NA MWANDISHI WETU
UONGOZI wa Wakala wa Barabara (Tanroad) Mkoa wa Dar
es Salaam, umesema maagizo ya kisiasa yanayotolewa na wanasiasa kuhusu matumizi
na utunzaji wa miundombinu ya barabara yamekuwa yakikinzana na sheria na
miongozo ya utunzaji barabara.
Kauli hiyo imetolewa na Mkuu wa Idara ya Mipango
Tanroad Mkoa wa Dar es Salaam, Elisony Mweladzi alipofanya mahojiano na
TANZANIA PANORAMA wiki iliyopita kuhusu malalamiko ya wafanyabiashara wa eneo
la Kimara Mwisho kupangishwa vibanda vya biashara vilivyo katika eneo la
Tanroad kwa bei kubwa.
Katika majibu yake, Mweladzi alisema sheria na
miongozo iliyopo hairuhusu mtu yeyote kufanya biashara pembeni ya barabara
hivyo Tanroad haijakodisha eneo lolote lililo pembezoni mwa barabara isipokuwa
wafanyabiashara wamekuwa wakivamia maeneo yaliyo wazi na kuyatumia
kibiashara kwa kufuata maagizo ya kisiasa yanayotolewa na wanasiasa.
"Kwanza nataka ieleweke hakuna mwekezaji eneo
la Kimara mwisho bali kuna wafanyabiashara pale. Kweli lile ni eneo la Tanroad
na imelitoa kwa wafanyabiashara wapatao sita, Wanne upande wa kulia na wawili
wapo upande wa kushoto wa barabara.
"Hawa tumewakodisha maeneo hayo na wanalipa kwa
dola (fedha za marekani) lakini kwa ajili ya maegesho ya magari na siyo kuweka
vibanda vidogo vidogo vya wafanyabiashara wa bidhaa za vyakula na nyinginezo.
" Sasa sisi tunatoa vibali vya kuegesha magari
tu lakini hatuhusiki hata kidogo na vibali vya wafanyabiashara wadogo ndani ya
hifadhi ya barabara. Na tulishachukua hatua hapo awali na kama wapo wengine
basi tutawashughulikia.
"Tatizo linalotukwamisha kusimamia ipasavyo
jambo hili ni matamko ya kisiasa yanayotolewa na viongozi wa kisiasa kwa sababu
hawazingatia sheria, wanawaruhusu kufanya biashara pembezoni mwa barabara jambo
ambalo ni kinyume kabisa cha sheria. Nadhani hata wewe mwandishi unaujua ugumu
wa kusimamia sheria panapokuwa na upinzani kutoka kwa wanasiasa," alisema
Mweladzi.
Awali wafanyabiashara wadogo wa eneo Kimara Mwisho
waliiambia TANZANIA PANORAMA kuwa mwekezaji aliyepewa eneo la pembezoni mwa
barabara na Tanroad anawatoza fedha nyingi za kukodi vibanda vya biashara na
hata wasiokuwa na vibanda nao wanatozwa bila kujali wana vitambulisho vya
wamachinga.
Walisema vibanda vya mbogamboga na mama lishe
vinatozwa kuanzia sh 50,000 hadi 300,000 na wapiga kiwi viatu ambao kikawaida
hawana vibanda wao wanalipia eneo wanaloweka meza sh 45,000 hadi 50,000.
Akijibu hilo, Mweladzi alisema malalamiko hayo
yanashagaza kwa sababu wafanyabiashara hao walipata kufika ofisini kwake
wakimsifia na kumshukuru mfanyabiashara aliyewapa eneo hilo na kuwaruhusu
kufanya biashara bila kuwatoza chochote na waliomba Tanroads inamruhusu
awajengee choo.
TANZANIA PANORAMA lilifika ofisini kwa
mfanyabiashara huyo eneo la Kimara Mwisho na kukutana na wasaidizi wake
walioeleza kuwa bosi wao hayupo hivyo wapewe muda wawasiliane naye kabla ya
kujibu maswali waliyoulizwa.
Wakijibu kwa niaba ya bosi wao walisema, Biashara
yote inayoendelea katika eneo hilo la pembezoni mwa barabara inatambuliwa na
kusimamiwa na Meneja wa Tanroads wa Mkoa wa Dar es Salaam hivyo kuna jambo
lolote linalohitaji ufafanuzi basi aulizwe yeye.
No comments:
Post a Comment