banner

Thursday, November 19, 2020

FISI MADOA MNYAMA ANAYEWEKA MIPAKA YA HIMAYA YAKE KWA KINYESI CHAKE


 NA ERNEST SITTA

MAISHA ya mnyama Fisi yana mengi ya kuvutia kuyajua ambayo yanamsaidia binadamu kutambua umuhimu wa mnyama huyu katika uso wa dunia.

Fisi wamegawanyika katika makundi manne ambayo ni Fisi Madoa, Fisi Miraba, Fisi Kahawia na Fisi Aardwolf na asili yao ni familia inayofahamika kwa jina la kitaalamu la Hyenidae.

Taungalie kwanza maisha ya Fisi Madoa, mnyama anayetokea kwenye familia ya Hyenidae.

Kwa kawaida Fisi wote ni wanyama wanatokea katika kundi la wanyama walao nyama.

Fisi madoa ana urefu wa sentimita 77 kutoka mkiani hadi kwenye mabega akiwa amesimama.

Uzito wake ni kilo 63 kwa dume na jike ni kilo 68, hivyo jike ni mkubwa kuliko dume.



Fisi madoa anabeba mimba kwa muda wa miezi mitatu na nusu na huzaa watoto kuanzia mmoja mpaka wanne. Umri wake wa kuishi ni miaka 50.

Aina hii ya wanyama wanapendelea kukaa kwenye mashimo au mapango katika familia inayoongozwa na mtawala ambaye ni jike na kufuatiwa na majike daraja mbalimbali za utawala katika familia.

Sehemu hizo za mapangoni hutumika kuishi na kulea watoto wa rika mbalimbali. Jinsia ya kike hukaa katika himaya waliyozaliwa maisha yao yote lakini Fisi madume baada ya kufikia miaka minne huanza kujiandaa kuondoka kwenye familia.

Fisi madume baada ya kutimiza miaka minne hutoka na kujiunga na familia nyingine.

Fisi hawa huweka mipaka ya himaya yake kwa kutumia utomvu wenye harufu kali kutoka kwenye tezi lililomo ndani ya sehemu ya kujisaidia haja kubwa.



Mnyama huyu ni mahiri wa kuwinda, ana uvumilivu na nguvu nyingi za shingo. Umbo la fuvu la kichwa lina meno makali yenye uwezo wa kutafuna hata mifupa.

Kinyesi cha Fisi Madoa kina rangi nyeupe kama chaki au chokaa.

 Jike mtawala pamoja na watoto wake humiliki himaya na chochote kilichopo ndani ya eneo kama ni mnyama wameshirikiana kuua ndani ya himaya wa kwanza kula ni jike mtawala pamoja watoto wake, wakishatosheka ndipo Fisi wengine watafuatia kwa kuzingatia daraja mbalimbali au rika.

Chakula kisipotosha familia nzima ya Fisi wawindaji au wavizia mizoga husafiri kwenda mbali muda wa siku moja au mbili kutafuta chakula kingine cha kutosheleza kundi zima na kurudi kuwatapikia watoto wao.



Watoto wa Fisi Madoa waliozaliwa na jike mtawala wanakuwa na bahati ya kuendelea kutawala, vivyo hivyo wanaozaliwa na mama ambaye yupo daraja la chini huendelea  kutawaliwa na hawapewi kipaumbele hasa katika masuala ya chakula.

Katika jamii zetu za kiafrika hasa za Kusini mwa Jangwa la Sahara, Fisi huhusishwa na imani za kishirikina na hasa wanaposikika kwa milio tofauti karibia na mazingira ya makazi ya watu.

Lakini kiuhalisia sauti za Fisi huashiria  kuomba msaada endapo mmoja ameona mawindo, mzoga au msaada kama kuna adui.

Fisi ni muhimu sana katika mapori tengefu na hifadhi za taifa. Mfano katika  mfumo wa kiikolojia wa Serengeti-Maasai Mara Kenya unajumuisha wanyama mbalimbali wakiwemo wanyama wahamiaji - Nyumbu zaidi ya milioni mbili ambao kila mwaka wanahama kutoka sehemu wanapozaa na kuenda sehemu wasipozaa kwa ajili ya mabadiliko ya hali ya hewa, kutafuta chakula, mazingira na maji.

Fisi Madoa na jamii nyingine za Fisi huitwa bwana afya katika hifadhi kwa sababu ya kula idadi kubwa ya mizoga ingawa kuna wanyama wengine kama Simba, Chui, Mbweha na ndege aina ya Tumbusi ambao nao hula mizoga hiyo.

Hivyo bila Fsi kula mizoga hiyo kwa idadi kubwa, hifadhi zingekuwa zinanuka na kukatisha wageni kuzitembelea jambo ambalo lingechangia kupoteza mapato yatokanayo na utalii.

ERNEST SITTA NI MTAALAMU WA ELIMU YA WANYAMA NA MIMEA AMBAYE AMEFANYA KAZI NA TAFITI MBALIMBALI KATIKA HIFADHI TOFAUTI TOFAUTI HAPA NCHINI KWA ZAIDI YA MIAKA 10

No comments:

Post a Comment