banner

Monday, November 30, 2020

UTATA UJENZI WA SOKO JIPYA TANDALE

 

 

Ujenzi wa Soko la Tandale ulipokuwa umefikia mwezi Agosti, mwaka huu

NA MWANDISHI WETU


WAKATI Serikali ya Awamu ya Tano ikiwa imeelekeza nguvu kubwa kwenye ujenzi wa miundombinu, shule, hospitali na masoko, jitihada hizo zimeanza kuingia doa baada ya kusimama kwa ujenzi wa soko jipya la Tandale.

Katikati ya hilo, msimamo wa Serikali ya Awamu ya Tano wa kutoa taarifa zinazohusu shughuli za maendeleo bila ukiritimba, zinazofanywa na serikali ili kutoa fursa kwa wananchi kujua miradi inayotekelezwa kwa kodi zao, nao unaonekana kuingia doa baada ya mkandarasi anajenga soko la Tandale, Namis Corporate Ltd kuweka zuio la upatikanaji wa taarifa hizo.

Haya yamebainika baada ya Tanzania PANORAMA Blog kufika eneo la ujenzi wa soko jipya la Tandale mapema wiki iliyopita kufuatilia maendeleo ya ujenzi wa mradi huo baada ya kudokezwa na baadhi ya wafanyakazi kuwa umesimama kutokana na ukosefu wa fedha.

Tanzania PANORAMA Blog baada ya kufika katika eneo la mradi, lilishuhudia mafundi wakiwa wamekaa kivulini huku ujenzi ukiwa umesimama na baada ya kuwahoji baadhi yao walisema wanasubiri kulipwa fedha zao waondoke kwa sababu mahali hapo hakuna kazi tena.

"Bora umekuja na sijui umeingiaje huku maana hamruhusiwi nyie kuingia humu na wakikuona watakugawana. Hapa hakuna kazi kama unavyoona ujenzi umesimama hakuna fedha. Tunasikia bosi hajalipwa huko serikalini ndiyo bado anafuatilia malipo lakini sisi tumeambiwa tukiulizwa tuseme tuna tatizo la simenti ambalo ni tatizo la kitaifa kwa sasa.

" Kama unaweza twende tukupeleke kwa msimamizi wetu ukamuhoji ila uwe unajiamini labda watatulipa. Sisi tunasubiri akipata pesa kutoka serikalini akitulipa ndiyo basi tunatafuta kazi sehemu nyingine maana hapa, wiki hii mnafanya kazi wiki ijayo hakuna kazi sasa tunajiuliza hiyo serikali inatoa hela kwa wiki?" alisema mmoja wa mafundi hao.

Msimamizi wa mradi alipofikiwa na Tanzania PANORAMA Blog na kuulizwa, kwanza alielekeza afuatwe ofisini ambako alichukua simu na kuwasiliana na Makao Makuu ya kampuni yake kisha alisema;

"Unasema kuna wenzako kwenye gari wanakusubiri .... Umesema hujapiga picha.... Hili ni eneo la ‘site,’ mtu yoyote haruhusiwi kuingia humu bila kibali cha makao Makuu, awe Mkuu wa Mkoa, awe Waziri anapotaka kuja hapa ni lazima awe na kibali kwa sababu anaweza kuangukiwa na kitu kizito kama nondo au ubao ukaumia.

" Sasa nimeongea na Makao Makuu nadhani umeona naongea na simu, kama una maswali nenda huko watakujibu na kama unataka kutembelea hapa uje na kibali cha maandishi kutoka makao makuu.

"Tena tumekuheshimu sana kwa sababu umeingia eneo ambalo haliruhusiwi ila kwa vile una wenzako nje njoo nikupitishe njia salama usije ukajikwaa halafu mkaanza kutunga uongo, " alisema.

Tanzania PANORAMA Blog lilifika Makao Makuu ya Kampuni ya Namis Corporate Ltd yaliyopo Mbezi Africana kwa ajili ya kupata maelezo ya kasimama kwa ujenzi wa soko la Tandale na kuelezwa kuwa mkataba wa ujenzi una kipengele kinachozuia kutoa taarifa yoyote ya mwenendo wa ujenzi isipokuwa kwa kibali cha Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni.

Akizungumza kuhusu katazo hilo alilodai lipo kwenye mkataba huo, Meneja Mradi aliyejitambulisha kwa jina la James Msumali alisema changamoto zinazowakabili katika ujenzi huo anaweza kuzizungumzia iwapo atapata kibali cha maandishi kutoka kwa Mkurugenzi wa Manispaa.

"Mimi ndiyo meneja mradi na ndiye ninayeweza kuzungumza, bosi unayetaka kuonana naye hayupo. Utaratibu upo hivi, mkataba wetu una kipengele kinachoelekeza kuwa taarifa yoyote ya mradi haiwezi kutolewa mpaka kwa kibali cha Mkurugenzi.

"Tena kibali cha maandishi au anipigie simu yeye mwenyewe aseme nitoe taarifa kwako. Kwa hiyo nenda Manispaa kamtafute Mkurugenzi muombe kibali au mwambie anipigie simu ndiyo uje nikueleze hicho unachotafuta," alisema Msumali.



Alipofikiwa na kuelezwa hali hiyo, Mkurugenzi wa Manispaa ya Kinondoni, Aron Kagulimjuli alihoji ni kwanini Tanzania PANORAMA Blog linafuatilia mradi wa ujenzi wa soko la Tandale wenye kelele nyingi badala ya  kuandika maendeleo ya ujenzi wa jengo la Ghorofa la Ofisi ya Mkurugenzi wa Manispaa ya Kinondoni au ujenzi wa bwawa na kufua umeme la Mwalimu Nyerere.

"Kwanini Ujenzi wa Soko la Tandale ambalo lina kelele nyingi saaana. Kwanini huandiki kuhusu ujenzi wa ghorofa hiyo hapo sasa umefikia ghorofa ya nne, kwanini huandiki kuhusu ujenzi wa bwawa la Mwalimu Nyerere? Kwanini huandiki kuhusu ujenzi wa Reli ya Kisasa, kwanini huandiki kuhusu stendi Mpya ya mabasi ya Dar es Salaam?

" Lakini nimeitwa mahali sasa siwezi kuwasikiliza kwa sababu nimeitwa na wakubwa. Njooni kesho," alisema Kagurumjuli.

Alipotafutwa siku iliyofuata alisema kusimama kwa mradi huo kunachangiwa na sababu nyingi ikiwemo ya kukosekana kwa saruji. Alipoulizwa kuhusu zuio la kuandika habari za soko hilo alisema halitambui isipokuwa mwananchi anapaswa kufuata utaratibu kuingia katika miradi ya aina hiyo.

"Hilo zuio silijui na nitoe barua kwa mwandishi kwenda kuandika habari kutoka lini hiyo. Hao watakuwa na yao lakini wananchi wanaruhusiwa kuingia kwenye miradi ya aina hiyo kwa kufuata utaratibu maalumu ulioandaliwa na (project manager) Meneja mradi," alisema Kagurumjuli.

Alipotafutwa Mkurugenzi Mtendaji wa Namis Corporate Ltd, Thomas Uiso alikataa kuzungumza lolote na kueleza aulizwe meneja mradi, Msumali.

Tanzania PANORAMA inaendelea kufuatilia sakata hilo.

 

JWTZ, TISS KUOMBWA KUMSAKA MWANAFUNZI ALIYEPOTEA ST MARY’S

 


NA MWANDISHI WETU

JESHI la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) na Idara ya Usalama wa Taifa (TISS) wataombwa kumsaka mwanafunzi aliyekuwa akisoma Shule ya Sekondari ya Bweni ya St. Mary’s iliyoko Mbezi Makonde, Labna Said Salim ambaye ametoweka tangu Oktoba 4, 2020.

Taarifa iliyotolewa na Afisa Elimu Sekondari wa Wilaya ya Kinondoni, Joseph Kapere kwa Tanzania PANORAMA Blog leo, imeeleza kuwa taasisi hizo zitaombwa kusaidia kumsaka mwanafunzi huyo popote alipo baada ya jitihada za Jeshi la Polisi kumsaka kushindwa kuzaa matunda.

Kapere ambaye alikuwa akizungumzia mwenendo wa uchunguzi wa timu ya maafisa wanne wa serikali iliyoundwa na Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Daniel Chongolo kuchunguza mazingira ya kutoweka kwa mwanafunzi huyo na kumsaka mahali alipo, ameeleza kuwa tume hiyo imekwishamkamata kijana anayedaiwa kuishi na mwanafunzi huyo baada ya kutoroka shuleni na sasa inasubiri wanafunzi wa kidato cha nne wamalize mitihani ya taifa ili iweze kuchukua hatua zaidi.

Timu hiyo inayomsaka mwanafunzi huyo inaundwa na Kamanda wa Polisi wa Wilaya ya Kinondoni, Afisa Usdalama wa Wilaya ya Kinondoni, Afisa Elimu Sekondari wa Wilaya ya Kinondoni na Mdhibiti Ubora wa Elimu Kanda.

“Uchunguzi wetu unaendelea lakini hatufanikiwa kumpata huyo mtoto. Tiumekwishamkamata na kumuhoji kijana ambaye inadaiwa kuwa yule mtoto alitorokea kwake, anakiri kwamba ni kweli alikwenda chumbani kwake lakini huwa anakwenda mara kwa mara na marafiki zake na kwamba aliondoka akamuacha hapo chumbani akiwa na marafiki zake.

“Lakini wale marafiki zake saba tuliowakuta nyumbani kwa baba yake mahali ambako anaishi huyo kijana wakiwa wanavuta bangi wameeleza kuwa ni kweli huyo mtoto alipotoroka shule ule usiku alikwenda kwa huyo kijana wakawa wote kabla ya kutoweka kusikojulikana,

“Na wale waliomsindikiza kwenda kwenye hiyo nyumba ambao ni wanafunzi wenzake nao tuimewahoji na wanakiri kuwa mtoto Labna alikuwa na uhusiano wa kimapenzi na huyo kijana na kwamba siku hiyo walimsindikiza akaenda kwake.

“Sasa unajua wanafunzi wengi wa kidato cha nne wako kwenye mitahani, tunasubiri jumatano wamalize ili tuiwakutanishe pamoja wote tuliowahoji watueleze kwa pamoja ndipo tuchukua hatua zaidi,” alisema Kapere.

Alipoulizwa hatua zitakazochikuliwa na timu hiyo baada ya kukamilisha uchunguzi wake alisema itaandika taarifa itakayoipeleka kwa Mkuu wa Wilaya kwa ajili ya kuchukua hatua zaidi lakini itaomba Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) na Idara ya Usalama wa Taifa (TISS) vialikwe kusaidia kumsaka mwanafunzi huyo kutokana na jeshi la polisi kutopata mafanikio.

“Sisi tutaandika taarifa yetu na tumeishaanza kuandika, tutaeleza upungufu wote tulioubaini kwenye hiyo shule na tutatoa mapendekezo tutapeleka kwa mkuu wa wilaya ambaye ndiye aliyeunda timu hii. Lakini niseme tu moja kwa moja katika mapendekezo yetu tutashauri TISS na JWTZ waalikwe kumsaka huyu mtoto kwasababu nadhani polisi wanahitaji msaada maana mpaka sasa hawajafanikiwa,” alisema Kapere.



Mwanafunzi Labna alitoweka shuleni Oktoba 4, 2020 na taarifa za awali zilieleza kuwa alitoroka akiwa na wafunzi wanzake kwenda kwenye maeneo ya starehe na kutokomea moja kwa moja.

Zephania Maduhu ambaye ni mjomba wa mwanafunzi huyo aliyekuwa akimlipia ada ya shule aliieleza Tanzania PANORAMA Blog kuwa ana wasiwasi mtoto wake ameuawa kwani tangu Oktoba 4, 2020 alipopotea akiwa chini ya uangalizi wa shule, taarifa za kupotea kwake zilitolewa Oktoba 8, 2020 na matron wake, Sarah Murra aliyempigia simu mama mzazi wa mwanafunzi huyo akiulizia kama ameishafika nyumbani jambo ambalo limekuwa liibua hisia zinazotia shaka kuhusu usalama wa mtoto huyo.

“Huyo mtoto ninamlea mimi, ninamlipia ada ya shule mimi, ni mtoto wa dada yangu, anasoma St. Mary’s, Mbezi Makonde. Oktoba 8, mwaka huu, matron wake anaitwa Sarah Murra, alimpigia simu mama yake, yaani dada yangu akimuuliza kama Labna kafika nyumbani.

 “Dada yangu ambaye wakati huo alikuwa mkoani Shinyanga akashangaa akamuuliza amefikaje nyumbani wakati yupo shule au shule zimefungwa ghafla tena? Yule matron akamjibu ametoroka shuleni tangu Oktoba 4, 2020 hivyo alikuwa anataka kujua kama yupo nyumbani, dada akamwambia yeye yupo mkoani Shinyanga na anajua mtoto wake yupo shule.

 “Aliporudi kutoka safari Shinyanga akakuta mtoto hajapatikana na shule haijatoa taarifa polisi yaani hata wasiwasi hawana. Ikabidi yeye aende kutoa ripoti Kituo cha Polisi cha Stakishari, waliponipa taarifa mimi nikafunga safari mpaka shuleni.

 “Pale shuleni nikamkuta mkuu wa shule anaitwa Reca Ntipoo, akanijibu mtoto alitoroka shule usiku hajarudi na hawajui alipokwenda. Nikauliza kama wamefanya jitihada zozote za kumtafuta na kama wameisha ripoti polisi akasema hilo ni jukumu letu wazazi.

 “Sasa hapo nikakasirika nikamuuliza mtoto tumemkabidhi shule na ada tumelipa kumbe katoroka zaidi ya mwezi hata taarifa polisi hawajatoa, hapo akajibu labda tukamtafute kwenye vijiwe vyao vya usiku wakitoroka huwa wanakwenda huko ambako wanafunzi wenzake wanavijua, akamuita mwanafunzi mmoja kweli akatuelekeza huko wanakokwenda usiku.

 “Nilikuwa na rafiki yangu alinisindikiza tukaenda kumtafuta huko hatukumpata, hatukuwa na jinsi ikatubidi sisi tukatoe taarifa nyingine kituo cha Polisi Goba na polisi tulipowaelezea nao walishangaa  kweli kweli.

 “Sasa RB tunayo ni STK/RB/10714/2020 na mpelelezi wa shauri hilo ni Afande Gwake Mwakapande. Sidhani kama yupo hai sisi tunaamini ameishakufa lakini uongozi wa shule hii ndiyo umetuulia mtoto wetu. Polisi wanajua sasa sijui kama wameishawauliza au bado,” alisema Maduhu.

 Kapere amekwishaieleza Tanzania PANORAMA Blog kuwa Mkuu wa Shule ya St. Mary’s, Ntipoo alikiri kufanya uzembe kutotoa taarifa polisi na kwa wazazi kuhusu kupotea kwa mwanafunzi Labna na kwamba kutoroka kwa wanafunzi usiku na kwenda kwenye maeneo ya starehe ni jambo alilolikuta shuleni hapo hivyo hata baada ya kutoonekana kwa Labna aliamini kuwa alitoroka usiku kwenda kwenye mambo yake lakini angerudi.

 Aidha Kapere amwishaeleza kuwa timu imebaini kuwa Shule ya Sekondari ya St Mary’s ni chafu, haina ulinzi wa kutosha na ukuta wake haufai.

 

 

 

KAMANDA BUKOMBE AONDOLEWA KINONDONI, APELEKWA MAKAO MAKUU


NA MWANDISHI WETU

ALIYEKUWA Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Kipolisi wa Kinondoni (RPC), Kamishna Msaidizi Mwandamizi, Edward Bukombe, amehamishwa kituo chake cha kazi na kupelekwa makao makuu.   

Taarifa zilizoifikia Tanzania PANORAMA Blog kutoka vyanzo vyake vya habari zimeeleza kuwa Kamanda Bukombe sasa anakwenda kuongoza kitengo cha picha na matukio na kwamba uhamisho huo ni wa kawaida.

Kwa mujibu wa taarifa hizo, nafasi ya Kamanda Bukombe imechukuliwa na Kamishna Msaidizi wa Polisi, Ramadhani Kingai ambaye katika mahojiano yake leo na Tanzania PANORAMA Blog amethibitisha kurithi wadhfa huo akitokea mkoani Arusha.  

Thursday, November 26, 2020

WAZABUNI WANAOIDAI TAMESA WAOMBA MSAADA WA WAZIRI MKUU


NA MWANDISHI WETU

WAZABUNI waliosambaza vipuli na kutengeneza magari ya Wizara na Idara za Serikali kupitia Karakana Kuu ya Temesa - MT Depot, wamemuomba Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa aingilie kati kusaidia walipwe madeni wanayodai.

Akizungumza na Tanzania PANORAMA Blog, Mwenyekiti wa Umoja wa Gereji Tanzania (UGETA), Lumona Mkala, alisema wanachama wake wanaidai Temesa - MT. Depot zaidi ya shilingi Bilioni nne.

Mkala amesema kwa nyakati tofauti wamefuatilia kulipwa fedha zao bila mafanikio na wakati mwingine wanapewa  majibu yasiyoonyesha ushirikiano kutoka Ofisi ya Meneja wa MT Depot, Injinia Joseph Maronga.

"Unapofika ofisi ya meneja, unaambiwa nenda kwa mhasibu, ukifika kwa mhasibu anakwambia urudi kwa Meneja...Hivyo tunakuwa hatuna majibu ya lini pesa zetu tutalipwa," amesema Mkala.

Amezitaja baadhi ya gereji zinazodai kuwa ni Beka Investment shilingi 250,563,150, Moroturbo shilingi 80,256,197, Planet Busines link shilingi 175,312,570 na Ndeken shipingi 194,801,393

Nyingine ni Kigustar Enterprisess,  Leonardo Automotive Garage, Nedea Enterprisess, RaaR Investment, Kigoma Garage, Adam Motor na Point A.

Mkala amesema wamelazimika kumuomba Waziri Mkuu aingilie kati baada ya hatua alizozianza mwanzoni mwa mwaka huu,  kuzitaka wizara na idara za serikali ambazo ndizo zilizohudumiwa na gereji hizo!kulipa madeni yao wanayodaiwa kushindwa kufanikiwa.

"Hizi Idara na wizara tulizozihudumia tunazo taarifa kwamba baada ya agizo la Waziri Mkuu wamelipa fedha lakini Meneja wa MT Depot hataki kutulipa," amesema.

Alipotafutwa kuzungumzia madai hayo, Meneja wa MT Depot, Injinia Maronga, amesema yeye siyo msemaji wa taasisi hiyo na kumuelekeza mwandishi wa habari hizi kumtafuta Ofisa Habari ya Temesa, Theresia Mwami.

Mwami alipotafuta na kuulizwa kuhusu madai hayo, alisema hana majibu na kumtaka mwandishi awasiliane na Mtendaji Mkuu wa Temesa Dk. Stephen Masele.

Mtendaji wa Temesa alipotafutwa na kuulizwa kuhusu madeni hayo,  alikiri taasisi hiyo kudaiwa lakini alitaka mwandishi apate  nafasi ya kumfafanulia madeni hayo.

"Nipo Dodoma kuna vikao tunaendelea navyo, nitakupigia baadaye au njoo Dodoma," amrsema Masele.

Hata hivyo, taarifa zilizopatikana kutoka Ofisi za Mhasibu Mkuu wa MT Depot zimedai kuwa fedha zilizokusanywa hazizidi shilingi milioni 500 ambapo Temesa wameziweka  wakisubiri maelekezo ya Waziri Mkuu ili waweze kuwalipa wazabuni hao.

"Kiukweli hili suala ni dogo sana, lakini mtendaji wetu anasubiri kupata maelekezo ya nani  na nani alipwe, " alisema  na kuongeza,  "Temesa kama Temesa na sisi tunazidai hizo Idara na Wizara za serikali karibu Shilingi billion 5.

Wazabuni hao, wanalalamika kuwa kutolipwa madeni yao tangu  2016 kunasababisha washindwe kujiendesha kwa vile nao wanadaiwa fedha nyingi  na taasisi za fedha.

ANAYETUHUMIWA KUMTOROSHA MWANAFUNZI ST MARY'S MBARONI

NA MWANDISHI WETU

MAKACHERO wa Jeshi la Polisi wamemkamata Rahim Nyamka kwa tuhuma za kumtorosha na kumuachisha masomo, mwanafunzi Labna Said Salim anayesoma kidato cha tatu katika Shule ya Sekondari ya Bweni ya St. Mary's iliyoko Mbezi Makonde.

Taarifa za uhakika zilizoifikia Tanzania PANORAMA kutosha ndani ya timu ya maafisa wanne waandamizi wa serikali Wilaya ya Kinondoni inayomsaka Labna zimeeleza kuwa Nyamka alikamatwa Juzi, Novemba 24 na kuhojiwa kabla ya kupendekezwa na timu hiyo kuwa asipewe dhamana.

Timu inayomsaka Labna ambaye alitoweka shuleni tangu Oktoba 4, 2020 inaundwa na Kamanda wa Polisi wa Mkoa Kinondoni, Afisa wa Usalama wa Wilaya, Afisa Elimu Sekondari na Mthibiti Elimu Kanda.

Taarifa kutoka ndani ya timu ya uchunguzi zimeeleza kushangazwa na uamuzi wa polisi kutozingatia maelekezo ya timu ya uchunguzi ya kutompatia dhamana mtuhumiwa huyo.

"Tumemsaka huyo mtuhumiwa mpaka tumempata, tulimkamata tukiwa na askari wapelelezi tukampeleka kituo cha Polisi Goba ambako ndiko kesi ilikofunguliwa, huko tulimuhoji kisha tukawaachia polisi lakini tuliwaambia wasimwachie kulingana na mwenendo wa uchunguzi wa shauri hili.

" Ajabu tulipoondoka wakampa dhamana. Hili jambo limetushangaza hata sisi kwani tumeshindwa kujua kuna nini kinaendelea pale Polisi Goba lakini wapo wenzangu wa vyombo vya ulinzi na usalama ndani ya timu nao wameliona hili na limewashangaza pia naamini watalifanyia kazi, alisema mmoja wa wajumbe wa timu hiyo.

Akizungumzia mwenendo wa uchunguzi ulipofikia alisema Labna bado hajapatikana na baada ya kuhojiwa kwa Nyamka alikana kumtorosha au kuwa naye.

"Bado aisee, yule mtuhumiwa Nyamka amekana tuhuma zote lakini vijana sita tuliowakamata wakivuta bangi ndani ya nyumba ya baba yake Nyamka ambaye Kamishna Mstaafu Magereza wamekiri katika mahojiano kuwa Labna alifika kwenye hiyo Nyumba na alikuwa anawapikia na walipata kumvutisha bangi.

" Mbali na hao, wale vijana waliomsadia kuruka ukuta nao wamekiri kuwa ni kweli walitenda tukio hilo. Tatizo kuna mambo ambayo timu inapigana kuyabaini lakini huko chini kuna watu wanavuruga," alisema.

Jitahidi za kumpata Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Kipolisi Kinondoni kuzungumzia suala hilo hazikuzaa matunda baada ya simu yake kuwa inaita  bila kupokelewa.

Labna alitoweka shuleni Oktoba 4, mwaka huu lakini uongozi wa shule ya St Mary's alificha taarifa za kutoweka kwake hadi Oktoba 8, 2020 ambapo Matroni wake anayefamika kwa jina la Sarah Murra alipompigia simu yake mama yake kumuiliza kama yupo nyumbani.

Mkuu wa Shule ya St. Mary's Sekondari, Reca Ntipoo amekaririwa na timu ya uchunguzi akiungama kuwa uongozi wa shule ulifanya makosa kutotoa taarifa polisi kuhusu kutoweka kwa mtoto huyo.

Ntipoo pia alieleza timu hiyo kuwa alipohamishiwa shuleni hapo alikuta wanafunzi hao wakitoroka usiku na kurudi alfajili jambo lilimjanisha kuwa hata Labna baada ya kutoroka angerudi kwa sababu kitendo hicho ni kawaida shuleni hapo.

Aidha uchunguzi wa awali wa timu umebaini kuwa shule hiyo imepungukiwa sifa kwa sababu ni chafu, haina ulinzi wa kutosha na uzio wake (ukuta) siyo imara.

Timu hiyo pia ilibaini vijana saba waliokuwa wakivuta bangi nyumbani kwa Kamishna Mstaafu wa Jeshi Magereza na pia ndani ya ua wa nyumba kulikuwa na shamba la bangi. Nyumba hiyo ndiyo anayoishi Rahim na ndugu yake.

Tuesday, November 24, 2020

WALIOFICHA SARUJI KUSAKWA MKOA KWA MKOA



*Waziri Mkuu Majaliwa awaagiza MA RC kuwakagua mawakala, wauzaji wa kati na wadogo

NA MWANDISHI MAALUM

SERIKALI sasa imeanza kuchukua hatua mahususi za kupambana na wafanyabiashara wasiokuwa waaminifu walioficha saruji kwa lengo la kuleta taharuki katika nchi.

Hatua hizo zimetangazwa mwishoni mwa wiki iliyopita na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa kwa kuwaagiza wakuu wa mikoa yote nchini kufanya ukaguzi kwenye viwanda vya kuzalisha saruji, kwa mawakala na wauzaji wa kati na wadogo.

Waziri Mkuu Majaliwa amewaagiza wakuu wa mikoa kuwachukulia hatua stahiki wale wote watakaobainika kuficha saruji katika msako watakaoufanya.

Agizo hilo alilitoa alippkuwa akizungumza na Wakuu wa Mikoa yote nchini kuhusu tatizo la kupanda kwa bei ya saruji, kwenye kikao alichokiendesha kwa njia ya video (video conferencing) kutokea ofisini kwake Mlimwa, jijini Dodoma.

"Wakuu wa Mikoa na Kamati zenu za Ulinzi na Usalama fanyeni ukaguzi kwa mawakala, ukikuta wamerundika saruji kamata na kuwashtaki. Nendeni pia kwa wauzaji wa kati, nao pia chekini maghala yao.

“Piteni kwa maafisa biashara na muwasimamie iwe ni kwenye Sekretarieti za Mikoa au katika Halmashauri zenu, tunataka bei irudi kama ilivyokuwa mwezi Septemba kwa sababu hakuna badiliko lolote kwenye tozo ya kodi,” alisisitiza.

Agizo hili la kupambana na walanguzi wa saruji limetolewa na Waziri Mkuu Majaliwa katika kikao chake cha kwanza na Wakuu wa Mikoa tangu alipoapishwa kushika wadhfa huo kwa mara pili.

"Wakati wa uapisho, Novemba 16, mwaka huu nilitambulisha tatizo la kupatikana saruji kwa bei ya juu sana. Niliagiza kila Mkuu wa Mkoa afuatilie ni kwa nini bei imepanda kiasi hicho.

"Nimepokea taarifa zenu na kuona hali halisi iliyoko kwenye mikoa yenu. Hali si nzuri, akiba iliyopo ni ndogo na bei ni ya juu sana. Nasema bei ni ya juu sababu tunaangalia bei ya mlaji kwa sasa. Awali ilikuwa kati ya sh. 14,000 hadi 15,000 lakini sasa hivi imefikia sh. 24,000 kwa mfuko mmoja,” alisema.



Waziri Mkuu Majaliwa alisema hiyo ni tofauti ya sh. 9,000 hadi 10,000 lakini kwa sasa ni lazima bei ishuke kwa sababu hakuna tozo za kodi zilizoongezeka.

“Kuna watu wanatumia kigezo cha gharama za usafirishaji, hii si kweli kwani hata Septemba, walikuwa wakisafirisha bidhaa hiyo kwa njia zetu zile zile," alisema.

Waziri Mkuu Majaliwa alisema serikali ya awamu ya tano imekuwa ikihimiza ujenzi wa viwanda ili bidhaa zinazozalishwa nchini zipatikane kwa wingi. “Kwenye saruji malighafi ziko nchini, hazitoki nje, kwa hiyo tunataraji upatikanaji wake uwe rahisi na bei ingekuwa nafuu," alisema.

Aidha, aliwaagiza wakurugenzi wa Wizara ya Viwanda na Biashara wakutane na wenye viwanda na kuweka ratiba ya mwaka ili kuepuka viwanda vingi kufungwa kwa matengenezo ya mwaka kwa wakati mmoja na kufanya saruji iadimike na kupandisha ghafla bei ya saruji.

Vilevile, aliwaagiza viongozi wa Tume ya Ushindani (FCC) wafuatilie wamiliki wenye viwanda vya saruji na wafanye uchunguzi kubaini uhalali wa bei zinazopangwa na mawakala na wafanyabiashara wa saruji nchini.  Pia akawataka wawasisitizie wazingatie sheria za nchi.

Kwa upande wao, wakuu wa mikoa walisema wamepokea maelekezo na watayatekeleza.

Mkutano huo uliwashirikisha pia Naibu Makatibu Wakuu wa Wizara za Viwanda na Biashara; Uchukuzi na watendaji kutoka Tume ya Ushindani.

Friday, November 20, 2020

MSAKO WA LABNA WA ST MARY'S WAIBUA MADUDU YA KUTISHA, SHAMBA LA BANGI LABAINIKA NYUMBANI KWA KAMISHNA

 


NA MWANDISHI WETU

TIMU ya maafisa wanne waandamizi wa serikali iliyoundwa na Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Daniel Chongolo kumsaka mwanafunzi wa kidato cha tatu wa Shule ya Sekondari ya Bweni ya St Mary's, aliyepotea tangu Oktoba 4, 2020 imebaini kuwa shule hiyo imepungukiwa sifa zinazostahili kisheria.

Afisa Elimu Sekondari ya Wilaya ya Kinondoni, Joseph Kapere ameyasema hayo alipokuwa akielezea mwenendo wa msako na uchunguzi wa mazingira ya kutoweka kwa mwanafunzi Labna unaofanywa na timu iliyoundwa na Chongolo.



Kapere alisema katika uchunguzi huo ulioanza jana  kwa kumuhoji Mkuu wa Shule ambaye alieleza kuwa Labna aliwaambia walimu hataki shule na alitoroka akaenda kwa rafiki yake ya kiume wakawa wanaishi pamoja.

"Tunafanya uchunguzi kwa umakini sana. Tumeishamuhoji Mkuu wa Shule na yeye ametueleza kuwa huyo mtoto alikwishawambia walimu kuwa hataki shule na aliondoka shuleni kwa kutoroka.

"Mkuu wa Shule alituambia kuwa motto alitoroka shuleni kwa kuruka ukuta usiku akisaidiwa na wanafunzi wenzake wavulana wawili, akaenda kwa boy friend wake wakaanza kuishi pamoja huko,” Kapere alimkariri mkuu wa shule.

Alisema mkuu huyo wa shule aliipeleka timu ya serikali nyumba aliyokuwa akiishi Labna na mpenzi wake baada ya kutoroka shule lakini waliwakosa na badala yake walikuta wavulana saba wakiwa wanavuta bangi.

"Mkuu wa shule anapajua alipotorokea mtoto huyo na alitupeleka kwenye hiyo nyumba. Ni nyumba ya Kamishna Mstaafu wa Magereza ambayo wanaishi watoto wake wawili lakini hapo hatukumta Labna wala boy friend wake, tulikuta vijana saba waliokuwa wanavuta bangi na nyumba nzima ilikuwa imetapakaa misokoto ya bangi.

"Kwa kweli ni hali ya kutisha sana kwa vijana wetu. Walituambia ni kweli Labna alipotoroka shule alikuwa akiishi hapo na boy friend wake na alikuwa mama wa nyumbani kwani alikuwa akiwapikia na kufanya usafi wa nyumba lakini baada ya muda kidogo aliondoka.

"Boy friend wake naye hatukumkuta, wale vijana wavuta bangi walisema anasoma chuo CBE na anaishi hostel sasa tumepeleka makachero akakamatwe huko.

“Lakini hiyo nyumba baada ya kuichunguza kwa sababu ina uzio mkubwa sana tulikuta shamba la bangi humo ndani. Yaani bangi inalimwa humo humo nyumbani kwa Kamishna wa Magereza wanavuna wanavuta hao vijana.

"Basi wale vijana tuliwachukua hadi polisi wamelala huko kwa ajili ya uchunguzi zaidi na taratibu nyingine zitafuata," alisema Kapere.

Alipoulizwa iwapo timu hiyo imebaini ni kwanini Mkuu wa Shule baada ya kuambiwa na Labna kuwa hataki shule hakuwapa taarifa wazazi na hata alipotoroka uongozi wa shule ulikaa kimywa wala haukutoa ripoti polisi, alisema mwalimu huyo amekiri kuwa yeye na wenzake walikosea.

Tanzania PANORAMA lilimuuliza pia Kapere kama timu ya serikali imebaini ni kwanini Mkuu wa Shule baada ya kubaini mwanafunzi wake ametoroka na alikuwa akiishi na mwanaume nje ya shule hakuchukua hatua za kutoa taarifa kwa wazazi na polisi ili wote wawili wakamatwe kwa kuzingatia mwanafunzi huyo wazazi wake walimkabidhi kwa uongozi wa shule, Kapere alisema swali hilo ni zuri na watamuuliza Mkuu wa Shule.

"Timu yetu ina polisi, hata nyumba ya  kamishna tuliivamia tukiwa na polisi. Polisi waliizingira kisha wakaingia ndani ndiyo wakakuta lile shamba la bangi na ile misokoto. Lakini Mwalimu anajitetea yeye ni mgemi na tabia ya watoto kutoroka usiku wakarudi alfajili aliikuta. Lakini pia mkuu wa shule alituambia kuwa awali yeye, polisi na wajomba wa huyo wa mtoto walikwenda hadi kwenye hiyo nyumba kumsaka lakini polisi na wajombe hawakuingia ndani, waliishia nje.  

"Sasa hata Labna alipotoroka Mwalimu amesema mwenyewe alijua ndiyo kawaida yao atarudu lakini kwa bahati mbaya yeye hakurudi, akahamia kabisa kwa huyo boy friend wake.

"Uchunguzi wetu sasa pale shuleni imebaini kuwa ile shule haifai, imepungukiwa sifa stahiki za kuitwa shule. Kwanza ni chafu sana, haina walinzi wa kutosha na hata ukuta wake haufai," alisema Kapere.

Alisema anaamini mtoto huyo yupo hai na atapatikana katika msako unaoendelea.

Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Daniel Chongolo alipoulizwa jana alisema yupo msibani hivyo hayupo katika nafasi kuzungumza.

Labna, mwanafunzi wa Shule ya Sekondari ya St. Mary’s iliyoko Mbezi Makonde Jijini Dar es Salaam alitoweka shuleni tangu Oktoba 4, 2020 lakini tukio  la kutoweka kwake halikuripotiwa polisi na uongozi wa shule.

SERIKALI YAANZA MSAKO MKALI MWANAFUNZI ALIYEPOTEA ST MARY'S

 

NA MWANDISHI WETU

HATIMAYE serikali imeanzisha msako mkali wa mwanafunzi Labna Salim Said wa kidato cha tatu katika Shule ya Sekondari ya Bweni ya St Mary's ambaye amepotea tangu Oktoba 4, 2020 akiwa shuleni.

Taarifa za uhakika zilizoifikia Tanzania PANORAMA Blog zimeeeza kuwa, msako huo umeanza jana baada ya kufanyika kwa kikao cha ulinzi na usalama cha Wilaya ya Kinondoni kilichoongozwa na Mkuu wa wilaya hiyo, Daniel Chongolo.

Chongolo ameithibitishia Tanzania PANORAMA  kuitisha na kuongoza kikao hicho na kueleza kuwa serikali imeanza kuchunguza mazingira ya tukio la kupotea kwa mwanafunzi huyo akiwa shuleni kwa kuunda kikosi maalumu kinachojumuisha vyombo vya ulinzi na usalama.

Hata hivyo, Chongolo alisema hayuko katika nafasi nzuri ya kulizunguzia suala hilo kwa sababu kuhofia kuharibu mwenendo wa uchunguzi wa timu yake aliyoiunda.

Akizungumzia hatua hiyo ya serikali kujitosa rasmi kwenye sakata la kupotea kwa mwanafunz Labna, Afisa Elimu Sekondari wa Wilaya ya Kinondoni, Joseph Kapere Chongolo aliitisha kikao cha kamati ya ulinzi na usalama ofisini kwake jana mchana baada ya kupokea malalamiko ya wazazi wa mtoto huyo kupotea akiwa shuleni.

Kapere alisema katika kikao hicho kilichohudhuliwa pia na wazazi wa mtoto huyo, Chongolo aliunda kamati ya watu  wanne kumsaka mtoto Labna popote alipo na kuchunguza mwenendo mzima wa tukio la  kupotea kwake.

"Hili tukio ni la aina yake lakini tunasikitika kuwa limechelewa kutufikia, hata mkuu wa wilaya kafahamu jana baada ya wazazi kumfikishia kesi hiyo. Hizo shule zipo chini yangu mimi ndiyo nashughulika nazo.

"Sasa mkuu wa wilaya aliitisha kamati ya ulinzi ya usalama na ameteua kikosi cha watu wanne kumsaka mtoto huyo.

"Walioteuliwa kwenye kikosi hicho ni viongozi waandamizi wakiwemo kutoka ofisi ya Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Kipolisi wa Kinondoni, ofisi ya Afisa Usalama wa Wilaya ya Kinondoni, mimi mwenyewe Afisa Elimu Sekondari Wilaya ya Kinondoni," alisema Kapere.

Mwanafunzi msichana, Labna wa Shule ya Sekondari ya Bweni ya St. Mary’s alitoroka shuleni usiku na kutokomea kusikojulikana na hadi sasa hajapatikana.

Labna alitoroka Oktoba 4, 2020 akiwa chini ya uangalizi wa shule lakini taarifa za kupotea kwake zilitolewa Oktoba 8, 2020 na matron wake Sarah Murra aliyempigia simu mama mzazi wa Labna akiulizia kama ameishafika nyumbani.

Katika hatua ya kushangaza, uongozi wa Shule ya Sekondari ya St Mary’s haukutoa taarifa polisi kuhusu kupotea kwa mwanafunzi huyo na badala yake wazazi ndiyo walioripoti tukio la mtoto wao kupotea akiwa shuleni.

 

Thursday, November 19, 2020

FISI MADOA MNYAMA ANAYEWEKA MIPAKA YA HIMAYA YAKE KWA KINYESI CHAKE


 NA ERNEST SITTA

MAISHA ya mnyama Fisi yana mengi ya kuvutia kuyajua ambayo yanamsaidia binadamu kutambua umuhimu wa mnyama huyu katika uso wa dunia.

Fisi wamegawanyika katika makundi manne ambayo ni Fisi Madoa, Fisi Miraba, Fisi Kahawia na Fisi Aardwolf na asili yao ni familia inayofahamika kwa jina la kitaalamu la Hyenidae.

Taungalie kwanza maisha ya Fisi Madoa, mnyama anayetokea kwenye familia ya Hyenidae.

Kwa kawaida Fisi wote ni wanyama wanatokea katika kundi la wanyama walao nyama.

Fisi madoa ana urefu wa sentimita 77 kutoka mkiani hadi kwenye mabega akiwa amesimama.

Uzito wake ni kilo 63 kwa dume na jike ni kilo 68, hivyo jike ni mkubwa kuliko dume.



Fisi madoa anabeba mimba kwa muda wa miezi mitatu na nusu na huzaa watoto kuanzia mmoja mpaka wanne. Umri wake wa kuishi ni miaka 50.

Aina hii ya wanyama wanapendelea kukaa kwenye mashimo au mapango katika familia inayoongozwa na mtawala ambaye ni jike na kufuatiwa na majike daraja mbalimbali za utawala katika familia.

Sehemu hizo za mapangoni hutumika kuishi na kulea watoto wa rika mbalimbali. Jinsia ya kike hukaa katika himaya waliyozaliwa maisha yao yote lakini Fisi madume baada ya kufikia miaka minne huanza kujiandaa kuondoka kwenye familia.

Fisi madume baada ya kutimiza miaka minne hutoka na kujiunga na familia nyingine.

Fisi hawa huweka mipaka ya himaya yake kwa kutumia utomvu wenye harufu kali kutoka kwenye tezi lililomo ndani ya sehemu ya kujisaidia haja kubwa.



Mnyama huyu ni mahiri wa kuwinda, ana uvumilivu na nguvu nyingi za shingo. Umbo la fuvu la kichwa lina meno makali yenye uwezo wa kutafuna hata mifupa.

Kinyesi cha Fisi Madoa kina rangi nyeupe kama chaki au chokaa.

 Jike mtawala pamoja na watoto wake humiliki himaya na chochote kilichopo ndani ya eneo kama ni mnyama wameshirikiana kuua ndani ya himaya wa kwanza kula ni jike mtawala pamoja watoto wake, wakishatosheka ndipo Fisi wengine watafuatia kwa kuzingatia daraja mbalimbali au rika.

Chakula kisipotosha familia nzima ya Fisi wawindaji au wavizia mizoga husafiri kwenda mbali muda wa siku moja au mbili kutafuta chakula kingine cha kutosheleza kundi zima na kurudi kuwatapikia watoto wao.



Watoto wa Fisi Madoa waliozaliwa na jike mtawala wanakuwa na bahati ya kuendelea kutawala, vivyo hivyo wanaozaliwa na mama ambaye yupo daraja la chini huendelea  kutawaliwa na hawapewi kipaumbele hasa katika masuala ya chakula.

Katika jamii zetu za kiafrika hasa za Kusini mwa Jangwa la Sahara, Fisi huhusishwa na imani za kishirikina na hasa wanaposikika kwa milio tofauti karibia na mazingira ya makazi ya watu.

Lakini kiuhalisia sauti za Fisi huashiria  kuomba msaada endapo mmoja ameona mawindo, mzoga au msaada kama kuna adui.

Fisi ni muhimu sana katika mapori tengefu na hifadhi za taifa. Mfano katika  mfumo wa kiikolojia wa Serengeti-Maasai Mara Kenya unajumuisha wanyama mbalimbali wakiwemo wanyama wahamiaji - Nyumbu zaidi ya milioni mbili ambao kila mwaka wanahama kutoka sehemu wanapozaa na kuenda sehemu wasipozaa kwa ajili ya mabadiliko ya hali ya hewa, kutafuta chakula, mazingira na maji.

Fisi Madoa na jamii nyingine za Fisi huitwa bwana afya katika hifadhi kwa sababu ya kula idadi kubwa ya mizoga ingawa kuna wanyama wengine kama Simba, Chui, Mbweha na ndege aina ya Tumbusi ambao nao hula mizoga hiyo.

Hivyo bila Fsi kula mizoga hiyo kwa idadi kubwa, hifadhi zingekuwa zinanuka na kukatisha wageni kuzitembelea jambo ambalo lingechangia kupoteza mapato yatokanayo na utalii.

ERNEST SITTA NI MTAALAMU WA ELIMU YA WANYAMA NA MIMEA AMBAYE AMEFANYA KAZI NA TAFITI MBALIMBALI KATIKA HIFADHI TOFAUTI TOFAUTI HAPA NCHINI KWA ZAIDI YA MIAKA 10

DSTV YAJA NA OFA KABAMBE YA MSIMU WA SIKUKUU

 



NA MWANDISHI MAALUM

KATIKA kunogesha zaidi msimu wa sikukuu za mwisho wa mwaka na mwaka mpya, Kampuni ya MultiChoice Tanzania imetangaza ofa kabambe kwa wateja wapya wa DStv yenye lengo la kuhakikisha Watanzania wengi wanapata huduma hiyo ili waweze kufurahia burudani, elimu na habari wao na familia zao msimu huu wa sikukuu.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa kampeni ya DStv ya msimu wa sikukuu iliyopewa jina la ‘Vibe la sikukuu na DStv kama DStv’, Mkuu wa Masoko wa MultiChoice Tanzania, Ronald Shelukindo amesema kama ilivyo ada kwa DStv, kila unapofika msimu wa sikukuu hutoa ofa maalum kwa wateja wake ili kuwapa uhakika wa kupata huduma za DStv kipindi cha sikukuu na watu wengi wakiwemo watoto huwa likizo hivyo kuwepo kwa uhitaji mkubwa wa burudani nyumbani.

Akifafanua, Shelukindo amesema kampeni ya msimu wa sikukuu DStv hutoa ofa maalum kwa wateja wake.

“Kwa wale ambao bado hawajajiunga na DStv, huu ndio wakati muafaka kwani kuna ofa maalum ya kujiunga ambapo mteja ataunganishwa na DStv kwa Sh,79,000 tu na zawadi ya kifurushi cha Family mwezi mmoja bila malipo” alisema Shelukindo.

Alisema ofa hii inawapa uhakika wateja wapya kufurahia maudhui motomoto ndani ya DStv na itadumu hadi mwisho wa mwezi Desemba 2020.


Mkuu wa Mauzo wa MultiChoice Tanzania, Salum Salum akizungumza wakati wa uzinduzi wa kampeni ya msimu wa sikukuu ambapo DStv imetangaza ofa kabambe kwa wateja wake


Akifafanua zaidi kuhusu ofa hiyo alisema inapatikana nchi nzima kwa mawakala wa DStv hivyo mteja atapata ofa hii na huduma ya kufungiwa DStv popote alipo kwa urahisi na haraka.

“Tunafahamu kuwa kipindi hiki cha sikukuu watu wengi husafiri kuungana na familia zao maeneo mbalimbali mijini na vijijini na kwa kulitambua hili tumejipanga kuhakikisha huduma zetu zinapatikana kirahisi kila mahali”

Amewashauri wateja wote ambao wanahitaji huduma za DStv, mbali na kwenda kwenye vituo au mawakala wa DStv, wanaweza pia kupata huduma hiyo kwa kupiga simu 0659070707 au kwa kutembelea kurasa za DStv Tanzania za mitandao ya kijamii Instagram @dstvtanzania, Twitter @DStv_Tz na Facebook @DStv(tz) ambapo wanaweza kupata huduma mbalimbali za DStv kama vile kuunganishwa, kulipia vifurushi, kubadili kifurushi na huduma nyinginezo.

Kwa wateja wa DStv, Salum amesema wataendelea kupata maudhui kemkem kuanzia michezo, burudani, vipindi vya elimu, chaneli za watoto, sinema na tamthilia za ndani na nje bila kusahau chaneli za habari zitakazowahakikishia taarifa mbalimbali kutoka pande zote za dunia.

Kwa wale wanaosafiri, amewakumbusha kupakua App ya DStv Now inayowawezesha kuendelea kufurahia huduma za DStv kwenye vifaa mbalimbali kama simu janja bila gharama yaziada.

“Kwa wale wanaosafiri na wangehitaji kuendelea kuburudika na DStv, ni vyema wakatumua huduma yetu ya DStv Now kwa kupakua app yetu na hivyo kuweza kutumia akaunti zao katika vifaa zaidi ya vine popote walipo nchini bila kulazimika kulipia malipo yoyote ya ziada” alisisitiza Salum



Waigizaji maarufu katika tamthilia ya Karma Ford (kulia) na Misa (Katikati) wakiwa pamoja na maafisa wa DStv Tanzania – Mkuu wa Masoko Ronald Shelukindo (wa pili kulia), Mkuu wa Mauzo Salum Salum (wa pili kushoto) na Afisa Uhusiano wa kampuni hiyo Grace Mgaya (kushoto) wakati wa uzinduzi wa kampeni ya msimu wa sikukuu

 Hafla ya kuzindua kampeni hiyo ya DStv ilihudhuriwa na baadhi ya wasanii maarufu wa Bongo Movie wanaoigiza katika tamthilia na filamu mbalimbali zinazoonyeshwa kwenye chaneli ya Maisha Magic Bongo ndani ya DStv akiwemo kinara wa tamthilia maarufu ya Karma Wema Sepetu.

 

 

Wednesday, November 18, 2020

WAFANYAKAZI MR CLEAN WAMLILIA JPM

 


NA MWANDISHI WETU

WAFANYAKAZI wa Kampuni ya udobi ya Mr Clean ya jijini Dar es Salaam wamemuomba Rais John Magufuli atakapoteua Baraza la Mawaziri, amuelekeze Waziri wa Kazi, Vijana na Ajira kutafuta suluhu ya kudumu kwa watanzania wanaofanyishwa kazi muda mrefu bila kupewa mikataba ya kazi.

Wakizungumza na Tanzania PANORAMA Blog hivi karibuni kuhusu kutopatiwa mikataba ya kazi na mwajiri wao kwa muda mrefu, walisema wao ni sehemu tu ya watanzania wengi wanaonyanyasika sehemu za kazi na wameamua kupaza sauti zao ili Rais ambaye amekuwa akiwatetea wanyonge awasikie.

"Tunaamini Rais akisikia kilio chetu atatusidia kutatua hii kero yetu. Sisi tumefanya kazi kwa zaidi ya mwaka mmoja sasa katika Kampuni ya Udobi ya Mr Clean lakini mwajiri wetu hajatupa mikataba ya kazi. Kila tukiomba anatishia kutufukuza kazi.

"Tunapenda kufanya kazi kwa sababu bila kazi kwa maisha ya sasa mtu unakufa njaa na tunafurahi wanapojitokeza wawekezaji na wafanyabiashara wenye makampuni wanaotoa nafasi za kazi lakini mazingira ya kazi ni magumu mno.

"Mtu unakuwa kibarua mwaka mzima, miaka miwili, kazi yenyewe ngumu maana tunafua nguo kwa madawa ambayo hatujui yana kemikali za aina gani. Matokeo yake ukiugua unaondolewa kazini.

"Hatuna pensheni ya aina yoyote, hatuna Bima ya Afya, tunafua nguo kwa kutumia madawa, tunalipwa mkononi kama vibarua serikali haipati kodi yoyote ambayo ingetokana na mishahara yetu. Tunaomba kilio chetu kimfikie rais atuletee waziri wa kutafuta ufumbuzi wa matatizo yetu wafanyakazi wa sekta binafsi," alisema mmoja wa wafanyakazi hao.

Alipoulizwa Mkurugenzi wa Kampuni ya Mr Clean, Ravi Shankar kuhusu malalamiko ya wafanyakazi hao alisema suala hilo aulizwe msemaji wa Kampuni yake aliyemtaja kwa jina la Morris Ngonyani.

 

Alipoulizwa Ngonyani alisema yeye siyo msemaji wa kampuni ya Mr Clean bali mwenye Kampuni akiwa na hisa asilimia 90 na huyo alielekeza aulizwe ni mfanyakazi wake ambaye hana ruhusa ya kuzungumza lolote kwa sababu amemuweka kiwandani hapo kama msimamizi wa wafanyakazi tu.

Akijibu malalamiko ya wafanyakazi hao alisema walikuwa vibarua ambao kwa sasa wameishaondolewa kazini na kwamba Kampuni ya Mr Clean imebaki na wafanyakazi saba tu nchi nzima kutokana na mwenendo mgumu wa biashara.

CCM ILALA YATOA MSIMAMO MADAI YA DIWANI WAKE KUDANGANYA URAIA




NA MWANDISHI WETU

CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Ilala kimesema hakina shaka na maelezo yaliyotolewa na Diwani wake wa Kata Kivukoni, Sharik Choughule kuhusu uraia wake.

Kimesema kabla ya wagombea wa chama hicho kupitishwa kupeperusha bendera  ya chama katika uchaguzi, kilijiridhisha kuwa wote wana sifa stahiki.

CCM kimesema watu wanaoibuka sasa kudai uraia wa Choughule una utata wanapaswa kupuuzwa kwa sababu CCM huteua wagombea wake kwa umakini na baada ya kujiridhisha hivyo wenye shaka na uteuzi huo wafuate taratibu za kimahakama kuthibitisha madai yao.

Hayo yameelezwa jana na Katibu wa CCM wa Wilaya ya Ilala Iddi Mkowa katika mahojiano yake na Tanzania PANORAMA kuhusu madai ya utata wa uraia wa Choughule na kwamba alitoa taarifa zisizokuwa sahihi kwa chama zilizomuwezesha kuteuliwa.

Mkowa alisema CCM hakina muda wa kuanza kuchunguza tuhuma za udanganyifu au utata wa uraia wa kada wake huyo kwa sababu kina uhakika na taarifa alizotoa hivyo wenye wasiwasi wana wajibu wa kuthibitisha madai yao kisheria ndipo chama kiweze kuchukua hatua.

Kauli hii ya Mkowa inafuatia taarifa iliyoripotiwa juzi na Tanzania PANORAMA kuwa Choughule anadaiwa kutoa taarifa zisizokuwa sahihi kuhusu uraia wake ili kufanikisha azma yake ya kuwa kiongozi katika chama hicho.

Madai hayo yalianza kusambaa mapema mwezi uliopita lakini jitahada za Tanzania PANORAMA kumfikia kuyazungumzia hazikuweza kufanikiwa kutokana na kile kilichoelezwa kuwa kutingwa na shughuli nyingi za kisiasa.

Hata hivyo, mmoja wa viongozi wa kata hiyo aliyefikiwa na Tanzania PANORAMA na kukubali kuzungumza kwa sharti la jina lake kuhifadhiwa kwa vile hataki aonekane ana nia mbaya dhidi ya mbio za kusaka uongozi wa kisiasa za Choughule, alisema awali kulikuwa na utata huo lakini ulitatuliwa.

Taarifa zilizokusanywa Tanzania PANORAMA zimeonyesha kuwa Choughule aliingia nchini kwa kutumia hati ya kusafiria ya India akiwa ameambata na ndugu yake wa kiume, ambao walikuja kumtembelea mjomba wao anayefanya biashara jijini Dar es Salaam.

Uchunguzi umeonyesha kuwa Choughule na ndugu yake walikuja nchini kuonana na mjomba wao aliyekuwa ametwaa mali za baba yao baada ya kufariki dunia.

Washirika wa karibu wa Choughule wamekaririwa kuwa vijana hao wawili walishindwa kuafikiana na mjomba wao ndipo walipogoma kuondoka nchini kurejea India walikokuwa wakiishi na mama yao.

Kwamba ili kuzika mzozo baina yao, mjomba wao aliwaingiza katika moja ya kampuni zake kufanya kazi huku akiwataka wawe na subira ya kutatua utata wa umiliki wa mali hizo.

 Imeelezwa kuwa mjomba (jina limehifadhiwa kwa sababu hajapatikana kuzungumza) alitoa taarifa ofisi za uhamiaji kuhusu uwepo wa vijana hao waliokuwa wakiishi nchini na kufanya kazi kinyume cha sheria na walikamatwa na taratibu za kuwarudisha India zilianza kufanyika.

Taarifa zaidi zimeeleza kuwa vijana hao walilia na kupiga magoti mbele ya mjomba wao wakimuomba azungumze na maofisa wa Uhamiaji ili wasirejeshwe India kwa sababu walikuwa wakiishi maisha ya shida na mama yao baada ya baba yao kufariki na kwamba mjomba wao alikuwa hawatumii fedha kama alivyokuwa akifanya baba yao licha ya kujimilikisha mali zote.

Inadaiwa mjomba wao aliwapa sharti la kutomuuliza tena kuhusu mali alizotwaa kwa marehemu kama wanataka kiendelea kuwepo Tanzania, amri ambayo waliiafiki na yalifanyika mazungumzo wakaachiwa.

 Afisa mmoja wa CCM wa Kata ya Kivukoni ambaye jina lake limehifadhiwa ameeleza kuwa ni kweli vijana hao waliingia nchini wakitokea India na kufikia kwa mjomba wao kabla ya kukamatwa na maofisa uhamiaji ambao waliwapakia kwenye ndege na kuwarudisha India ambako walikataliwa kuingia na kurudishwa hapa nchini.

"Ni kweli Choughule alikuja nchini akiwa na mwenzake. Walikuja kwa mjomba wao lakini baadaye kulitoka mtafaruku wakakamatwa na uhamiaji wakapandishwa ndege wakarejeshwa India ambako hawakupokelewa walirudishiwa uwanja wa ndege, wakarejea Tanzania.

"Hakukuwa na namna ikabidi wapokelewe hapa nchini wakarudi tena kuishi na mjomba wao ndipo zikaanza kufanyika taratibu za uraia na uhamiaji iliwasafisha kwa kuwapa uraia wakawa huru kujihusisha na shughuli za kisiasa na mpaka sasa Choughule anaendelea na siasa," alisema.

Choughule amekuwa akikwepa kulizungumzia suala hilo kwa zaidi ya wiki tatu sasa kwani licha ya Tanzania PANORAMA kufika ofisi za CCM Kata ya Kivukoni ambako hakupatikani na kisha kutafutwa kwa simu yake ya kiganjani na kuomba apewe muda kabla ya kuzungumza, hajatekeleza ahadi yake hiyo wala kujibu maswali aliyotumiwa.

Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Hamphery Polepole ambaye alitafutwa kwa simu yake ya kiganjani kuzungumzia suala hilo, simu yake imekuwa ikiita bila majibu na hata alipotumiwa ujumbe wa maandishi kwenye simu yake hakuujibu.

Kwa mujibu wa taratibu za Idara ya Uhamiaji, raia wa kigeni anaweza kupewa uraia kabla ya kuwa na sifa za kugombea nafasi za uongozi wa kisiasa isipokuwa urais wa Tanzania akiishi nchini kuanzia miaka nane na kufuata taratibu za kuomba uraia ikiwemo muda wote wa kuishi nchini kuwa na kibali.

Tanzania PANORAMA limeperuzi sifa zinazotakiwa kwa wanachama wa CCM kugombea uongozi wa kisiasa ambapo ya kwanza inasomeka awe raia wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

 

 


WAZIRI MKUU AZINDUA UCHEPUSHAJI MAJI MTO RUFIJI

 


Misri yaahidi kufundisha Watanzania 25 kwa miaka mitatu mfululizo

NA MWANDISHI MAALUMU

WAZIRI MKUU, Kassim Majaliwa amezindua kazi ya uchepushaji maji ya Mto Rufiji kwenda kwenye handaki ili kupisha ujenzi wa tuta kuu la bwawa la kufua umeme wa megawati 2115.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, alisema mradi huo utawezesha nchi kuwa na umeme mwingi na wa kutosha lakini pia utawezesha kufanya biashara ya umeme na nchi za jirani.

Uzinduzi huo ambao ulifanyika jana Novemba 18, 2020 kwenye eneo la mradi, mkoani Pwani, ulimpa fursa Waziri Mkuu kukagua maendeleo ya utekelezaji wa mradi wa uzalishaji umeme kwa kutumia maporomoko ya Mto Rufiji.

"Upatikanaji wa *umeme wa bei nafuu na uhakika nchini kwetu utachochea ukuaji na mapinduzi katika sekta ya viwanda nchini kwa kushusha gharama za uendeshaji viwandani, kukabiliana na mfumuko wa bei, kuwezesha ushindani wa bidhaa za Tanzania katika masoko ya Afrika Mashariki, Afrika na duniani,” alisema.

Waziri Mkuu Majaliwa alisema hatua hiyo itaenda sambamba na kuvutia uwekezaji mkubwa, wa kati na mdogo katika sekta mbalimbali nchini kutokana kupungua kwa gharama za umeme za uzalishaji pamoja na kuwawezesha Watanzania wote kumudu gharama za umeme mijini hadi vijijini.



Alisema mradi huo ambao unafadhiliwa na serikali kwa asilimia 100 kwa gharama ya sh. trilioni 6.557, unasimamiwa na Mhandisi Mshauri wa Kitanzania kwa asilimia 100.

“Serikali imeendelea kuwaamini na kuwatumia wataalamu wa Kitanzania katika kusimamia miradi mikubwa, na kwa kutambua hilo mradi huu unasimamiwa na Mhandisi Mshauri wa Kitanzania kwa asilimia 100,” alisema.

Alisema mradi huo wa kufua umeme kwa kutumia maji wa Julius Nyerere ni mkubwa, wa kimkakati na wa aina yake katika ukanda wa Afrika, ukiwa ni wa kwanza kwa ukubwa kwa Afrika Mashariki na wa nne barani Afrika na akasisitiza kuwe na usimamizi makini na wa viwango ili kuhakikisha unakamilika katika muda uliopangwa.

“Nimeambiwa kwamba, mradi huu unaenda sambamba na ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme ya msongo wa kilovoti 400 kutoka eneo la mradi hadi Chalinze, yote hii ni kuhakikisha umeme unaotoka hapa unaingizwa kwenye gridi ya Taifa.”

Mapema, akimkaribisha Waziri Mkuu kuzungumza na washiriki wa hafla hiyo, Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati, Mhandisi Zena Said alisema hadi kufikia Oktoba 31, mwaka huu, mradi huo ulikuwa umeshatoa ajira za moja kwa moja 6,364 ambapo kati ya hizo, ajira 5,728 zikiwa ni za Watanzania.

Akielezea hatua iliyofikiwa kwenye usambazaji wa umeme nchini, Katibu Mkuu huyo alisema hadi sasa vijiji 9,884 kati ya 12,264 vilivyopo nchini vimekwishapatiwa umeme.

“Tuna mpango wa kukamilisha vijiji vyote vilivyobakia ndani ya miaka miwili ijayo,” alisema.

Wakati huohuo, Waziri wa Nyumba na Huduma za Mijini wa Misri, Dkt. Assem el Gazzar alisema Rais wa nchi hiyo, Abdel Fattah al-Sisi anafuatilia kwa karibu utekelezaji wa mradi huo ambao unajengwa kwa ubia na kampuni za Arab Contractors and El Sewedy Electric kutoka Misri.

“Rais wetu anafuatilia kwa karibu maendeleo ya mradi huu na tunatarajia utaisha ndani ya muda uliopangwa. Kukamilika kwa mardi huu kutahakikisha nishati ya umeme inakuwa ya uhakika katika kuleta maendeleo,” alisema.

Katika hatua nyingine, Waziri wa Umeme na Nishati Jadidifu wa Misri, Dkt. Mohamed Shaker El-Markabi alisema Serikali ya nchi hiyo iko tayari kubadilishana uzoefu na Wizara ya Nishati ya Tanzania na kwamba itatoa mafunzo kwa Watanzania 25 kwa miaka mitatu ijayo.

“Tunawapongeza Watanzania kwa hatua hii ya kihistoria. Wizara yetu iko tayari kubadilishana uzoefu na kujengeana uwezo na Wizara ya Nishati ya Tanzania, na katika kipindi cha miaka mitatu ijayo, tutatoa mafunzo (full training) kwa Watanzania 25,” alisema.

Alisema upatikanaji wa umeme wa uhakika ni suala la muhimu kwa wananchi kama ilivyo kwa maji na huduma nyingine muhimu.

“Uzalishaji wa megawati 2,115 utaiwezesha Tanzania kuwa na umeme wa uhakika, itaongeza kiwango cha upatikanaji wa umeme na kutengeneza fursa za ajira na za kibiashara.

 “Ndani ya miaka mitatu ijayo, Tanzania itakuwa kinara wa uzalishaji nishati ya umeme katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kati. Mradi wa umeme wa Julius Nyerere (JNHPP) utakapokamilika, unatarajiwa kutoa ziada ya kuuza kwenye nchi za jirani,” alisema.

Mkurugenzi Mkuu wa TANESCO, Dkt. Tito Mwinuka alisema ujenzi wa mradi huo umefikia asilimia 75.76 na kwamba uchepushaji wa maji ya mto uliofanyika sasa ni wa muda tu ili kupisha ujenzi wa tuta kuu.

“Tumekwepesha umbali wa mita 700 tu, na tukimaliza ujenzi wa tuta, tutarudisha maji ya mto kwenye njia yake ya awali,” alisema.