banner

Friday, November 20, 2020

MSAKO WA LABNA WA ST MARY'S WAIBUA MADUDU YA KUTISHA, SHAMBA LA BANGI LABAINIKA NYUMBANI KWA KAMISHNA

 


NA MWANDISHI WETU

TIMU ya maafisa wanne waandamizi wa serikali iliyoundwa na Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Daniel Chongolo kumsaka mwanafunzi wa kidato cha tatu wa Shule ya Sekondari ya Bweni ya St Mary's, aliyepotea tangu Oktoba 4, 2020 imebaini kuwa shule hiyo imepungukiwa sifa zinazostahili kisheria.

Afisa Elimu Sekondari ya Wilaya ya Kinondoni, Joseph Kapere ameyasema hayo alipokuwa akielezea mwenendo wa msako na uchunguzi wa mazingira ya kutoweka kwa mwanafunzi Labna unaofanywa na timu iliyoundwa na Chongolo.



Kapere alisema katika uchunguzi huo ulioanza jana  kwa kumuhoji Mkuu wa Shule ambaye alieleza kuwa Labna aliwaambia walimu hataki shule na alitoroka akaenda kwa rafiki yake ya kiume wakawa wanaishi pamoja.

"Tunafanya uchunguzi kwa umakini sana. Tumeishamuhoji Mkuu wa Shule na yeye ametueleza kuwa huyo mtoto alikwishawambia walimu kuwa hataki shule na aliondoka shuleni kwa kutoroka.

"Mkuu wa Shule alituambia kuwa motto alitoroka shuleni kwa kuruka ukuta usiku akisaidiwa na wanafunzi wenzake wavulana wawili, akaenda kwa boy friend wake wakaanza kuishi pamoja huko,” Kapere alimkariri mkuu wa shule.

Alisema mkuu huyo wa shule aliipeleka timu ya serikali nyumba aliyokuwa akiishi Labna na mpenzi wake baada ya kutoroka shule lakini waliwakosa na badala yake walikuta wavulana saba wakiwa wanavuta bangi.

"Mkuu wa shule anapajua alipotorokea mtoto huyo na alitupeleka kwenye hiyo nyumba. Ni nyumba ya Kamishna Mstaafu wa Magereza ambayo wanaishi watoto wake wawili lakini hapo hatukumta Labna wala boy friend wake, tulikuta vijana saba waliokuwa wanavuta bangi na nyumba nzima ilikuwa imetapakaa misokoto ya bangi.

"Kwa kweli ni hali ya kutisha sana kwa vijana wetu. Walituambia ni kweli Labna alipotoroka shule alikuwa akiishi hapo na boy friend wake na alikuwa mama wa nyumbani kwani alikuwa akiwapikia na kufanya usafi wa nyumba lakini baada ya muda kidogo aliondoka.

"Boy friend wake naye hatukumkuta, wale vijana wavuta bangi walisema anasoma chuo CBE na anaishi hostel sasa tumepeleka makachero akakamatwe huko.

“Lakini hiyo nyumba baada ya kuichunguza kwa sababu ina uzio mkubwa sana tulikuta shamba la bangi humo ndani. Yaani bangi inalimwa humo humo nyumbani kwa Kamishna wa Magereza wanavuna wanavuta hao vijana.

"Basi wale vijana tuliwachukua hadi polisi wamelala huko kwa ajili ya uchunguzi zaidi na taratibu nyingine zitafuata," alisema Kapere.

Alipoulizwa iwapo timu hiyo imebaini ni kwanini Mkuu wa Shule baada ya kuambiwa na Labna kuwa hataki shule hakuwapa taarifa wazazi na hata alipotoroka uongozi wa shule ulikaa kimywa wala haukutoa ripoti polisi, alisema mwalimu huyo amekiri kuwa yeye na wenzake walikosea.

Tanzania PANORAMA lilimuuliza pia Kapere kama timu ya serikali imebaini ni kwanini Mkuu wa Shule baada ya kubaini mwanafunzi wake ametoroka na alikuwa akiishi na mwanaume nje ya shule hakuchukua hatua za kutoa taarifa kwa wazazi na polisi ili wote wawili wakamatwe kwa kuzingatia mwanafunzi huyo wazazi wake walimkabidhi kwa uongozi wa shule, Kapere alisema swali hilo ni zuri na watamuuliza Mkuu wa Shule.

"Timu yetu ina polisi, hata nyumba ya  kamishna tuliivamia tukiwa na polisi. Polisi waliizingira kisha wakaingia ndani ndiyo wakakuta lile shamba la bangi na ile misokoto. Lakini Mwalimu anajitetea yeye ni mgemi na tabia ya watoto kutoroka usiku wakarudi alfajili aliikuta. Lakini pia mkuu wa shule alituambia kuwa awali yeye, polisi na wajomba wa huyo wa mtoto walikwenda hadi kwenye hiyo nyumba kumsaka lakini polisi na wajombe hawakuingia ndani, waliishia nje.  

"Sasa hata Labna alipotoroka Mwalimu amesema mwenyewe alijua ndiyo kawaida yao atarudu lakini kwa bahati mbaya yeye hakurudi, akahamia kabisa kwa huyo boy friend wake.

"Uchunguzi wetu sasa pale shuleni imebaini kuwa ile shule haifai, imepungukiwa sifa stahiki za kuitwa shule. Kwanza ni chafu sana, haina walinzi wa kutosha na hata ukuta wake haufai," alisema Kapere.

Alisema anaamini mtoto huyo yupo hai na atapatikana katika msako unaoendelea.

Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Daniel Chongolo alipoulizwa jana alisema yupo msibani hivyo hayupo katika nafasi kuzungumza.

Labna, mwanafunzi wa Shule ya Sekondari ya St. Mary’s iliyoko Mbezi Makonde Jijini Dar es Salaam alitoweka shuleni tangu Oktoba 4, 2020 lakini tukio  la kutoweka kwake halikuripotiwa polisi na uongozi wa shule.

No comments:

Post a Comment