banner

Monday, December 21, 2020

WATANZANIA NA USINGIZI WA NJOZI TATU


NA MWANDISHI WETU

KWA mwaka wa pili sasa, Watanzania wanalala usingizi ulioambatana na jonzi tatu.

Njozi hizo ni, mosi; Wakala wa Barabara (TANROADS), pili; barabara ya juu iliyopo eneo la Tazara inayofahamika zaidi kwa jina la Mfugale Flyover, na tatu; Mhandisi Patrick Mfugale.

Walianza kuota njozi hizi usiku wa kuamkia Septemba 16, 2018 baada ya kuanza kutumika kwa barabara ya juu ya Mfugale iliyopo eneo la Tazara, Septemba 15, 2018.

Kabla ya hapo, Watanzania hasa waliokuwa wakitumia barabara ya Julius Nyerere na Nelson Mandela, walikuwa wanaota wamefukuzwa au kupewa barua ya karipio kali kwa kuchelewa kazini.



Wasafiri walikuwa wanaota wameachwa na ndege au treni na wafanyabiashara waliota hasara na kupoteza saa nyingi wakiwa katika foleni.

Ali Msafiri, mfanyabiashara na mkazi wa eneo la Gongo la Mboto jijini Dar es Salaam ambaye alihudhuria uzinduzi wa Mfugale Flyover alinukuriwa na vyombo vya habari akieleza hivi:

"Kuzinduliwa kwa Mfugale Flyover kutaturahisishia usafiri wakazi wa Jiji la Dar es Salaam na hata wasiokuwa wakazi wanaofika katika jiji hili kubwa la kibiashara nchini Tanzania.

"Wananchi tutakuwa tumepata fursa na foleni na msongamano utabaki ndoto sasa. Lile tatizo sugu na la miaka mingi la kwenda kazini sasa naona limeisha."

Watanzania wengi walikuwa wakilala hoi kutokana na shida ya usafiri iliyokuwa ikisababishwa na foleni. Wakazi wa Jiji la Dar  es Salaam wanaotumia barabara za Nyerere na Mandela kwenda kazini na kurudi nyumbani walilazimika kulala kuanzia saa tano usiku na kuamka saa 10 alfajili ili kuwahi kupambana na foleni.



Wasafiri wanaosafiri kwa ndege au treni ya Tazara nao walilazimika kutenga muda wa hadi saa tatu za kutoka katikati ya Jiji la Dar es Salaam au pembezoni kwenda uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere au Stesheni ya Reli ya Tazara kwa sababu ya foleni na msongamano wa magari.

Wafanyabiashara na wasafirishaji wanaotumia barabara hizo walikuwa wakipoteza fedha na muda mwingi kukabiliana na foleni na shughuli za kiuchumi kwa taifa na raia mmoja mmoja zilikuwa zikikutana na changamoto kubwa kutokana na tatizo la foleni katika barabara hizo.

Daniel Masanja, Dreva la roli ambaye mara nyingi hutumia barabara ya Mandela kusafirisha mizigo inayotoka bandarini ambaye naye alihudhuria uzinduzi huo, yeye alikaririwa akisema hivi;



"Kulikuwa na shida kubwa sana. Tulikuwa tunapoteza fedha nyingi sana kwa kukaa saa nyingi barabarani, sasa tutasafirisha mizigo ya wateja na kuifikisha kwa wakati, hakika tutaongeza tija. Tutalala tukiota njonzi njema za barabara ya juu ya Mfugale."

Septemba 16, 2018, wanafunzi, wafanyakazi, wafanyabiashara, wasafirishaji na wasafiri walitumia barabara za Nyerere na Mandela kwa mara ya kwanza zikiwa hazina msongamano baada ya kuzinduliwa kwa Mfugale Flyover.



Mfugale Flyover ni barabara ya kwanza ya juu katika historia ya Tanzania inayounganisha sehemu kuu za Jiji la Dar es Salaam na maeneo makuu ya kiuchumi kama Uwanja wa Ndege wa Julius Nyerere, Bandari ya Dar es Salaam, machinjio ya Vingunguti na barabara zinazoelekea viwandani.

Ni barabara inayojumuisha njia kuu nne na daraja. Imetatua tatizo la msongamano na foleni na sasa imeongeza muda wa watu kufanya kazi badala ya kutumia muda mwingi wakiwa wamekwama barabarani kwenye foleni.

Kuanza kutumika kwa Mfugale Flyover kumewafanya Watanzania na wageni wanaotumia barabara za Nyerere na Mandela kulala usingizi mwororo huku wakiota ndoto ya kupita barabara ya juu ya Mfugale kuwahi katika shughuli zao za kiuchumi, masomo na usafiri.



Hii ndiyo ndoto ya kwanza ambayo Watanzania wanaota sasa kila walalapo usingizi.

Ndoto ya pili wanayoota sasa Watanzania ni TANROADS. Watanzaia wanaiota TANROADS kuwa taasisi yao iliyoshirikiana na kampuni kubwa ya ujenzi kutoka Japan ya Sumitomo Mitsui Construction Co. LTD kujenga barabara ya kwanza ya juu iliyopewa jina la Mhandisi Mfugale kwa mafanikio makubwa.



Wanaota maneno ya Rais wa Tanzania, Dk. John Pombe Magufuli aliyeitaka TANROADS kuitunza barabara hiyo na sasa ikiwa imepita miaka miwili tangu kuzinduliwa kwake, ipo katika mwonekano mzuri kutokana na uangalizi makini wa TANROADS.

Watanzania ambao sasa si taifa masikini tena wanaota mkataba wa ujenzi wa barabara hiyo uliosainiwa Oktoba 15, 2015 kati ya Tanzania National Roads Agency (TANROADS) na Sumitomo Mitsui Construction Co.,Ltd. (SMCC), lengo likiwa kuboresha makutano ya barabara ya Nyerere na Mandela. Lengo ambalo limefikiwa.



Awali wengi walikuwa wakiota kuwa ujenzi  wa barabara za aina hiyo hautawezekana Tanzania kwa sababu unagharimu matrilioni ya Dolla za Marekani ambayo Tanzania haina hivyo ili kuwa na barabara ya aina hiyo ni sharti kuomba mkopo kwa wazungu.

Sasa ndoto hizo hazipo, Watanzania wanaota shilingi bilioni 100 za kodi zao zinazokusanywa na Serikali ya Awamu ya Tano kuwa zinaweza kujenga barabara ya juu ya kisasa kama zile zilizoko Chicago na California nchini Marekani na wakiamka wanapita kwenye barabara ya aina hiyo.



Ni ndoto iliyosubiriwa tangu Aprili 16, 2016, siku ambayo Rais Magufuli alizindua ujenzi wa barabara hiyo ya juu.

Ndoto ya tatu inamuhusu Injinia Patrick Mfugale ambaye mchango wake katika ujenzi wa daraja hilo utabaki kuwa kielelezo cha Mtanzania mzalendo aliyetumia vema elimu yake kulinufaisha taifa lake.



Watu walio karibu pamoja na wasaidizi wake wanaeleza kuwa Injinia Mfugale ni mkali kwa watu wanaomsifia yeye binafsi hata kama anastahili kusifiwa. Anapenda sifa zinazomstahili zielekezwe kwa serikali anayoitumikia, taifa na Watanzania.

Kwa sababu ya ukali wake huo, Watanzania wamebaki kuuota uzalendo, utaalamu na uadilifu wake ndotoni. Haina shaka sifa zake nyingi zitatolewa hadharani na bila kuogopa katazo lake atakapokuwa hayupo.

Lakini kwa sababu katazo lake hilo siyo sheria hivyo haliifungi Tanzania PANORAMA Blog kumtendea haki, linafuata nyayo za Rais Magufuli ambaye kwa kuutambua mchango wake katika ujenzi wa barabara hiyo na utumishi wake uliotukuka kwa taifa alimpa heshima ya juu kwa kuiita kwa jina lake.



Dunia sasa inapaswa kumtambua Mhandisi Patrick Mfugale kuwa mtaalamu wa kwanza wa fani ya uhandisi duniani aliyetumia utaalamu wake kujenga sehemu kubwa ya miundombinu ya barabara na madaraja ya taifa lake.

Kumbukumbu za kazi za kihandisi zilizoonwa na Tanzania PANORAMA Blog mpaka sasa zinaonyesha kuwa rekodi ya Mhandisi Mfugale ya kusaidia kujenga madaraja 1400 katika nchi ya baba na mama zake haijafikiwa na mhandisi mwingine yeyote duniani.



Rekodi zinamtaja pia Mhandisi Mfugale kuwa mtaalamu wa kwanza wa fani ya uhandisi duniani ambaye baada kupata elimu ya juu ya uhandisi nje ya nchi hakulikimbia taifa lake kwenda kufanya kazi ughaibuni ambako wahandisi hulipwa mishahara minono, bali alirejea kulijenga na mpaka sasa amebuni na kusimamia barabara za Taifa la Tanzania zenye urefu wa zaidi ya kilomita 36,258.

Kwa mujibu wa rekodi za kihandisi zilizoonwa na Tanzania PANORAMA Blog, Mhandisi Mfugale ndiye pekee duniani mpaka sasa aliyetoa mchango mkubwa kwa nchi yake katika ujenzi wa miundombinu ya barabara.

Watanzania wanaoota taswira ya Patrick Mfugale kila wanapopita juu ya Mfugale Flyover wanapaswa kukumbuka maneno yake mbele ya Rais Magufuli siku ya ufunguzi wa barabara hiyo ili yawajengee uzalendo, unyenyekevu katika utumishi na uwajibikaji, aliposema;



"Ukiwa waziri wa ujenzi ulinituma Japan kwenda kuweka sahihi mkataba wa kazi hiyo, lakini tulikuwa hatujapata mkandarasi na ulinielekeza kuwa nisirudi huku mpaka niwe nimesaini mkataba.

"Na nilipoiambia Japan nimeambiwa na nchi yangu nisirudi, wakasema viza yako imeisha, kwa hiyo ni lazima urudi, nikasema ninaweza nikakaa hata railway stesheni, ili mradi kama mkimbizi lakini tenda hii tutafute namna ya kufanya daraja hili lijengwe,"

Mtu huyu Mhandisi Patrick Mfugale alizaliwa mkoani Iringa na kupata elimu yake ya msingi katika Shule ya Msingi ya Consolata ya mjini Iringa na 1975 alihitimu elimu yake ya shule ya upili katika shule ya upili mkoani Moshi.



Mwaka 1977, Mfugale aliajiriwa Wizara ya Ujenzi kabla ya kujiunga na Chuo Kikuu cha Rocky nchini India ambako alihitimu mwaka 1983  na kutunukiwa shahada yake ya kwanza ya uhandisi kisha akarejea nchini kuja kulijenga taifa lake

Mwaka 1991 Mhandisi Mfugale alisajiliwa kama mhandisi mtaalamu na mwaka 1992 aliteuliwa kuwa mkurugenzi wa barabara za mikoa.

Mwaka 1994 hadi 1995 alikwenda ughaibuni kusoma katika Chuo Kikuu cha  Loughborough, Braunshweig nchini Uingereza ambako alihitimu ya kutunukiwa shahada yake ya pili ya uhandisi na kisha akarejea tena nchini kuendelea kulijenga taifa lake.

Mwaka 1995  aliteuliwa kuwa mhandisi mkuu wa madaraja nchini Tanzania na wakati huo huo akiwa masomoni nchini Uingereza alitafiti na kutengeneza mfumo wa madaraja nchini Tanzania.



Mhandisi Mfugale alibuni Daraja la Magarasi lenye mita 178 lililogharimu shilingi za Tanzania milioni 300 na pia, kwa uchache amejenga
Daraja la Mkapa Rufiji, Daraja la Umoja linalounganisha Tanzania na Msumbuji, Daraja la Rusumo, Daraja la Kikwete na  Daraja la Nyerere huko Kigamboni


Wednesday, December 16, 2020

UBUNGO INTERCHANGE PICHA HALISI YA WATANZANIA


 

 NA MWANDISHI WETU

BARABARA za juu zilizopo eneo la Ubungo zinazofahamika zaidi kwa jina la Ubungo Interchange ni picha halisi ya uchapakazi, uwezo wa kiuchumi na utaalamu wa Watanzania.

Kila mtumiaji wa barabara hizo, awe mtanzania au raia wa kigeni licha ya kuvutiwa na uzuri wake anapopita juu yake, picha ya raia wazalendo wa Watanzania wanaoipenda nchi yao, pia humjia akilini.

Ubungo Interchange imejengwa na vijana wa kitanzania waliokuwa asilimia 90 ya wajenzi wote, imesimamiwa na wataalamu wa ndani ya Tanzania ambao ni Wakala wa Barabara (TANROADS) wakiongozwa na Mtendaji Mkuu, Patrick Mfugale huku meneja mradi akiwa Mhandisi Barakaeli Mmari.

Mfugale


Saruji, mchanga, nondo na vifaa vingine vyote vilivyotumika katika ujenzi wa barabara hizo kwa kiwango kikubwa ama zimetengenezwa na kuzalishwa na viwanda vya ndani vya Tanzania au ni vifaa vilivyo ndani ya Tanzania. Ubungo Interchange ni barabara za Watanzania zilizojengwa na Watanzania kwa kutumia akili, fedha, vifaa na nguvu kazi ya Watanzania wenyewe.

Barabara hizo za kuvutia katika ukanda wote wa Afrika Mashariki zinakutanisha barabara tatu za Mandela, Sam Nujoma na Morogoro na ujenzi wake ulikamilika Disemba, 2020.

Rais Magufuli


Rais John Pombe Magufuli alipotangaza mpango wa ujenzi wa barabara hizo kulikuwa na mapokeo ya aina mbili, kwanza ni Watanzania waliopokea taarifa za mpango huo kwa furaha kwa imani kwamba zitapunguza au kuondoa kabisa tatizo la msongamano wa magari katika eneo la Ubungo ambalo lilikuwa likidumaza sana uchumi wa mtu mmoja mmoja na taifa kwa ujumla.

Furaha hiyo pia ilijengeka katika nyuso za wananchi wengi kwa matumaini ya kupata ajira na zaidi ni tamaa ya maendeleo. Kila Mtanzania alitamani kuiona Tanzania ikiwa na interchange yenye mwonekano wa zile zilizo kwenye mataifa ya dunia ya kwanza

Mapokeo ya pili yalikuwa ya husda kutoka kwa maadui wa taifa ambayo nayo yaligawanyika katika makundi mawili makuu; la kwanza ni lile lililotamani mpango huo usifanikiwe na sababu yao kubwa ni kutotaka kuiona Tanzania ikipiga hatua za kimaendeleo huku kundi jingine ni lile lililotaka lihusike kwenye ujenzi ili kwanza livune pesa na kutoa ajira kwa watu wao ambao haina shaka wangeletwa kwa wingi kufanya kazi kwenye mradi huo na pia kutamani Tanzania iendelee kuwa tegemezi kwa kukosa pesa za ujenzi au kuomba msaada na wataalamu kutoka nje.

Matamanio haya yamekuwa hewa kwa sasa ambapo Watanzania wengi wanayaishi maono na falsafa za Rais Magufuli zinazowafanya watembee kifua mbele kwa sababu wanaamini wanaweza kuijenga nchi yao wenyewe na TANROADS imekuwa mfano bora kabisa katika hili.



Mei 2020, Mhandisi Barakaeli Mmari alipoutangzia umma kuwa kwa mara ya kwanza barabara ya ghorofa ya chini ya Morogoro itafunguliwa kwa majaribio ifikapo Mei 30, 2020 kwa kuruhusu magari kupita na Septemba 30, 2020 barabara ya ghorofa ya pili ya Nelson Mandela / Sam Nujoma itafunguliwa kwa majaribio pia, Watanzania na raia wa nchi jirani wanaotumia barabara ya Morogoro kama lango kuu la kuingilia jijini Dar es Salaam walianza kushuhudia picha halisi ya Tanzania mpya.



Mhandisi Mmari ambaye alitoa darasa la matumizi ya barabara hizo alisema kuna barabara ngazi tatu, ya chini, ya kati na ya juu. Ngazi ya chini itatumiwa na magari yanayotoka mjini kwenda Mwenge, Mwenge-Kimara, Kimara-Buguruni na Buguruni kwenda mjini. Vile vile, itatumiwa na magari yote yatakayokuwa yanapinda kushoto kwenye maungio hayo.

Alisema ngazi ya kati itatumiwa na magari yanayotoka Kimara kwenda mjini na yatokayo mjini kwenda Kimara.



Ngazi ya juu itatumiwa na magari yatokayo Mwenge kwenda Buguruni na yatokayo Buguruni kwenda Mwenge.

Mhandisi Mmari alisema barabara za juu zimejumuisha njia maalumu kwa ajili ya mabasi ya mwendo kasi.



Hivi sasa, Watanzania wakiwa wamezama katika ujenzi wa miradi mikubwa ya kitaifa, picha halisi ya ubora wa miradi hiyo inaonekana kwa kutazama na kupita juu ya barabara za ghorofa za Ubungo Interchange.

GULAM ATAFAKARI KUPAMBANA NA UBALOZI WA INDIA

 

Mwenyekiti wa Kampuni za MeTL, Gulam Dewji

NA MWANDISHI WETU

MFANYABIASHARI mwenye ukwasi wa kutosha ambaye kampuni, viwanda, mashamba na biashara zake zimetoa ajira kwa Watanzania na raia wa kigeni anatafakari kujibu mapigo dhidi ya Ubalozi wa India uliyoyataja makampuni yake kuwa siyo sehemu salama kufanya kazi.

Wiki iliyopita, siku moja baada ta Gulam kumpa maagizo mmoja wa wasaidizi wake kutuma ujumbe kwa Tanzania PANORAMA Blog wa kusaka suluhu baina ya menejimenti za Kampuni za Mohamedi Enterprises Tanzania Limited (MeTL) na wafanyakazi wa kigeni wanaodai kunyanyaswa alisema anajipanga kujibu mapigo.

Gulam alisema amesikitisha na tamko la ubalozi wa India lililosambazwa mitandaoni kwa sababu linalenga kuwatetea watu wanaomuibia na kumsumbua.

“Ndiyo nimeliona tamko kwani nani kasema hajui kuwa ni tamko la Ubalozi wa India, lakini mimi nasema nakusanya ushahidi halafu nitatoa tangazo kwa vyombo vya habari kwa sababu ubalozi unatetea wezi, unatetea watu wanaoniibia na kunitesa sana na hata polisi wanazo taarifa hizi. Sasa ninazungumza na ubalozi halafu nitatoa statement yangu ambayo mimi nitaitoa kama tangazo,” alisema Gulam.   

AWALI Tanzania PANORAMA Blog, iliripoti kuwa uongozi wa kampuni zilizo chini ya mwamvuli wa Mohamedi Enterprises Tanzania Limited (MeTL) umesema utatafuta njia ya kumaliza mgogoro baina yake na wafanyakazi ambao ni raia wa India katika meza ya mazungumzo.

Hayo yameelezwa na mmoja wa maafisa wa kampuni hiyo aliyetumwa na Mkurugenzi wa MeTL, Gulam Dewji kutoa ufafanuzi kwa Tanzania PANORAMA Blog kuhusu andishi lililowekwa kwenye mitandao ya kijamii likiwatahadhalisha raia wa India wote kuepuka kufanya kazi katika Kampuni za MeTL.

Andiko hilo mtandaoni linaeleza kuwa Ubalozi wa India umekuwa ukipokea kwa mfululizo malalamiko ya wafanyaakazi wa Kampuni za MeTL kunyanyaswa na uongozi pamoja na mwajiri wao kuwafungulia kesi za kughushi mahakamani kiasi cha kusababisha wanafamilia wa wafanyakazi hao kulazimika kurejea India.

Kwamba Mwenyekiti wa Makampuni ya MeTl, Gulam Dewji na maafisa waandamizi wamekuwa wakiwafanyia vitendo vya unyanyasaji na udhalilishaji wafanyakazi hao wanapofikisha malalamiko kwao.

Linahitimishwa kwamba raia wote wa India wasikubali kuajiriwa na Kampuni za MeTL kutokana na mwenendo usiofaa wa viongozi wake wa juu.

Alipoulizwa Mwenyekiti Gulam, kuhusu suala hilo kupitia simu yake ya kiganjani alisema aandikiwe maswali kwa maandishi ili ayajibu na alipoandikiwa, muda mfupi baadaye mtu mmoja mwenye asili ya kiasia alituma ujumbe kwa njia ya whatsapp akieleza kuwa ametumwa na Gulam kufikisha ujumbe kwa Tanzania PANORAMA Blog.

Ujumbe aliuotuma ulisomeka; ‘Bwana Dewji amezungumza na sisi na ametuhakikishia uwajibikaji wa menejimenti katika kulinda maslahi ya wafanyakazi. Tumekubaliana kuwa na mazungumzo ya kina, tungependa kutatua jambo hili kwa njia ya mazungumzo.’

Ujumbe mwingine chini ya huo aliuotuma ulisomeka; ‘leo hii mmelalamika mazingira ya watu wenu ila tusema ukweli pia mnawanyanyasa sana Watanzania sema tu wanashindwa nani wa kuwasemea pia kutokana na hali za maisha yao ila mazingira ya ufanyaji kazi siyo.

Jitahidi za Tanzania PANORAMA Blog kuzungumza na Ubalozi wa India kuhusu suala hili zinaendelea.    

MWANAFUNZI ALIYEPOTEA ST. MARY’S APATIKANA

 

Labna Said

NA MWANDISHI WETU

LABNA Salim Said,  mwanafunzi wa Shule ya Sekondari ya Bweni ya St. Mary’s iliyopo Mbezi Makonde ambaye alipotea tangu Oktoba 4, 2020, amepatikana.

Mwanafunzi huyo alipatikana Disembe 12, 2020, eno la Banana Relini akiwa amewekwa kinyumba na mwanaume ambaye jina lake halikufahamika mara moja baada ya kufanikiwa kuwakimbia polisi waliokwenda kuwakamata.

Taarifa za kupatikana kwa Labna zilithibitishwa na Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Kipolisi Kinondoni (RPC) Ramadhani Kingai katika mahojiano mafupi kwa njia ya simu ambaye alisema, taarifa za kupatikana kwa mwanafunzi huyo anazo lakini hawezi kuongea zaidi kwa sababu yupo kwenye kikao.

Mama mzazi wa Labna anayefahamika kwa jina la Rabia Swedan alisema walipata taarifa za kuwepo kwa mtoto wao eneo Banana Relini usiku na walifika eneo hilo wakiwa wameambatana na polisi wawili na kumkuta akiwa amelala chini pamoja na aliyemtorosha.

“Inasikitisha, tulipata taarifa za huyu mtoto kuwepo Banana Relini usiku, tukaenda Kituo cha Polisi Stakishari kuomba polisi, tukapewa wawili tukaambatana nao mpaka kwenye hiyo nyumba tukawakuta wamelala chini. Yule bwana aliyekuwa naye alipotuona na polisi akakurupuka akakimbia, sasa kwa sababu polisi walikuwa wawili hawakuweza kumfukuza.

“Mtoto alikuwa hoi, tulimpeleka Stakishari polisi huo usiku wa saa saba akakaa hapo wakimuhoji mpaka saa 12.00 asubuhi, kwa jinsi alivyokuwa wakatuambia tumpeleke hospitali.

“Tukampeleka Hospitali ya Amana na baada ya matibabu tukamchukua hadi Kituo cha Polisi Goba kwa sababu ndiko kesi yake inakopelelezwa, nao  wakamuhoji wakaturudishia tuendelee kumtibu ila akiwa na nafuu tutampeleka tena polisi,” alisema Swedan.   

Mwanafunzi msichana Labna wa Shule ya Sekondari ya Bweni ya St. Mary’s iliyoko Mbezi Makonde alitoweka shuleni tangu Oktoba 4, 2020 na kutokomea kusikojulikana hadi alipopatikana Disemba 12.

Labna alitoweka akiwa chini ya uangalizi wa shule lakini taarifa za kutoweka kwake zilitolewa Oktoba 8, 2020 na matron wake, Sarah Murra aliyempigia simu mama mzazi wa Labna akiulizia kama ameishafika nyumbani.

Katika hatua ya kushangaza, uongozi wa Shule ya Sekondari ya St Mary’s haukutoa taarifa polisi kuhusu kutoweka kwa mwanafunzi huyo na badala yake wazazi ndiyo walioripoti tukio la mtoto wao kupotea akiwa shuleni.

 

 

Thursday, December 10, 2020

MeTL YAZUNGUMZIA TUHUMA ZINAZOIANDAMA

 

Mwenyekiti wa Makampuni ya MeTL, Gulam dewji

NA MWANDISHI WETU

UONGOZI wa Kampuni zilizo chini ya mwamvuli wa Mohamedi Enterprises Tanzania Limited (MeTL) umesema utatafuta njia ya kumaliza mgogoro baina yake na wafanyakazi ambao ni raia wa India katika meza ya mazungumzo.

Hayo yameelezwa na mmoja wa maafisa wa kampuni hiyo aliyetumwa na Mkurugenzi wa MeTL, Gulam Dewji kutoa ufafanuzi kwa Tanzania PANORAMA Blog kuhusu andishi lililowekwa kwenye mitandao ya kijamii likiwatahadhalisha raia wa India wote kuepuka kufanya kazi katika kampuni za MeTL.

Andiko hilo mtandaoni linaeleza kuwa Ubalozi wa India umekuwa ukipokea kwa mfululizo malalamiko ya wafanyaakazi wa Kampuni za MeTL kunyanyaswa na uongozi pamoja na mwajiri wao kuwafungulia kesi za kughushi mahakamani kiasi cha kusababisha wanafamilia wa wafanyakazi hao kulazimika kurejea India.

Kwamba Mwenyekiti wa Makampuni ya MeTl, Gulam Dewji na maafisa waandamizi wamekuwa wakiwafanya vitendo vya unyanyasaji na udhalilishaji wafanyakazi hao wanapofikisha malalamiko kwao.

Linahitishwa kwamba raia wote wa India wasikubali kuajiriwa na Kampuni za MeTL kutokana na mwenendo usiofaa wa viongozi wake wa juu.

Gulam

Alipoulizwa Mwenyekiti Gulam, kuhusu suala hilo kupitia simu yake ya kiganjani alisema aandikiwe maswali kwa maandishi ili ayajibu na alipoandikiwa, muda mfupi baadaye mtu mmoja mwenye asili ya kiasia alituma ujumbe kwa njia ya whatsapp akieleza kuwa ametumwa na Gulam kufikisha ujumbe kwa Tanzania PANORAMA Blog.

Ujumbe aliuotuma ulisomeka; ‘Bwana Dewji amezungumza na sisi na ametuhakikishia uwajibikaji wa menejimenti katika kulinda maslahi ya wafanyakazi. Tumekubaliana kuwa na mazungumzo ya kina, tungependa kutatua jambo hili kwa njia ya mazungumzo.’

Ujumbe mwingine chini ya huo aliuotuma ulisomeka; ‘leo hii mmelalamika mazingira ya watu wenu ila tusema ukweli pia mnawanyanyasa sana watanzania sema tu wanashindwa nani wa kuwasemea pia kutokana na hali za maisha yao ila mazingira ya ufanyaji kazi siyo.

Jitahidi za Tanzania PANORAMA Blog kuzungumza na Ubalozi wa India kuhusu suala hili zinaendelea.