NA MWANDISHI WETU
IMEBAINIKA kuwa baadhi ya
wafanyabiashara jijini Dar es Salaam wanaendelea kutengeneza mifuko ya
plastiki iliyopigwa marufuku na serikali kutokana na kuwa chanzo cha uharibifu
wa mazingira.
Uchunguzi waTanzania PANORAMA umebaini kuwepo kwa viwanda hivyo
katika makazi ya watu yaliyo nje kidogo ya jiji huku ikiwa haina vibali vyovyote
vya uzalishaji wa vifungashio.
Aidha, maeneo vilipo viwanda hivyo kuna walinzi ambao hukaa
umbali wa hatua 30 hadi 50 ambao kazi yao ni kuangalia kama kuna watu wanaofutilia
uzalishaji au kuchunguza eneo la kiwanda kisha hutoa taarifa kwa walio
kiwandani kusimamisha uzalishaji na kufunga kiwanda.
Uchunguzi wa kina wa Tanzania PANORAMA umebaini moja ya kiwanda
cha mifuko ya plaskiti kipo eneo la Mbezi Kifuru kwa Richard ambacho mmiliki
wake hafiki eneo la kiwanda bali ameweka walinzi wanaompatia taarifa za kila
mtu anayefika kiwanda hapo kwa kumpigia simu.
Wakizungumza na Tanzania PANORAMA, wafanyakazi wa kiwanda
hicho walisema wanajua wanafanya kazi kwa uficho na katika mazingira magumu
lakini wanalazimika kufanya kutokana na ugumu wa maisha.
Msimamizi mkuu wa kiwanda hicho ambaye alikataa
kujitambulisha jina lake alieleza kuwa kazi yake ni kuangalia usalama na kumpa
taarifa bosi wake ambaye pia ni mjomba wake kuhusu wageni wanaofika kiwanda
hapo.
“Kiukweli mimi ni msimamizi ila mjomba ndiye anajua kila
kitu mje wakati mwingine atakapokuwa hapa.
Najua hatuna vibali na tunaendesha kiwanda kinyume cha taratibu lakini mkiongea
na mjomba yeye anajua kila kitu,” alisema.
Mmiliki wa kiwanda hicho aliyefamika kwa jina la Ali Mbonde
alipoongea na Tanzania PANORAMA kwa simu alisema anajua kila kitu lakini jambo
hilo linahitaji mazungumzo badala ya kuandikwa kwa sababu litasababisha
usumbufu usiokuwa wa lazima.
Tanzania PANORAMA inaendelea na uchunguzi wa sakata hili.

No comments:
Post a Comment