banner

Friday, November 20, 2020

SERIKALI YAANZA MSAKO MKALI MWANAFUNZI ALIYEPOTEA ST MARY'S

 

NA MWANDISHI WETU

HATIMAYE serikali imeanzisha msako mkali wa mwanafunzi Labna Salim Said wa kidato cha tatu katika Shule ya Sekondari ya Bweni ya St Mary's ambaye amepotea tangu Oktoba 4, 2020 akiwa shuleni.

Taarifa za uhakika zilizoifikia Tanzania PANORAMA Blog zimeeeza kuwa, msako huo umeanza jana baada ya kufanyika kwa kikao cha ulinzi na usalama cha Wilaya ya Kinondoni kilichoongozwa na Mkuu wa wilaya hiyo, Daniel Chongolo.

Chongolo ameithibitishia Tanzania PANORAMA  kuitisha na kuongoza kikao hicho na kueleza kuwa serikali imeanza kuchunguza mazingira ya tukio la kupotea kwa mwanafunzi huyo akiwa shuleni kwa kuunda kikosi maalumu kinachojumuisha vyombo vya ulinzi na usalama.

Hata hivyo, Chongolo alisema hayuko katika nafasi nzuri ya kulizunguzia suala hilo kwa sababu kuhofia kuharibu mwenendo wa uchunguzi wa timu yake aliyoiunda.

Akizungumzia hatua hiyo ya serikali kujitosa rasmi kwenye sakata la kupotea kwa mwanafunz Labna, Afisa Elimu Sekondari wa Wilaya ya Kinondoni, Joseph Kapere Chongolo aliitisha kikao cha kamati ya ulinzi na usalama ofisini kwake jana mchana baada ya kupokea malalamiko ya wazazi wa mtoto huyo kupotea akiwa shuleni.

Kapere alisema katika kikao hicho kilichohudhuliwa pia na wazazi wa mtoto huyo, Chongolo aliunda kamati ya watu  wanne kumsaka mtoto Labna popote alipo na kuchunguza mwenendo mzima wa tukio la  kupotea kwake.

"Hili tukio ni la aina yake lakini tunasikitika kuwa limechelewa kutufikia, hata mkuu wa wilaya kafahamu jana baada ya wazazi kumfikishia kesi hiyo. Hizo shule zipo chini yangu mimi ndiyo nashughulika nazo.

"Sasa mkuu wa wilaya aliitisha kamati ya ulinzi ya usalama na ameteua kikosi cha watu wanne kumsaka mtoto huyo.

"Walioteuliwa kwenye kikosi hicho ni viongozi waandamizi wakiwemo kutoka ofisi ya Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Kipolisi wa Kinondoni, ofisi ya Afisa Usalama wa Wilaya ya Kinondoni, mimi mwenyewe Afisa Elimu Sekondari Wilaya ya Kinondoni," alisema Kapere.

Mwanafunzi msichana, Labna wa Shule ya Sekondari ya Bweni ya St. Mary’s alitoroka shuleni usiku na kutokomea kusikojulikana na hadi sasa hajapatikana.

Labna alitoroka Oktoba 4, 2020 akiwa chini ya uangalizi wa shule lakini taarifa za kupotea kwake zilitolewa Oktoba 8, 2020 na matron wake Sarah Murra aliyempigia simu mama mzazi wa Labna akiulizia kama ameishafika nyumbani.

Katika hatua ya kushangaza, uongozi wa Shule ya Sekondari ya St Mary’s haukutoa taarifa polisi kuhusu kupotea kwa mwanafunzi huyo na badala yake wazazi ndiyo walioripoti tukio la mtoto wao kupotea akiwa shuleni.

 

No comments:

Post a Comment