banner

Wednesday, November 18, 2020

WAFANYAKAZI MR CLEAN WAMLILIA JPM

 


NA MWANDISHI WETU

WAFANYAKAZI wa Kampuni ya udobi ya Mr Clean ya jijini Dar es Salaam wamemuomba Rais John Magufuli atakapoteua Baraza la Mawaziri, amuelekeze Waziri wa Kazi, Vijana na Ajira kutafuta suluhu ya kudumu kwa watanzania wanaofanyishwa kazi muda mrefu bila kupewa mikataba ya kazi.

Wakizungumza na Tanzania PANORAMA Blog hivi karibuni kuhusu kutopatiwa mikataba ya kazi na mwajiri wao kwa muda mrefu, walisema wao ni sehemu tu ya watanzania wengi wanaonyanyasika sehemu za kazi na wameamua kupaza sauti zao ili Rais ambaye amekuwa akiwatetea wanyonge awasikie.

"Tunaamini Rais akisikia kilio chetu atatusidia kutatua hii kero yetu. Sisi tumefanya kazi kwa zaidi ya mwaka mmoja sasa katika Kampuni ya Udobi ya Mr Clean lakini mwajiri wetu hajatupa mikataba ya kazi. Kila tukiomba anatishia kutufukuza kazi.

"Tunapenda kufanya kazi kwa sababu bila kazi kwa maisha ya sasa mtu unakufa njaa na tunafurahi wanapojitokeza wawekezaji na wafanyabiashara wenye makampuni wanaotoa nafasi za kazi lakini mazingira ya kazi ni magumu mno.

"Mtu unakuwa kibarua mwaka mzima, miaka miwili, kazi yenyewe ngumu maana tunafua nguo kwa madawa ambayo hatujui yana kemikali za aina gani. Matokeo yake ukiugua unaondolewa kazini.

"Hatuna pensheni ya aina yoyote, hatuna Bima ya Afya, tunafua nguo kwa kutumia madawa, tunalipwa mkononi kama vibarua serikali haipati kodi yoyote ambayo ingetokana na mishahara yetu. Tunaomba kilio chetu kimfikie rais atuletee waziri wa kutafuta ufumbuzi wa matatizo yetu wafanyakazi wa sekta binafsi," alisema mmoja wa wafanyakazi hao.

Alipoulizwa Mkurugenzi wa Kampuni ya Mr Clean, Ravi Shankar kuhusu malalamiko ya wafanyakazi hao alisema suala hilo aulizwe msemaji wa Kampuni yake aliyemtaja kwa jina la Morris Ngonyani.

 

Alipoulizwa Ngonyani alisema yeye siyo msemaji wa kampuni ya Mr Clean bali mwenye Kampuni akiwa na hisa asilimia 90 na huyo alielekeza aulizwe ni mfanyakazi wake ambaye hana ruhusa ya kuzungumza lolote kwa sababu amemuweka kiwandani hapo kama msimamizi wa wafanyakazi tu.

Akijibu malalamiko ya wafanyakazi hao alisema walikuwa vibarua ambao kwa sasa wameishaondolewa kazini na kwamba Kampuni ya Mr Clean imebaki na wafanyakazi saba tu nchi nzima kutokana na mwenendo mgumu wa biashara.

No comments:

Post a Comment