje ya ukumbi wa Bunge.

Mmoja wa watalaamu waliobeba katika mambo ya mabunge ya Jumuiya ya Madola ambaye ni mshauri na mkufunzi wa kanuni, utamaduni, utaratibu na mienendo wa mabunge barani Afrika ameeleza kuwa uamuzi wa Kamati Kuu ya Chadema ni mchezo wa kisiasa wenye lengo la kukirudisha chama hicho midomoni na masikioni mwa watanzania wakati huu kinapoelekea kutoweka.

Alisema kisheria, kikanuni na utamaduni wa mabunge wa Jumuiya ya Madola, wabunge 19 wanawake wa viti maalumu wa Chadema hawana kosa lolote katika mchakato mzima uliowezesha kuapishwa kwao hivyo hawapaswi kuhukumiwa kwa namna yoyote ile.



Alisewa mbali na wabunge hao, Spika wa Bunge, Job Ndugai pia hana kosa kwa sababu hajakiuka sheria na kanuni za Bunge kuwaapisha wabunge hao na wala hajatenda kinyume na tamaduni na taratibu za kibunge ambapo Bunge la Tanzania linafuata mfumo wa kiuendeshaji wa mabunge ya Jumuiya ya Madola.

Alisema kabla ya kuapishwa kwa wabunge hao kulikuwa na mawasiliano ambayo kisheria ni ya siri baina ya chama cha siasa husika na Tume ya Taifa ya Uchaguzi yaliyohusu uwasilishaji na upokeaji wa orodha ya watu wenye sifa za kuwa wabunge, orodha ambayo baada ya kupokelewa na NEC, ilifanyiwa kazi kisha ikawasilishwa kwa Spika.

"Kwa mujibu wa sheria, katibu mkuu wa chama ndiyo mwenye jukumu la kuwasilisha majina NEC na kwa maelezo ya NEC hilo lilifanyika. Na mawasiliano kati ya chama cha siasa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi kuhusu chama kuwasilisha orodha ya majina ya watu wenye sifa kuwa wabunge wa viti maalumu na tume kuyapokea na kuyafanyia kazi huwa siri.

 


"Yakishafanyiwa kazi na NEC ndiyo humjulisha Spika na yeye huendelea na taratibu za kibunge.

"Wakati hayo yakitendeka baina ya Katibu Mkuu wa Chadema na NEC, wabunge hawakupewa fursa ya kujua mawasiliano yaliyofanyika na hawakupaswa kujua. Baada ya hilo walijulishwa na chama chao kuwa wameteuliwa kuwa wabunge na walipaswa kuripoti bungeni.

"Spika yeye alipokea barua tu toka NEC kumjulisha juu ya uteuzi huo na ndiyo utaratibu ulivyo, Spika hutaarifiwa na NEC. Sasa mpaka hapo wabunge hao 19 na Spika hawawa kosa lolote.

"Labda kama NEC ingesema aliyeandika barua siyo katibu mkuu na kwa hiyo orodha ya Chadema isingepokelewa lakini NEC imesema wazi katika tamko lake kuwa orodha hiyo ilitoka Chadema.

"Kwa hiyo Chadema iweke wazi na ijibu kauli ya NEC kuwa wao ndiyo waliandika barua na kuwasilisha orodha ya wabunge wa viti maalumu bila kuwa na sharti la namna walivyopatikana kwa sababu siyo hitaji la NEC kujua, badala ya kumshambulia Spika na kudhalilisha wabunge waliokwishaapishwa" alisema mtaalamu huyo wa mambo ya kibunge ya Jumuiya ya Madola.



Mbali na huyo, mwanasheria nguli wa sheria za uchaguzi na masuala ya Katiba ambaye naye hakupenda kutajwa jina lake, yeye alisema wabunge 19 wa viti maalumu wa Chadema hawawezi kutengua kiapo chao na uamuzi wa Kamati Kuu ya Chadema hauwazuii kuendelea kutekeleza majukumu yao ya kibunge.

"Mambo ya hicho chama sipendi kuyaongelea kisheria kwa sababu kila siku wanaibuka na jambo. Lakini nitakueleza kisheria ilivyo ila sitaki kuandikwa jina mimi kwa sababu sihitaji kuingia kwenye malumbano ya kisanii na hao watu. Naeleza kuwajuza watanzania.

"Kwa namna yoyote ile wabunge 19 wa viti maalumu wa Chadema wataendelea na wajibu wao, sioni sababu ya kutengua kiapo chao.

"Kuapa nje ya Bunge ni sharti jipya la kikanuni kwa wabunge waliochelewa kuapa kabla ya ufunguzi wa Bunge na Spika mwenyewe amekwishalitolea ufafanuzi na lipo ndani ya kanuni za Bunge labda kama hao Chadema hawasomi kanuni.

"Kwa msingi huo sharti hilo linapata nguvu ya ibara ya 89 ya Katiba kwa kutunga Kanuni za Bunge na ndiyo uwepo wa kanuni hiyo mpya.

"Lakini Pia anayetuhumu ndiyo mwenye jukumu la kuthibitisha pasipo shaka kuwa barua ile siyo yao na siyo ya NEC. Chadema watoke wakanushe kama barua iliyopo NEC siyo ya kwao.

"Upo ushahidi wa kutosha kuwa Katibu Mkuu wa Chadema, John Mnyika aliwasilisha barua ya orodha ya wabunge wa viti maalumu kwa rejista na mawasiliano ya simu na ofisi ya NEC baada ya kuomba ajulishwe rasmi kwa barua sharti la kuwasilisha orodha ya majina ya wabunge wa viti maalumu," alisema ngwiji huyo wa Sheria za Uchaguzi na Mambo ya Katiba.

Alitoa mfano kuwa kinachofanya na Chadema ni sawa sawa na mbunge aliyetambulishwa na chama chake kuwa mgombea, baada zoezi la uchaguzi anapopewa hati ya kutangazwa kuwa mbunge na baadaye kwenda kula kiapo anafukuzwa na chama chake.