*Asema ameridhishwa na shughuli inavyoendelea
WAZIRI MKUU na Mjumbe wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya
Taifa ya Chama cha Mapinduzi (CCM), Kassim Majaliwa amepiga kura kijijini kwake
Nandagala, wilayani Ruangwa, mkoani Lindi.
Waziri Mkuu ambaye ni mbunge mteule wa jimbo la Ruangwa alipiga
kura kwenye kituo cha Shule ya Msingi Nandagala Jumatano, Oktoba 28, 2020 akiwa
na mkewe Mama Mary Majaliwa.
Akizungumza mara baada ya kupiga kura, Waziri Mkuu alisema shughuli
ya kupiga kura ni haki ya msingi na anamshukuru Mungu imeenda salama.
“Ninamshukru Mungu nimeweza kushiriki haki yangu ya msingi
ya kumchagua kiongozi ninayempenda ili aweze kuliongoza taifa hili.
“Kwa hapa Nandagala, Mbunge na Diwani walishapita bila
kupingwa, kwa hiyo leo nimepiga kura moja tu ya kumchagua Mheshimiwa Rais wa Jamhuri
ya Muungano wa Tanzania,” alisema.
Waziri Mkuu Majaliwa aliwasili kituoni saa 4:20, na
kujipanga foleni yeye na mkewe, alifuata taratibu kama wananchi wengine na alipiga
kura saa 4:53. Aliondoka kituoni hapo saa 5:00 asubuhi.
Akielezea kuhusu utaratibu wa upigaji kura, Majaliwa alisema
shughuli zima ilienda vizuri na aliwapongeza wasimamizi wa kituo hicho kwa
sababu alikuta kuna utulivu na watu wamekaa kwenye foleni wakisubiri kuingia
ndani.
“Nimekuta watu wanafuata utaratibu, wanapatiwa maelekezo,
vitambulisho vinahakikiwa, ni jambo la kujivunia. Amani kwetu bado ni tunu
ambayo hatutakiwi kuidondosha chini ikaharibika. Ninatoa wito kwa Watanzania
tujitokeze tukapige kura ili tupate viongozi wa ngazi zote ambao watatuongoza.
Ni nafasi muhimu, ukiikosa leo, hutaipata tena kwa miaka mitano ijayo,” alisema.

No comments:
Post a Comment