banner

Saturday, October 31, 2020

MAJALIWA AKABIDHIWA CHETI CHA UBUNGE RUANGWA

 

 



Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akipokea cheti cha ushindi wa Ubunge wa Jimbo la Ruangwa kutoka kwa Msimamizi Mkuu wa uchaguzi wa Jimbo hilo, Frank Chonya (kushoto)  kwenye viwanja vya Ofisi ya Mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya  ya Ruangwa, Oktoba 29, 2020. Kulia ni Mke wa Waziri Mkuu, Mama Mary Majaliwa. (Picha na Ofisi  ya Waziri Mkuu)


MWANDISHI WETU

MBUNGE Mteule wa Jimbo la Ruangwa na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa amepokea cheti cha kumtambulisha rasmi kuwa mbunge mteule wa jimbo hilo.

Alipokea cheti hicho Alhamisi, Oktoba 29, 2020 kutoka kwa Msimamizi wa Uchaguzi wa Jimbo la Ruangwa, Frank Chonya katika ofisi za Halmashauri ya Wilaya ya Ruangwa.

Akizungumza mara baada ya kupokea cheti hicho, Majaliwa amesema anamshukuru Mungu kwa kuwezesha yote na kuwafikisha hapo na kuwavusha salama kipindi cha kampeni kwa karibu miezi miwili

Majaliwa ambaye alikuwa ameambatana na mkewe Mama Mary Majaliwa, alisema kipekee anashukuru vyama vya siasa wilayani humo kwa kumuamini na kuthamini maendeleo.

"Sisiti kusema vyama vya siasa vimeendelea kuthamini maendeleo ya wilaya yetu. Lakini katika hili, niseme kwamba tumeliweka mbele sana suala la maendeleo ya wilaya yetu. Ninawashukuru sana."

Alisema kupatiwa cheti cha kumtambua rasmi kuwa mbunge mteule hadi atakapoapishwa, kumetokana na imani yao kubwa waliyoionesha kwake na kuamua apite bila kupingwa.

"Leo niko hapa mbele yenu, nimemaliza muda wangu wa 2015-2020, mmenivumilia, mmenipa ushirikiano na mmenisaidia kuifanya kazi yangu vizuri. Ninawashukuru viongozi wote na wananchi wa Ruangwa kwa mchango wenu uliowezesha Ruangwa ipige hatua ya maendeleo. Mimi, mke wangu na watoto tunawashukuru sana."

Alisema katika miaka mitano iliyopita, yako mambo mengi waliyofanya na katika kipindi hiki yako mambo yaliyobakia kama kupeleka umeme na maji vijijini. "Ninawaahidi kushirikiana nanyi ili kufikia malengo yaliyowekwa na Ilani ya Uchaguzi ya CCM."

Aliwapongeza madiwani wote walioshinda katika kata zote 22 na kuwaahidi kuwa yuko pamoja nao kuijenga Ruangwa.

Mapema, akizungumza kabla ya kumkabidhi cheti chake, Msimamizi wa Uchaguzi wa jimbo la Ruangwa, Frank Chonya alisema jimbo hilo lenye kata 22, lilikuwa na watu waliojiandikisha kupiga kura 106,043 na lilikuwa na vituo 311 vya kupigia kura.

Alisema vyama vilivyoshiriki uchaguzi huo ni CCM, ACT Wazalendo, CUF na CHADEMA.

"Kabla ya uchaguzi, kata saba, wagombea wake kutoka Chama cha Mapinduzi walipita bila kupingwa. Jana baada ya uchaguzi, CCM imeshinda kata 12, ACT kata mbili na CUF kata moja." Alisema.

 

 

 

  

WAZIRI MKUU MAJALIWA APIGA KURA KIJIJINI KWAKE

 


*Asema ameridhishwa na shughuli inavyoendelea

 NA MWANDISHI WETU

WAZIRI MKUU na Mjumbe wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya Chama cha Mapinduzi (CCM), Kassim Majaliwa amepiga kura kijijini kwake Nandagala, wilayani Ruangwa, mkoani Lindi.

Waziri Mkuu ambaye ni mbunge mteule wa jimbo la Ruangwa alipiga kura kwenye kituo cha Shule ya Msingi Nandagala Jumatano, Oktoba 28, 2020 akiwa na mkewe Mama Mary Majaliwa.

Akizungumza mara baada ya kupiga kura, Waziri Mkuu alisema shughuli ya kupiga kura ni haki ya msingi na anamshukuru Mungu imeenda salama.

“Ninamshukru Mungu nimeweza kushiriki haki yangu ya msingi ya kumchagua kiongozi ninayempenda ili aweze kuliongoza taifa hili.

“Kwa hapa Nandagala, Mbunge na Diwani walishapita bila kupingwa, kwa hiyo leo nimepiga kura moja tu ya kumchagua Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,” alisema.

Waziri Mkuu Majaliwa aliwasili kituoni saa 4:20, na kujipanga foleni yeye na mkewe, alifuata taratibu kama wananchi wengine na alipiga kura saa 4:53. Aliondoka kituoni hapo saa 5:00 asubuhi.

Akielezea kuhusu utaratibu wa upigaji kura, Majaliwa alisema shughuli zima ilienda vizuri na aliwapongeza wasimamizi wa kituo hicho kwa sababu alikuta kuna utulivu na watu wamekaa kwenye foleni wakisubiri kuingia ndani.

“Nimekuta watu wanafuata utaratibu, wanapatiwa maelekezo, vitambulisho vinahakikiwa, ni jambo la kujivunia. Amani kwetu bado ni tunu ambayo hatutakiwi kuidondosha chini ikaharibika. Ninatoa wito kwa Watanzania tujitokeze tukapige kura ili tupate viongozi wa ngazi zote ambao watatuongoza. Ni nafasi muhimu, ukiikosa leo, hutaipata tena kwa miaka mitano ijayo,” alisema.

Tuesday, October 27, 2020

DK. MAGUFULI APIGA SIMU, AOMBA KURA NACHINGWEA


NA MWANDISHI WETU

MGOMBEA Urais kwa tiketi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dk. John Pombe Magufuli amepiga simu na kuwaomba wakazi wa Nachingwea wampe kura za ndiyo kesho watakapoenda kupiga kura.

Kesho, Jumatano, Oktoba 28, 2020 ni siku ya uchaguzi mkuu hapa nchini ambapo Watanzania watapata nafasi ya kumchagua Rais, wabunge na madiwani.

Dk. Magufuli ameongea nao leo mchana Jumanne, Oktoba 27, 2020 wakati akizungumza na maelfu ya wakazi wa Nachingwea kupitia simu aliyompigia Mjumbe wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya CCM, Kassim Majaliwa ambaye alikuwa akizungumza na wakazi wa Kata ya Boma katika mkutano uliofanyika viwanja vya Bomani kwenye mji mdogo wa Nachingwea, mkoani Lindi.

Majaliwa leo amehitimisha mikutano ya kampeni ya kumuombea kura mgombea urais kwa tiketi ya CCM, Dk. John Pombe Magufuli kwa kumnadi mgombea ubunge wa Jimbo la Nachingwea kupitia CCM, Dk. Amandus Chinguile na wagombea udiwani wa kata za wilaya hiyo.

“Ninawasalimu sana wana-Nachingwea. Zile changamoto za zao la korosho, ninazijua; zile changamoto za barabara ninazijua na yote hayo tumeyapanga kwenye Ilani yetu. Nilitamani nifike huko lakini nimemtuma Waziri Mkuu wangu mpendwa aje kuniombea kura, yote atakayoyasema ni ya kwangu. Baada ya uchaguzi, nitakuja kuwaona.

“Nawaombeni kura zenu nyingi, nawaomba mumchague mbunge wa CCM na madiwani wa CCM ili tufanye nao kazi. Nataka Nachingwea ibadilike, zile barabara zote tutazijenga kama tulivyoahidi kwenye ilani yetu,” amesema.

Baada ya Rais Dk. Magufuli kuzungumza na wananchi hao, Majaliwa aliwasisitiza wakazi hao wahakikishe kesho wanapiga kura zote za ndiyo kwa mgombea urais, wabunge na madiwani wa CCM ili wapate ushindi wa kishindo.

“Kesho asubuhi, kila mmoja na kadi yake, nenda kapige kura. Wako waliojipanga kununua kadi za wapigakura ili kutunyima ushindi. Kura yako ina thamani sana kuliko hiyo elfu tano atakayokupa. Usikubali kupoteza kura yako.”

Wakati huo huo, mbunge mteule wa Jimbo la Mtama, Nape Nnauye alipopewa nafasi kumuombea kura Dk. Magufuli alisema ana imani kwamba ushindi wa CCM uko dhahiri kwani hapo Nachingwea wakazi wake ni karibu 100,000 lakini wanaCCM peke yake ni 86,000.

“Hawa wanataka kushindana na CCM, sasa hao watashindaje? Kati ya majimbo zaidi ya 200 hapa nchini, tayari tuna majimbo 28 ambayo wagombea wake wamepita bila kupingwa. Tukienda kwenye urais, tuna wapiga kura milioni 29 na kati yao, milioni 18 ni wanaCCM. Je bado wana nafasi ya kushinda? Watapitia wapi?” alihoji.

Aliwataka wakazi hao waache ushabiki wa kisiasa na wajifunze kutoka nchi jirani ambayo wananchi wake walipata maafa baada ya uchaguzi na wagombea wakabakia na makundi

 

  

 

 

MAJALIWA: RAIS MAGUFULI ANATUPENDA, TUMPE KURA ZETU ZOTE ZA NDIYO

 

 

NA MWANDISHI WETU

*Awasihi waweke kando itikadi za vyama, wajali kupata maendeleo

MJUMBE wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya Chama cha Mapinduzi (CCM), Kassim Majaliwa amewataka Watanzania wamchague Dk. John Pombe Magufuli ili awe Rais wa Tanzania.

Alitoa wito huo leo Jumanne, Oktoba 27, 2020 wakati akizungumza na wakazi wa Kata za Nakapanya na Namakambale, wilayani Tunduru, mkoani Ruvuma katika mkutano alioufanya akiwa njiani kuelekea Nachingwea, mkoani Lindi.

“Tupeni viongozi wa CCM ili waweze kukamilisha yale tuliyoaanzisha. Leo saa 10 jioni Rais wetu, Dk. John Pombe Magufuli atazungumza na Taifa kupitia kwenye vyombo vya habari. Tukae tumsikilize, yeye bado ni Rais wetu. Bado anawapenda Watanzania, bado anataka kuwatumikia wananchi wake. Tumpe kura zetu zote za ndiyo.”

Alisema Rais Dk. Magufuli ana dhamira ya kuwaletea maendeleo wananchi na akawataka bila kujali itikadi zao, wampe miaka mingine mitano ili atimize malengo yake katika kuwaletea miradi ya maendeleo. “Hata kama uko ACT, CUF au CHADEMA, mchague Dk. Magufuli sababu maendeleo hayana chama,” alisisitiza.

Majaliwa alikuwa wilayani Tunduru ambako alienda kumuombea kura mgombea urais kwa tiketi ya CCM, Dk. John Pombe Magufuli, mgombea ubunge wa jimbo la Tunduru Kaskazini, Hassan Zidadu Kungu na wagombea udiwani wa kata hizo.

Akielezea utekelezaji wa Ilani iliyokwisha, Majaliwa alisema Serikali ilitoa sh. bilioni 3.4 kwa ajili ya ujenzi wa madarasa, vyoo, mabweni, mabwalo, ukarabati wa shule kongwe za sekondari na uboreshaji wa miundombinu ili wanafunzi wafaulu zaidi.

“Tulileta sh. bilioni 3.4 za kufanya ukarabati kwenye sekondari za Matemanga, Nakapanya, Masonya, Mataka na Tunduru. Tumeanza kujenga mabweni ili watoto walale hukohuko, wasome vizuri na waweze kufaulu,” alisisitiza.

Wakati huo huo, Majaliwa amewataka wakazi hao wajiandae kunufaika na fursa mbalimbali zitakazopatikana kutokana na ujenzi wa reli ya kutoka Mtwara hadi Mbamba-bay.

“Upembuzi yakinifu umekamilika, uchoraji wa ramani umekamilika na hii reli itaanzia Mtwara itapita Mnazi Mmoja hadi Masasi. Itapita hapa Nakapanya, itaenda Namtumbo, Songea mjini, Peramiho hadi Mbamba-bay.”

“Itakuwa reli ya umeme, itabeba abiria na mizigo. Na reli hii ikianza kujengwa, italeta ajira kwa wote katika maeneo yote itakapopita,” alisisitiza.

Katika hatua nyingine, Majaliwa amewataka wakazi wa Tunduru Mjini wakichague Chama Cha Mapinduzi kwa sababu ni chama chenye sera zinazotekelezeka.

Alitoa wito huo jana Jumatatu, Oktoba 26, 2020 wakati akizungumza na wakazi mji wa Tunduru na vitongoji vyake waliofurika kwenye viwanja vya uwanja wa ndege, kata ya Majengo.

“Sera za CCM zinatekelezeka kwa sababu ziko kwenye Ilani. Mafanikio yote haya mnayoyaona, yaliainishwa kwenye ilani. Ile imekwisha na sasa tumekuletea ilani nyingine ya uchaguzi yenye muendelezo wa yale yaliyobakia.”

Aliwataka wakazi hao wasikubali kugawanywa kwa misingi ya ukanda, ukabila wala udini.

 

 

 

HATUENDI KWENYE UCHAGUZI KWA JAZBA - MAJALIWA

 

 

NA MWANDISHI WETU

 MJUMBE wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya Chama cha Mapinduzi (CCM), Kassim Majaliwa amewataka Watanzania wasichague kiongozi kwa sababu ya jazba au hasira.

Alitoa wito huo leo Jumatatu, Oktoba 26, 2020 wakati akizungumza na wakazi wa Kata ya Nalasi, wilayani Tunduru, mkoani Ruvuma katika mkutano uliofanyika kwenye viwanja vya Katani.

Majaliwa alizuru Wilaya ya Tunduru akimuombea kura mgombea urais kwa tiketi ya CCM, Dk. John Pombe Magufuli.

“Hatuendi kwenye chama kwa jazba wala kwa hasira. Hatari ya kipindi hiki unaweza kujikuta unaenda kwenye chama ambacho hakina sera wala hakieleweki. Chama makini kinapaswa kuwa na viongozi wanaoeleweka,” alisema.

Akitoa mfano, Majaliwa alisema leo hii kuna chama viongozi wake wamegombana na wala hakina mgombea urais. “Je ukikichagua chama hiki na ukawa na changamoto inakukabili, utaipeleka wapi? Au utampelekea nani? Na ukimchagua diwani au mbunge wa chama hicho, hayo masuala yako atayawakilisha kwa nani?”

“Ninawasihi, unapochagua viongozi, usichague chama kwa sababu maendeleo hayana chama. Chagueni chama ambacho kina mwelekeo na kinajali kutatua shida za watu. Ukienda kupiga kura, chagua diwani, mbunge na Rais anayetoka Chama cha Mapinduzi. Keshokutwa, tumchague Dk. Magufuli kwa kura nyingi za ndiyo,” alisisitiza.

Majaliwa yuko wilayani Tunduru ambako alienda kumuombea kura mgombea urais kwa tiketi ya CCM, Dk. John Pombe Magufuli, mgombea ubunge wa Jimbo la Tunduru Kusini, Adimu Mpakate na wagombea udiwani wa kata nne za jimbo hilo.

Akiwa njiani kuelekea Tunduru, Majaliwa alifanya mkutano wa hadhara katika viwanja vya stendi ya mabasi ya Mangaka, wilayani Nanyumbu mkoani Mtwara.

Akizungumza na wakazi wa Mangaka, aliwasihi Watanzania wasikubali kuandamana kwa kisingizio cha kutokubali matokeo ya uchaguzi kwa sababu huko ni kuvunja sheria.

“Ninawasihi vijana mjihadhari, msikubali kuandamana kwani mtakuwa mnavunja sheria na mtajikuta mnajiingiza matatizoni. Kuna mtu anakuja hapa na anatulazimisha kuandamana, huyo hafai kuwa Rais wa nchi.”

Majaliwa alitumia fursa hiyo kumuombea kura mgombea urais kwa tiketi ya CCM, Dk. John Pombe Magufuli, mgombea ubunge wa Jimbo la Nanyumbu, Yahya Muhata na wagombea udiwani wa kata zote za jimbo hilo.

 

 

MAJALIWA: ZIMEBAKI SIKU SABA TU, TUWE MAKINI

 

 

NA MWANDISHI WETU

MJUMBE wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), Kassim Majaliwa amewataka wananchi wa Mtwara wawe makini kuamua wanataka kiongozi wa aina gani kwasababu zimebakia siku saba tu kabla ya uchaguzi mkuu.

"Zimebaki siku saba tu ndugu zangu kabla ya siku ya uchaguzi. Lazima tuwe makini na tutafakari ni aina gani ya kiongozi tunamtaka," alisema.

Alitoa wito huo leo (Jumanne, Oktoba 20, 2020) wakati akizungumza na wakazi wa Kitangari, Wilayani ya Newala kwenye mkutano uliofanyika stendi kuu ya Newala.

Majaliwa ambaye yuko mkoani Mtwara kumuombea kura mgombea Urais kwa tiketi ya CCM, Dk. John Pombe Magufuli, alitumia fursa hiyo kumnadi mgombea ubunge wa Jimbo la Newala Vijijini,  Maimuna Mtanda na mgombea udiwani wa Lata ya Kitangari, Mfaume Ladda.

Amesema wananchi wanapaswa kuamua aina ya kiongozi wa kumchagua ili aweze kuleta maendeleo ya haraka. "Maendeleo hayana chama sababu tukijenga shule watasoma watoto wetu wote. Kwa hiyo, nawaomba sana tumchague Dk. Magufuli ili aje aendeleze mazuri aliyoyaanzisha."

Kuhusu uboreshwaji wa miundombinu, Majaliwa alisema upanuzi wa Bandari ya Mtwara unaendelea ambapo sh. bilioni 170 zilitolewa na Serikali ili ujenzi wa kitako kikubwa cha kuweza kuweka mizigo na magari zaidi ya 600 ufanyike.

"Vilevile sh. bilioni 50 zimetolewa kwa ajili ya upanuzi wa Uwanja wa Ndege wa Mtwara ili uweze kupokea moja kwa moja ndege kubwa kutoka Ulaya bila kulazimika kutua kwanza Dar es Salaam."

Kuhusu ujenzi wa barabara ya lami, Majaliwa alisema Serikali ilitoa sh. bilioni 89 kwa ajili ya ujenzi wa barabara yenye urefu wa km. 210 ambayo itaunganisha wilaya nne na itaanzia Mtwara Vijijini - Nanyamba - Newala - Masasi.

Kuhusu zao la Korosho, Majaliwa alisema mfumo wa mnada ulisaidia bei ya korosho ipande na kufikia sh.4,000/- lakini msimu uliopita bei ilizorota kwa sababu ya ugonjwa wa Corona.

"Wanunuzi wa ndani walipanga kununua Korosho kwa sh. 1,800/- lakini Mheshimiwa Rais aliamua kutoa sh. bilioni 900 ili zitumike kulipia ununuzi wa korosho za wakulima.

Majaliwa ambaye awali alisimamishwa na wananchi wa Kata ya Mkwiti, alisema Serikali imetoa sh. milioni 600 kufanya upembuzi yakinifu wa barabara ya kutoka Mtama hadi Tandahimba kupitia Mkwiti ikiwa ni utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM.

“Kukamilika kwa ujenzi wa barabara ya Mtama hadi Tandahimba kutasaidia kuboresha biashara na usafiri baina ya maeneo hayo na Jiji la Dar es Salaam.”

Pia alimuombea kura mgombea Urais kwa tiketi ya CCM, Dkt. John Pombe Magufuli, na kumnadi mgombea ubunge wa jimbo la Tandahimba kwa tiketi ya CCM, Katani Ahmad Katani na mgombea udiwani wa kata ya Mkwiti, Ismail Iddi Said.

 

 

 

 

 

 

 

Sunday, October 18, 2020

MAABARA NA KLINIKI ZA MIFUGO KUANZISHWA WILAYA ZA WAFUGAJI - MAJALIWA

 


NA MWANDISHI WETU

MJUMBE wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya Chama cha Mapinduzi (CCM), Kassim Majaliwa amesema serikali ijayo ya CCM itaanzisha maabara na kliniki za kutibu mifugo katika wilaya zote za wafugaji nchini, ikiwa ni utekelezaji wa Ilani ya CCM ya mwaka 2020-2025.

Ametoa kauli hiyo leo wakati akizungumza na wakazi wa Kata ya Orgosorok, Wilaya ya Ngorongoro, Mkoa wa Arusha, katika mkutano uliofanyika kwenye uwanja wa Waziri Mkuu, mji mdogo wa Loliondo.

"Tumeanza kuwatumikia na kuwahudumia wafugaji kwa kuhakikisha kuwa wana maeneo mazuri ya malisho, na sasa tumeamua kuwachimbia mabwawa ya kunywesha mifugo.

"Bado tutaendelea kubaini maeneo ya wafugaji na kuwachimbia mabwawa na majosho. Na sasa, tunaanzisha maabara kwa ajili ya kupima magonjwa ya mifugo. Tunajenga kliniki kwa ajili ya kutibu mifugo kwenye wilaya zote zinazofuga na pia tunatoa dawa ya ruzuku kwa ajili ya mifugo," amesema.

Amesema Serikali ya CCM itaendelea kuweka mazingira mazuri ya kuhudumia mifugo na hivyo, wafugaji waendelee kufuga kwa uhakika ili Watanzania wanufaike na sekta ya mifugo.

Kuhusu barabara, Majaliwa amesema Serikali ijayo ya CCM itajenga kwa kiwango cha lami barabara yenye urefu wa km. 300 kutoka Mto wa Mbu hadi Ngorongoro.

Majaliwa amewaomba wananchi wa Ngorongoro wamchangue tena Dk. John Magufuli ili aendelee kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwani katika kipindi cha miaka mitano iliyopita, ameonyesha uwezo mkubwa katika kukusanya mapato ya Serikali na kusimamia matumizi yake.

Amesema: “Kazi ya Urais ni kazi nzito na haina nafasi ya kufanyiwa majaribio na mtu ambaye hana historia na uongozi wa nchi,” na kusisitiza kuwa: “Amani ya nchi inategemea kwa kiwango kikubwa na kiongozi aliyeko madarakani, kwani akiwa kiongozi mahiri ataisimamia amani iliyopo, na akiwa kiongozi legelege amani itayumba.”

Wakati huohuo, Mama Mary Majaliwa amewaomba wakazi wa Ngorongoro wampe kura zote za ndiyo Dk. John Pombe Magufuli, mgombea ubunge wa Jimbo la Ngorongoro William Ole Nasha na wagombea udiwani wote kwa tiketi ya CCM.

Naye mgombea ubunge wa Jimbo la Ngorongoro kwa tiketi ya CCM, William Tate Ole Nasha amesema maendeleo yaliyopatikana katika kipindi cha awamu ya kwanza ya miaka mitano ya Dk. Magufuli ni makubwa na hakika historia ya maendeleo imeandikwa katika Wilaya ya Ngorongoro.

“Kwa mara ya kwanza, Chuo cha Ufundi VETA kinajengwa Ngorongoro na Serikali imetoa shilingi bilioni 1.5 kwa ajili ya ujenzi wa chuo hicho katika eneo la Samunge, Loliondo," amesema.

Ole Nasha amesema Serikali imetoa shilingi bilioni 2.2 kwa ajili ya ujenzi wa hospitali ya wilaya na hivyo kurahisisha upatikanaji wa huduma za afya kwani wananchi wa Ngorongoro hawatalazimika kwenda Arusha au nchi jirani ili kupata matibabu.

Majaliwa yuko mkoani Arusha kumuombea kura mgombea urais kwa tiketi ya CCM, Dk. John Pombe Magufuli, mgombea ubunge wa Jimbo la Ngorongoro, William Ole Nasha na wagombea udiwani kwa tiketi ya CCM.

 

Saturday, October 17, 2020

POLISI WALIA UKATA

 

NA MWANDISHI WETU

ASKARI Polisi wa Kituo Kidogo cha Polisi Mtongani kilichopo Mkoa wa Kipolisi wa Kinondoni jijini Dar es Salaam wameeleza kuwa wanakabiliwa na ukata mkali unaokwamisha utekelezaji wa majukumu yao ya kulinda usalama wa raia na mali zao.

Wameeleza hayo baada ya Tanzania PANORAMA Blog kuhoji sababu za mafaili ya kesi zilizofunguliwa kituo kidogo cha Polisi Mtongani kushindwa kupelekwa Kituo cha Polisi Kawe kwa zaidi ya siku tano.

Akijibu swali la mmoja wa walalamikaji jana asubuhi lililohoji; kwanini mafaili ya kesi zilizofunguliwa hayajapelekwa Kawe kwa zaidi ya siku tano wakati siyo mbali, mmoja wa askari aliyekuwa kituo hapo alisema "muzee walishindwa tu kukwambia ukweli, hali ni mbaya, tuna hali mbaya hadi usafiri wa kupeleka mafaili hapo Kawe hatuna."

Alipoambiwa kuwa mlalamikaji yupo tayari kuwasaidia polisi usafiri wa kubeba faili hizo kuzipeleka Kituo cha Polisi Kawe kwa sababu amesumbuka muda mrefu na anatumia gharama kuzunguka vituo vya polisi Kawe na Mtongani, polisi huyo alisema hilo haliruhusiwi ila atajitahidi kutafuta njia ya kuyapeleka mafaili hayo.

Dalili za kuwepo kwa ukata kwa polisi hao zilianza kuonekana Jumamosi ya Oktoba 10, 2020 baada ya Mwandishi wa Tanzania PANORAMA Blog kufika kituo kidogo cha Polisi Mtongani akiwa amejeruhiwa vibaya na wezi waliokuwa wamewateka abiria kwenye daladala na kuwashambulia kwa bisibisi na mapanga kabla ya kuwanyang'anya pesa, simu na vitu vingine vya thamani walivyokuwa navyo kisha kuwatupa pembezoni mwa barabara.

Mwandishi wetu aliwaeleza polisi hao kuwa alipanda daladala la wahalifu akiwa na abiria wenzake wawili katika kituo cha daladala cha njia panda ya kwenda Hotel ya Bahari Beach ambapo mmoja wa wahalifu alikuwa ametangaza kuwa linakwenda stendi ya Makumbusho.

"Hatukujua kama ndani ya daladala hilo kulikuwa na wahalifu, mmoja wao alitangaza kuwa linakwenda Makumbusho hivyo mimi na abiria wenzangu wawili tukapanda pale kituo cha kona ya kwenda Bahari Beach. Lakini lilipoondoka tu wale wezi ambao walikuwa zaidi ya 20 mle ndani wakaanza kupiga kelele kama washangiliaji wa mpira na dreva akawasha muziki kwa sauti ya juu ikawa kelele tu.

" Hapo wakaanza kutushambulia, walianza na mama tuliyepanda naye akawa anakataa kuachia pochi yake, wakamkata panga mkononi ukabaki unaning'inia, wakachukua kila kitu wakamsogeza mwisho kabisa wa gari na kijana mwingine niliyepanda naye yeye alikuwa amekatwa mapanga mawili kichwani na kuwapa kila kitu akabaki analia tu.

"Mimi nilijaribu kumwambia dreva apunguze sauti ya muziki ajabu alitoa upanga akanambia tulia kisha akaendelea kuendesha gari kwa kasi. Kwa sababu mlango wa gari ulikuwa umefungwa na taa zilikuwa zimezimwa niliiona hatari iliyokuwa mbele, sikuwa mbishi niliwapa pesa, simu nao walinisachi na kuchukua kila walichoona kinafaa.

" Walinishambulia kwa ngumi tu lakini walinijeruhi vibaya usoni na mdomoni nadhani kwa sababu sikuwa mbishi na walikwenda kunitupa Kona ya Mbuyuni wakawa wameondoka na mama ambaye wamemkata mkono, namba ya gari nimeikariri ina mstari wa njano ya wekundu wa damu ya mzee, tukiifukuza tunaikamata kwa sababu nimeona huko mbele kuna foleni," alijieleza mwandishi wetu mbele ya kaunta ya polisi.

Polisi aliyekuwa akisikiliza maelezo yake alisema hawana uwezo wa kuifukuza daladala hiyo kwa sababu eneo hilo la kipolisi hadi Kawe lina gari moja tu bali anamfungulia RB na atampa PF 3 akatibiwe kwa sababu alikuwa akivuja damu nyingi.

"Hatuna jinsi ya kulifukuza mzee tuna gari moja tu nalo muda huu linasambaza askari kwenye malindo, we acha kumzungumzia mama aliyekatwa mkono naye watamtupa huko mbele atakwenda kutoa taarifa kituo chochote cha polisi kama ulivyofanya wewe.

" Nakufungulia faili nakupa PF 3 nenda Hospitali ukatibiwe angalia tisheti yote ulivyoloa damu, jihurumie umeumua sana acha kuhurumia wengine.

"Kwa sababu umetutajia namba na rangi za mstari wa hilo daladala Jumatatu tu tutalikamata.  Hao wahalifu wamekuwa tishio huwa wanaenda beach huko kila weekend kufanya uhalifu msiwe mnapanda daladala zao maana ndiyo mbinu yao mpya.

"Katibiwe nenda nyumbani kasikilizie hali yako Jumatatu asubuhi saa mbili uwe polisi Kawe utamkuta mpelelezi wa kesi yako, kesho jumapili hakuna kazi hivyo jumatatu litakamatwa hilo daladala," alisema askari aliyekuwa kaunta.

Jumatatu, Oktoba 12, 2020, saa tano asubuhi mwandishi wetu alifika Kituo cha Polisi na kuonyesha RB namba KMT/RB/2428/2020 aliyopewa kituo kidogo cha Polisi Mtongani ili aonyeshwe mpelelezi wa kesi yake lakini polisi aliyekuwa kaunta alisema mafaili kutoka Mtongani hayajafika kituoni hapo wala hakuna kumbukumbu zake zilizorekodiwa kwenye rejista kituoni hapo na kuelekezwa arudi Mtongani kesi yake itashugulikiwa huko.

Alhamis, Oktoba 16, 2020 mwandishi wetu alirejea kituo cha Polisi Mtongani ambako baada ya polisi kukagua makaratasi mengi yaliyokuwa kaunta walisema faili lake bado lipo kituoni hapo likisuburi utaratibu wa kupelekwa Polisi Kawe.

"Siyo peke yako mzee, faili zote hizi hazijapelekwa hali mbaya, hakuna usafiri.  Wewe uwe unapitapita pale Polisi Kawe siku tukilipeleka utalikuta ataambiwa," alisema askari aliyekuwa kaunta.

Alipoelezwa kuwa kwa sababu ya kupunguza usumbufu na gharama za usafiri na pia kuokoa muda anaweza kutoa msaada wa usafiri ili mafaili hayo yapelekwe Kawe aliambiwa hilo haliruhusiwi.

Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Kipolisi Kinondoni, Camillius Wambura alipotafutwa jana kwa simu yake ya kiganjani kuzungumzia ukata huo alipokea msaidizi wake na kueleza kuwa yupo kwenye kikao atafutwe muda mwingine.

Alipotafutwa leo alipokea simu na kueleza kuwa hasikii vizuri anachoulizwa pengine yupo eneo baya hivyo atumiwe ujumbe na alipotumiwa ujumbe kwenye simu yake akiulizwa kuhusu kuwepo ukata katika eneo lake la utawala na kukwama kwa mafaili ya kesi kituo cha Polisi Mtongani kwa siku tano, hakujibu.