banner

Monday, November 9, 2020

WANAFUNZI WASICHANA ST MARY’S WATOROKA USIKU, MMOJA ATOWEKA

 


NA CHARLES MULLINDA

WANAFUNZI wasichana wa Shule ya Sekondari ya St. Mary’s iliyoko Mbezi Makonde Jijini Dar es Salaam wametoroka shuleni usiku kwenda mahali kusikojulikana huku mmoja akitoweka moja kwa moja.

Taarifa za uhakika zilizoifikia Tanzania PANORAMA Blog zimeeleza kuwa wanafunzi hao walitoroka shuleni wakiwa kundi na kurejea alfajili huko mmoja wao akitokomea mahali kusikojulikana.

Uchunguzi wa Tanzania PANORAMA umebaini kuwa tukio hilo lilitokea mwezi uliopita na mwanafunzi aliyetoweka anasoma kidato cha tatu lakini uongozi wa shule na bodi ya shule wamekuwa wakifanya jitihada kubwa za kuficha tukio hilo na hajawatoa taarifa polisi za kutoweka kwa mwanafunzi huyo.

Mwenyekiti wa bodi ya shule hiyo, Dallas Mhoja alipoulizwa na Tanzania PANORAMA alisema kupotea kwa mwanafunzi huyo akiwa shuleni kunamuhusu mkuu wa shule, siyo bodi.

“Wewe vipi bwana, unajua kuwa mimi ni mwenyekiti wa bodi? Sasa kupotea kwa mwanafunzi kunanihusu nini mimi? Mpigie mkuu wa shule muulize huyo ndiye anakaa na hao watoto,. Mimi nashughulika na mambo makubwa ya shule siyo suala na mtoto mmoja kupotea,” alisema Dallas.

Alipoelezwa kuwa taarifa za mwanafunzi kupotea akiwa mikononi mwa uongozi wa shule na shule kutotoa taarifa polisi kwa zaidi ya mwezi mmoja ni kubwa ikizingatiwa mpaka sasa hajapatikana alisema akipata nafasi atafuatilia kwa mwalimu.



Tanzania PANORAMA ilimweleza Mhoja kuwa imefanya uchunguzi wa kina kuhusu kupotea kwa mwanafunzi huyo na inazo taarifa kuwa suala hilo limekwishafikishwa kwake lakini hajachukua hatua yoyote alisisitiza kuwa kwa wadhfa wake wa mwenyekiti wa bodi hastahili kufuatilia mambo ya wasichana wanaotoroka shule usiku na kupotelea wanakokujua hivyo aulizwe mkuu wa shule.

“Aisee we mwandishi mbona una maswali ya kuudhi? Nakwambia hayanihusu mambo wewe umeng’ang’ania kunibana tu unataka nini? Mwenyekiti wa bodi na kupotea kwa mtoto mmoja wanahusianaje?

“ Mimi ni mwenyekiti wa bodi sihusika na kuangalia watoto shuleni tena wanaotoroka shuleni usiku kwenda kwenye mambo yao? Halafu wananogewa huko hawarudi? Muulize mkuu wa shule ndiye anayehusika na malezi ya watoto,” alisema Mhoja.

Alipotafutwa mkuu wa shule kupitia simu yake ya kiganjani, iliita bila kupokelewa.  

No comments:

Post a Comment