Labna Salim Said, mwanafunzi wa kidato cha
tatu katika Shule ya Sekondari ya Bweni Wasichana ya St. Mary's iliyopo Mbezi
Makonde ambaye amepotea kwa zaidi ya mwezi mmoja sasa
NA CHARLES MULLINDA
WAZAZI wa mwanafunzi msichana, Labna Salim Said wa
Shule ya Sekondari ya Bweni Wasichana ya St. Mary’s ambaye alitoroka shuleni
usiku na kutokomea kusikojulikana wameeleza kuwa wanahofia mtoto wao kauawa.
Zephania Maduhu ambaye ni mjomba wa mwanafunzi huyo
anayesoma kidato cha tatu na pia mlezi wake, ameieleza Tanzania PANORAMA kuwa
mtoto wake alipotea tangu Oktoba 4, 2020 akiwa chini ya uangalizi wa shule na
hadi sasa hajapatikana.
Alisema taarifa za kupotea kwa mwanafunzi huyo
zilitolewa Oktoba 8, 2020 na matron wake aliyemtaja kwa jina la Sarah Murra
aliyempigia simu mama mzazi wa mwanafunzi huyo akiulizia kama ameishafika
nyumbani.
“Huyo mtoto ninamlea mimi, ninamlipia ada ya shule
mimi, ni mtoto wa dada yangu, anasoma St. Mary’s Mbezi Makonde. Oktoba 8, mwaka
huu, matron wake anaitwa Sarah Murra, alimpigia simu mama yake, yaani dada
yangu akimuuliza kama Labna kafika nyumbani.
“Dada yangu ambaye wakati huo alikuwa mkoani
Shinyanga akashangaa akamuuliza amefikaje nyumbani wakati yupo shule au shule
zimefungwa ghafla tena? Yule matron akamjibu ametoroka shuleni tangu Oktoba 4,
2020 hivyo alikuwa anataka kujua kama yupo nyumbani, dada akamwambia yeye yupo
mkoani Shinyanga na anajua mtoto wake yupo shule.
“Aliporudi kutoka safari Shinyanga akakuta mtoto
hajapatikana na shule haijatoa taarifa polisi yaani hata wasiwasi hawana.
Ikabidi yeye aende kutoa ripoti Kituo cha Polisi cha Stakishari, waliniponipa
taarifa mimi nikafunga safari mpaka shuleni.
“Pale shuleni nikamkuta mkuu wa shule anaitwa Reca
Ntipoo, akanijibu mtoto alitoroka shule usiku hajarudi na hawajui alipokwenda.
Nikauliza kama wamefanya jitihada zozote za kumtafuta na kama wameisha ripoti
polisi akasema hilo ni jukumu letu wazazi.
“Sasa hapo nikakasirika nikamuuliza mtoto
tumemkabidhi shule na ada tumelipa kumbe katoroka zaidi ya mwezi hata taarifa
polisi hawajatoa, hapo akajibu labda tukamtafuta kwenye vijiwe vyao vya usiku
wakitoroka huwa wanakwenda huko ambako wanafunzi wenzake wanavijua, akamuuita
mwanafunzi mmoja kweli akatuelekeza huko wanakokwenda usiku.
“Nilikuwa na rafiki yangu alinisindikiza tukaenda
kumtafuta huko hatukumpata, hatukuwa na jinsi ikatubidi sisi tukatoe taarifa
nyingine kituo cha Polisi Goba na polisi tulipowaelezea nao walishangaa
kweli kweli.
“Sasa RB tunayo ni STK/RB/10714/2020 na mpelelezi wa
shauri hilo ni Afande Gwake Mwakapande. Sidhani kama yupo hai sisi tunaamini
ameishakufa lakini uongozi wa shule hii ndiyo umetuulia mtoto wetu. Polisi
wanajua sasa sijui kama wameishawauliza au bado,” alisema Maduhu.
Alipoulizwakwa simu yake ya kiganjani, Afande
Mwakapande kama analifahamu suala hilo alisema ni kweli faili la uchunguzi la
kupotea kwa mtoto huyo analishughulikia yeye lakini yuko kwa kinyozi ananyoa
nywele hivyo akimaliza atapiga simu kuelezea alipofikia katika upelelezi
wake, jambo ambalo hakulitekeleza.
Mwisho.

No comments:
Post a Comment